Balozi wa Algeria ambaye amemaliza muda wake wa utumishi nchini Tanzania, Mheshimiwa
Tabat Jallouh amewatakia Watanzania mwaka 2015 uwe ni mwaka wa mafanikio, amani na
utulivu, kwa kadri nchi inavyopitia katika mabadiliko makubwa ya kisiasa kwa njia
ya kura ya maoni ya Katiba Mpya na Uchaguzi Mkuu. Mheshimiwa Jallouh alitoa salamu
zake hizo kwa Watanzania usiku wa kuamkia, Jumatano, Januari 14, 2015, wakati alipokuwa
anaagana na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete,
Ikulu, Dar es Salaam.
Balozi Jallouh alimwambia Rais Kikwete kuwa anasikitika
kuondoka mapema bila kuwa shuhuda na shahidi wa matukio hayo muhimu katika historia
na uhai wa taifa la Tanzania.
“Nakutakia wewe binafsi, Mheshimiwa Rais na
kupitia kwako, Watanzania wote, mwaka wenye utulivu, mafanikio na amani kwa kadri
nchi inavyopita kipindi cha kutunga Katiba Mpya na Uchaguzi Mkuu. Ni matukio muhimu
sana katika historia na uhai wa taifa la Tanzania,” alisema Balozi Jallouh, ambaye
pia alimtakia Rais Kikwete maisha marefu na shughuli zenye mafanikio baada ya kustaafu. Balozi
Jallouh ambaye Tanzania ilikuwa nchi ya kwanza Kusini mwa Jangwa la Sahara kuitumikia
katika utumishi wake wa kibalozi, amekuwa Balozi wa Algeria katika Tanzania kwa miaka
mitano.
Naye Rais Kikwete amemshukuru Balozi Jallouh kwa kuinua kwa kiwango
kikubwa uhusiano wa Tanzania na Algeria. “Tunakushukuru kwa utumishi wako, tunakushukuru
kwa kutuunga mkono, tumekuwa marafiki wa miaka mingi lakini wewe umetoa mchango wa
pekee. Tutakukumbuka daima.”