2015-01-14 09:35:56

Hospitali ya Bambino Gesù: Prof. Profiti ang'atuka kutoka madarakani!


Professa Giuseppe Profiti, aliyekuwa Rais wa Hospitali ya Bambino Gesù. inayomilikiwa na kuendeshwa na Vatican, ameamua kung'atuka kutoka madarakani, ifikapo tarehe Mosi, Aprili 2015. Anasema, katika kipindi cha miaka saba ya uongozi wake katika Hospitali ya Bambino Gesù, anamshukuru Mungu kwa mafanikio makubwa yaliyopatikana na kwamba, anachukua fursa hii pia kuwashukuru na kuwapongeza wafanyakazi na wadau mbali mbali waliowezesha Hospitali ya Bambino Gesù kupata mafanikio makubwa kiasi hiki!

Professa Profiti anasema, umefika muda wa kuangalia kwa imani na matumaini changamoto nyingine zilizopo katika maisha na kutoa nafasi kwa kiongozi mwingine ili kuendeleza mafanikio pamoja na kufanya maboresho mengine zaidi. Itakumbukwa kwamba, tangu mwaka 2008 Professa Profiti aliteuliwa kuwa Rais wa Hospitali ya Bambino Gesù na tangu wakati huo kumekuwepo na maendeleo makubwa katika huduma ya tiba na tafiti, kiasi cha kuwa ni kituo kikuu cha tiba kwa watoto wadogo Barani Ulaya.

Hospitali ya Bambino Gesù imeendelea kushirikiana kwa karibu na wadau wengine katika huduma ya watoto wadogo huko Cambodia, Vietnam na Tanzania, hususan kwenye Hospitali ya Mtakatifu Gaspar, Itigi, Tanzania, ambako sasa watoto waliokuwa wanalazimika kupelekwa Italia kwa ajili ya tiba ya magonjwa ya moyo, wanaweza kutibiwa Hospitalini hapo.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.