Kardinali Gerhard L. Muller, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Mafundisho Tanzu ya
Kanisa katika hotuba yake kwa Marais wa Tume za Mafundisho Tanzu ya Kanisa kutoka
katika Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Ulaya, wanaokutana mjini Esztergom,
Hungaria kuanzia tarehe 13 hadi tarehe 15 Januari anakumbusha kwamba, Maaskofu kimsingi
ni walimu wa imani na kwamba, wanafanya mkutano wao nchini Hungaria, nchi ambayo ina
utajiri mkubwa wa imani, maisha na utume wa Kanisa.
Kardinali Muller anasema
msingi na maana ya huduma ya mafundisho tanzu ndani ya Kanisa inajikita katika Yesu
Kristo, Mkombozi wa Ulimwenguni, ambaye anawaalika wafuasi wake kuwa ni mashuhuda
wa ukweli katika imani iliyofunuliwa kwao kwa njia ya Fumbo la Umwilisho. Kutokana
na ukweli huu, taalimungu inaishi na kumwilishwa na imani, changamoto kwa wanataalimungu
kushirikiana kwa karibu zaidi na viongozi wa Kanisa, kwa ajili ya ustawi wa Kanisa
na maendeleo ya Familia ya Mungu: kiroho na kimwili.
Utume wa mamlaka ya ufundishaji
katika Kanisa umefungamana kwa hali halisi ya agano ambalo Mwenyezi Mungu amelianzisha
pamoja na Taifa lake. Kazi ya kichungaji ya mamlaka ya ufundishaji katika Kanisa ipo
pia kwa ajili ya kukesha ili Taifa la Mungu lidumu katika ukweli unaowafanya huru.
Ili kutekeleza utume huu, Kristo amewapa wachungaji karama ya kutokosea katika mambo
ya imani na maadili. Utekelezaji wa karama hii waweza kuwa wa namna nyingi.
Khalifa
wa Mtakatifu Petro, kichwa cha urika wa Maaskofu anayodhamana nyeti ya kuwaimarisha
ndugu zake katika imani na maadili mintarafu Neno la Mungu na utii kwa kutambua kwamba,
Khalifa wa Mtakatifu Petro ni Mtumishi wa Watumishi wa Mungu. Baraza la Kipapa la
Mafundisho Tanzu ya Kanisa lipo kwa ajili ya kumsaidia Baba Mtakatifu kutekeleza dhamana
na utume wake wa kufundisha, kuongoza na kuwatakatifuza watu wa Mungu; kwa kulinda
na kudumisha umoja wa Kanisa sanjari ya kusaidia mchakato wa kukuza na kuimarisha
imani katika ukweli.
Maaskofu wanapaswa kulinda na kutunza imani na maadili
ya Wakristo; kwa njia ya mafundisho yao huku wakiendelea kushikamana na Khalifa wa
Mtakatifu Petro. Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican kwa kutambua matatizo na
changamoto mbali mbali zinazowakabili Maaskofu mahalia, walikazia umuhimu wa kuanzishwa
kwa Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Kitaifa na Kikanda, kama sehemu muhimu sana ya kuweza
kubadilishana mang'amuzi na maoni katika ushirikiano mtakatifu, unaopania neema ya
Kanisa zima.
Kardinali Muller anasema ushirikiano kati ya Maaskofu katika urika
wao unapaswa kujionesha kwa Makanisa mahalia na kwa Kanisa la Kiulimwengu. Khalifa
wa Mtakatifu Petro ni chanzo, msingi dumifu na mwonekano wa umoja wa Maaskofu na Waamini
katika ujumla wao. Baba Mtakatifu huwakilisha Kanisa zima katika kifungo cha amani,
upendo na umoja.
Wataalam wa masuala ya kitaalimungu wanaweza kuwa ni wanachama
wa Tume ya Mafundisho Tanzu ya Kanisa, lakini ikumbukwe kwamba, hii ni dhamana kwanza
kabisa kwa Maaskofu. Tume hizi zinapaswa kuwasaidia Maaskofu katika kutekeleza dhamana
yao ya kufundisha, kuongoza na kuwatakatifuza Watu wa Mungu.
Kumbe, Tume hizi
pia zinapaswa kushirikiana kwa karibu zaidi na Baraza la Kipapa la Mafundisho Tanzu
ya Kanisa, ili kurahisisha mchakato wa kuwatangazia Watu Injili ya Furaha. Tume hizi
zinafanya kazi kwa idhini ya Maaskofu baada ya kupata ridhaa kutoka kwa Maaskofu.
Lengo ni kujenga na kuimarisha umoja na mshikamano wa Kanisa kwa kutambua
kwamba, wote ni sehemu ya Familia ya Mungu inayowajibika katika utofauti wake. Viongozi
wa Kanisa wajifunze kujiachilia mikononi mwa Yesu Kristo, Mwalimu mwaminifu anayepyaisha
imani na kuipatia utimilifu wake, kwa ajili ya mafao ya Watu wa Mungu.
Na Padre
Richard A. Mjigwa, C.PP.S Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.