Majadiliano ya kidini na kiekumene yajenge na kudumisha ushirikiano
Baba Mtakatifu Francisko, Jumanne jioni tarehe 13 Januari 2015 amekutana na kuzungumza
na viongozi wa dini mbali mbali walioko nchini Sri Lanka. Itakumbukwa kwamba, nchi
hii inaundwa na waamini wa dini ya Kibudha, Kihindu, Kiislam na Kikristo. Ni hija
ambayo inajikita katika hija inayofanywa na Mama Kanisa katika mchakato wa kuheshimu
na kuwapenda watu na imani na tamaduni zao, kama alivyofanya Mwenyeheri Paulo VI na
Mtakatifu Yohane Paulo II.
Baba Mtakatifu anasema, katika hija hii anapenda
kuwaimarisha Wakatoliki katika imani, kwa kushiriki nao katika furaha na mahangaiko
yao. Anapenda kushirikishana na viongozi wakuu wa dini mbali mbali, hekima, ukweli
na utakatifu wa maisha. Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican wameonesha heshima
kwa dini mbali mbali na kwamba, Kanisa linapenda kushirikiana na wote kwa ajili ya
mafao ya wengi nchini Sri Lanka.
Baba Mtakatifu anasema, anapenda kwa namna
ya pekee kabisa kuimarisha na kudumisha mchakato wa majadiliano na ushirikiano wa
kidini na kiekumene, kwani, ufanisi wa majadiliano na utamaduni wa watu kukutana unahitaji
watu kushirikishana imani yao, katika ukweli, uwazi na uaminifu, ili hatimaye, kutambua
mambo msingi ambayo yanawaunganisha na kuwaimarisha katika umoja. Hapa kutakuwepo
na njia mpya zitakazosaidia watu kuheshimiana, kushirikiana na kudumisha urafiki.
Baba
Mtakatifu anasema, kuna haja kwa watu wenye mapenzi mema kutoa kipaumbele cha kwanza
katika majadiliano na ushirikiano katika medani mbali mbali za maisha ya wananchi
wa Sri Lanka. Kwa miaka mingi watu wengi wameteseka kutokana na vita vya wenyewe kwa
wenyewe pamoja na kinzani. Sasa kuna haja ya kuanza mchakato wa upatanisho na umoja
wa kitaifa kwa kuondokana na kinzani pamoja na migawanyiko kati ya watu. Mafao ya
wengi na mahitaji ya familia ya binadamu, yapewe nafasi ya kwanza.
Ni matumaini
ya Baba Mtakatifu Francisko kwamba, majadiliano na ushirikiano wa kidini na kiekumene,
yatamiwlishwa katika uhalisia watu kwa kujenga na kudumisha utulivu unaojikita katika
udugu, kwani kwa kufanya hivi hakuna mtu au kikundi kinachoweza kupoteza utambulisho
wake wa kikabila na kidini.
Baba Mtakatifu anasema, kuna changamoto na mahitaji
makubwa yanayoweza kutekelezwa katika mazingira ya mshikamano na ushirikiano. Haya
ni mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili na hasa katika kipindi hiki ambacho familia
nyingi zinakumbana na athari za mtikisiko wa uchumi kimataifa, kuna ongezeko kubwa
la umaskini, watu kuendelea kutengwa na wengine kuomboleza kutokana na kuondokewa
na ndugu na jamaa zao.
Baba Mtakatifu anasema, wakati huu katika historia
ya Sri Lanka, wananchi wengi wanasubiri kuona mchakato wa ujenzi wa msingi wa maadili
kijamii. Ushirikiano kati ya viongozi mbali mbali wa dini unaweza kuwa ni alama na
kielelezo makini cha upatanisho kwa wananchi wote wa Sri Lanka, katika jitihada za
kupyaisha jamii na taasisi zake.
Baba Mtakatifu Francisko anasema, si vyema
kukufuru kwa kutumia dini kuhalalisha vita na kinzani. Hapa viongozi wa kidini wanapaswa
kuwa wakweli na makini, ili kuongoza jumuiya katika njia ya amani kwa kulaani kwa
macho makavu matendo ya vurugu na vita yanapojitokeza.
Na Padre Richard A.
Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican