2015-01-12 08:21:45

Lengo ni Uinjilishaji kwa cheche za majadiliano ya kidini!


Kardinali mteule Francis Xavier Kriengsak Kovithavanij, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Bangkok, Thailand anasema, Baba Mtakatifu Francisko anafanya hija yake ya kitume akiwa na Injili pamoja na cheche za majadiliano ya kidini, ili kulinda na kudumisha utu na heshima ya binadamu, upendo na mshikamano kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wengi.

Kanisa la kiulimwengu linaendelea kuonesha matumaini makubwa kwa Bara la Asia ambalo lina matatizo, changamoto na fursa mbali mbali zinazohitaji mchakato wa majadiliano ya kidini na kitamaduni, ili kweli imani ya Kikristo iweze kuota mizizi katika maisha na vipaumbele vya waamini na watu wote wenye mapenzi mema. Mtakatifu Yohane Paulo II aliwahi kusema kwamba, Uinjilishaji Barani Asia ni kati ya changamoto kubwa kwa Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo, licha ya ukweli kwamba, Wakristo ni kundi dogo sana wakilinganishwa na waamini wa dini kuu zilizoko Barani Asia.

Uinjilishaji Barani Asia unajikita katika mchakato wa majadiliano ya kidini kama anavyokazia Baba Mtakatifu Francisko! Haya ni majadiliano yanayopaswa kujikita katika uhalisia wa maisha, kwa kutekeleza kwa kina na mapana changamoto zilizotolewa na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, yaani majadiliano yaguse uhalisia wa maisha ya watu. Baraza la Maaskofu Katoliki Thailand katika mkutano wake wa mwaka, utakaofanyika mwezi Aprili 2015 utajikita zaidi katika Uinjilishaji mpya sanjari na majadiliano ya kidini.

Katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia, jambo linalopaswa kupewa kipaumbele cha kwanza anasema Kardinali mteule Francis Kovithavanij ni majiundo makini, ya awali na endelevu kwa waamini, ili kamwe wasimezwe na malimwengu, tayari kujisadaka kwa ajili ya kuyatakatifuza malimwengu kwa njia ya ushuhuda wa imani tendaji katika uhalisia wa maisha.

Hija ya kitume ya Baba Mtakatifu Barani Asia ni chachu kubwa kwa maendeleo ya waamini na watu wote wenye mapenzi mema Barani Asia, kwani ni kiongozi anayependwa na kuthaminiwa na wengi kutokana na mfano na unyofu wa maisha yake; ni kiongozi anayebeba ndani mwake Injili ya Furaha ambayo anataka kuimegea Familia ya Mungu Barani Asia. Ni matumaini ya Kanisa nchini Thailand kwamba, iko siku, Khalifa wa Mtakatifu Petro, atawatembelea ili kuwaimarisha katika imani, matumaini na mapendo!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.