2015-01-12 09:14:46

Mshikamano wa kimataifa dhidi ya vitendo vya kigaidi!


Wachunguzi wa mambo ya kisiasa wanasema, zaidi ya viongozi wakuu wa Serikali arobaini wameshiriki katika maandamano ya amani mjini Paris, Ufaransa, siku ya Jumapili jioni, tarehe 11 Januari 2015 ili kupinga vitendo vya kigaidi vinavyoendelea kuhatarisha amani, usalama na ustawi wa watu wengi pamoja na kuendelea kukazia uhuru wa kujieleza.

Rais Francois Hollande wa Ufaransa amewashukuru viongozi wakuu wa Serikali kwa kuonesha umoja na mshikamano katika mapambano dhidi ya vitendo vya kigaidi, vilivyosababisha watu 17 kupoteza maisha yao nchini Ufaransa, hivi karibuni.

Waandamanaji zaidi ya millioni mbili walionekana kwenye mitaa kadhaa nchini Ufaransa kupiga vitendo vya kigaidi. Maandamano kama haya yamefanyika pia katika sehemu mbali mbali za dunia. Viongozi wakuu wa nchi wameshiriki katika maandamano haya ili kuonesha umoja na mshikamano wa kimataifa dhidi ya vitendo vya kigaidi, kwa kulinda na kuendeleza uhuru wa mtu kujieleza kadiri ya Katiba ya nchi!

Wakati huo huo, vikosi vya ulinzi na usalama kutoka Ufaransa vinaendelea kumsaka kwa udi na uvumba msichana Hayat Boumedienne anayesadikiwa kuhusika kwa karibu zaidi na vitendo vya kigaidi mjini Paris, Ufaransa.







All the contents on this site are copyrighted ©.