2015-01-13 10:35:50

Waandishi 76 wako kwenye Msafara wa Papa Sri Lanka!


Baba Mtakatifu Francisko wakati akiwa njiani kuelekea nchini Sri Lanka, amewatakia matashi mema, heri na baraka waandishi wote ambao wako kwenye msafara wake huko Sri Lanka na baadaye Ufilippini, kwani wanayo kazi kubwa mbele yao ili kuhakikisha kwamba, watu wanaweza kusikia kwa ufasaha yale yanayojiri katika hija yake ya kitume Barani Asia.

Kabla ya kusalimiana na mwandishi mmoja mmoja na kubalishana naye mawili matatu; Padre Federico Lombardi, Msemaji mkuu wa Vatican amemwambia Baba Mtakatifu kwamba, msafara wake una ambatana na waandishi wa habari 76 na kati yao 14 wanatoka nchini Ufilippini, kwani kuna umati mkubwa wa watu wanaotarajia kusikia mengi wakati Baba Mtakatifu atakapowatembelea nchini mwao kuanzia tarehe 16 Januari 2015 hadi tarehe 19 Januari 2015 atakaporejea tena mjini Vatican.

Kuna waandishi wawili wa magazeti kutoka Ufaransa ambao hawakuweza kushiriki katika msafara wa Baba Mtakatifu kutokana na sababu za kiufundi, zilizowalazimu kubaki nchini Ufaransa baada ya matukio ya kigaidi yaliyoutikiza ulimwengu hivi karibuni.

Wakati huo huo, Baba Mtakatifu Francisko hakuweza kuzungumza na Baraza la Maaskofu Katoliki Sri Lanka kama ratiba ilivyopangwa kutokana na muda kuwatupa mkono na hivyo kulazimika kwenda kupata chakula cha mchana kwenye Ubalozi wa Vatican na Kardinali Pietro Parolin pamoja na msafara mzima wa Baba Mtakatifu kushiriki chakula cha mchana pamoja na Maaskofu Katoliki Sri Lanka.

Baba Mtakatifu Francisko akiwa njiani kutoka Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Colombo kuelekea kwenye Ubalozi wa Vatican nchini Sri Lanka, umbali wa kilometa 28, amekutana na umati mkubwa wa watu uliokuwa umejipanga pembeni mwa barabara, kumshangilia wakati alipokuwa anapita.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.