Baba Mtakatifu Francisko amewasili mjini Manila, Ufilippini siku ya Alhamisi tarehe
15 Januari 2015 na kupokelewa kwa heshima na taadhima na kwenye Uwanja wa Ndege wa
Villamour, Manila. Umati mkubwa wa watu ulikuwa umejipanga kwenye viunga vya mji wa
Manila, ili kumpokea na kumsalimia Baba Mtakatifu Francisko anapoanza hija yake ya
kitume nchini Ufilippini.
Hii ni mara ya tano kwa Ufilippini kutembelewa na
Khalifa wa Mtakatifu Petro. Itakumbukwa kwamba, mara ya kwanza Ufilippini ilitembelewa
na Mwenyeheri Paulo VI, miaka 45 iliyopita, baadaye Mtakatifu Yohane Paulo II akatembelea
Manila kunako mwaka 1981 na mwaka 1995. Baba Mtakatifu anafanya hija hii kama kielelezo
cha mshikamano na upendo kwa wananchi wa Ufilippini ambao wametikiswa vibaya sana
na majanga asilia, kiasi cha kuendelea kuwatumbukiza watu wengi katika umaskini wa
hali na kipato.
Kardinali Luis Antonio Tagle, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la
Manila anasema, Baba Mtakatifu Francisko katika hija yake ya kitume nchini mwao anataka
kukutana na kuzungumza na maskini na wale wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii,
ili kuwaonjesha huruma na upendo wa Mungu kwa waja wake; ni hija inayokazia majadiliano
ya kidini na kiekumene kama sehemu ya mchakato wa Uinjilishaji mpya Barani Asia.
Kardinali
Tagle anasema katika maandalizi ujio wa Baba Mtakatifu nchini humo, wamejitahidi kuwa
na kiasi kwa kutambua mtindo na mfumo wa maisha ya Baba Mtakatifu Francisko, mtu asiyependa
makuu! Anakuja kuwafariji ndugu zake katika shida na magumu, ili aweze kuwaimarisha
katika imani, matumaini na mapendo. Mapokeo ya Baba Mtakatifu ni changamoto inayowataka
waamini na watu wenye mapenzi kujenga utamaduni wa kuwajali na kuwahudumia maskini
na wahitaji.
Fedha itakayobakia katika maandalizi ya ujio wa Baba Mtakatifu
itatumika kwa ajili ya kuwahudumia maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii.
Baba Mtakatifu anataka kuwaimarisha ndugu zake katika imani, kwa kuwasikiliza na kusali
pamoja nao, kwa kutambua kwamba, umri wa Baba Mtakatifu pia umekwenda, kumbe anahitaji
mapumziko. Kardinali Luis Antonio Tagle anasema, Baba Mtakatifu yuko nchini Ufilippini
ili kukutana na Familia ya Mungu sanjari na kuwasikiliza maskini!
Na Padre
Richard A. Mjigwa, C.PP.S Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.