2015-01-14 14:54:43

Jipatanisheni ili kujenga umoja na udugu!


Baba Mtakatifu Francisko mara baada ya kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu na kumtangaza Padre Joseph Vaz kuwa Mtakatifu, Jumatano tarehe 14 Januari 2014 alielekea kwenye Madhabahu ya Bikira Maria wa Rozari Takatifu Madhu, kwa ajili ya kusali na kumshukuru Mungu kwa matendo makuu katika maisha na utume wa Kanisa nchini Sri Lanka. Katika madhabahu haya, wananchi na waamini wa dini mbali mbali wanajisikia kuwa nyumbani na kwamba, hapa wanapendwa na Mama!

Tukio hili limehudhuriwa na umati mkubwa wa watu ambao bado wanakumbuka mateso na madhulumu waliyokumbana nayo katika historia ya nchi yao. Ibada hii imefanyika pembeni mwa Sanamu ya Bikira Maria wa Rozari Takatifu wa Madhu, iliyopelekwa nchini Sri Lanka wakati wa kupandikiza mbegu ya Ukristo.

Familia nyingi zimeendelea kuwa na ibada kwa Bikira Maria anayewalinda wananchi wa Sri Lanka katika shida na magumu mbali mbali, kwani daima yuko karibu na Mwanaye Mpendwa, Yesu Kristo aliyesulubiwa, akafa na kufufuka ili kumkomboa mwanadamu kutoka katika lindi la dhambi na mauti!

Baba Mtakatifu katika tafakari yake, anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kumshukuru Bikira Maria aliyewapatia zawadi ya Yesu Kristo anayewakirimia ujasiri wa kujikita katika mchakato wa ujenzi wa amani katika mioyo yao. Baada ya chuki, kinzani, vita na uharibifu mkubwa, kuna haja ya kumshukuru Bikira Maria, ili awakirimia daima Yesu Kristo anayeweza kuponya madonda na kuipatia tena amani mioyo iliyovunjika na kupondeka.

Baba Mtakatifu anasema, ni pale tu ambapo, watu wanaweza kutambua uwezo wao na jinsi ambavyo wameshiriki katika mambo yote haya, tayari kutubu na kuomba msamaha, ili kupokea neema ya kuweza tena kukaribiana na jirani kwa moyo wa toba ya kweli, ili kutafuta upatanisho wa kweli. Waamini wanahamasishwa kuomba huruma na neema ya Mungu, ili kupata msamaha wa dhambi zao. Yote haya yanaweza kufahamika kwa mwanga wa Msalaba wa Kristo unaowajalia tena neema ya kutubu na kuanza mchakato wa upatanisho wa kweli, kama sehemu ya jitihada za kufikia amani ya kweli.

Baba Mtakatifu Francisko mwishoni anawaombea, ili Bikira Maria awasaidie wananchi wote wa Sri Lanka kujenga na kudumisha umoja wa kitaifa, kwa kutambua kwamba, wote ni ndugu wamoja wanaoweza kwenda nyumbani kwa Baba ili kujipatanisha sanjari na ujenzi wa umoja na udugu.

Wakati huo huo, Askofu Joseph Rayappu wa Jimbo Katoliki la Mannar amemshukuru Baba Mtakatifu Francisko kwa kuwa ni hujaji na mjumbe wa amani inayojikita katika ukweli, haki na upatanisho. Anampongeza kwa kuwajali na kuwapenda maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii. Mannar ni mahali ambapo kuna Wakristo wengi waliomwaga damu yao kutokana na chuki za kidini, kiasi kwamba, damu ya mashuhuda hawa imekuwa kweli ni mbegu ya Ukristo nchini Sri Lanka.

Madhabahu ya Madhu yana utajiri mkubwa wa kihistoria, kwani yalijengwa zaidi ya miaka 400 iliyopita; mahali ambapo watu walikimbilia kupata faraja wakati wa madhulumu; pakawa ni mahali pa kukuza na kudumisha imani na ibada kwa Bikira Maria. Ni madhabahu yanayohamasisha miito mbali mbali ndani ya Kanisa. Ni mahali ambapo umati mkubwa wa waamini unafurika kwa ajili ya Ibada kwa Bikira Maria.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.