2015-01-10 14:31:57

Yatakayojiri Sri Lanka na Ufilippini!


Baba Mtakatifu Francisko anatarajiwa kufanya hija ya kichungaji Barani Asia kuanzia tarehe 12 hadi tarehe 19 Januari 2015 kwa kutembelea Sri Lanka na Ufilippini. RealAudioMP3

Baba Mtakatifu ataondoka mjini Roma Jumatatu tarehe 19 Januari 2015 majira ya saa jioni 12:50 kwa saa za Ulaya na kuwasili kwenye Uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Colombo nchini Sri Lanka, majira ya saa 3: 00 Asubuhi. Hapo Baba Mtakatifu atapokelewa na kukaribishwa na viongozi wa Serikali na Kanisa.

Saa 7:15 mchana, Baba Mtakatifu anatarajiwa kukutana na kuzungumza na Baraza la Maaskofu Katoliki Sri Lanka, katika Makao makuu ya Jimbo kuu la Colombo. Jioni majira ya saa 11:00, Baba Mtakatifu atamtembelea Rais wa Sri Lanka Ikulu na baadaye saa 12:15 atakutana na kuzungumza na viongozi wakuu wa dini.

Baba Mtakatifu ataianza siku ya Jumatano tarehe 14 Januari 2015 kwa kumtangaza Mwenyeheri Giuseppe Vas kuwa Mtakatifu, katika Ibada ya Misa takatifu itakayoanza saa 2:30 kwenye Bonde la “Green Colombo”. Baadaye, Baba Mtakatifu atasafiri kwa njia ya Elkopta hadi kwenye Madhabahu ya Bikira Maria wa Rozari Takatifu yaliko Madhu, ili kusali na kutafakari kidogo kuhusu matendo makuu ya Mungu.

Tarehe 15 Asubuhi kabla ya kuondoka nchini Sri Lanka, Baba Mtakatifu Francisko atatembelea Kikanisa kilichowekwa wakfu kwa heshima ya Bikira Maria wa Lanka, kilichoko mjini Bolawalama. Baada ya hapo ataelekea Uwanja wa ndege wa Colombo, tayari kuanza safari kuelekea Manila, Ufilippini, na kuwasili majira ya saa 9: 00 na jioni saa 11: 45 atakaribishwa rasmi kitaifa.

Ijumaa tarehe 16 Januari 2015, majira ya saa 3:15 asubuhi Baba Mtakatifu atatembelea Ikulu na kukaribishwa rasmi na Rais wa Ufilippini baadaye atazungumza na viongozi wa Serikali na Wanadiplomasia nchini Ufilippini. Baadaye saa 5: 15 asubuhi, Baba Mtakatifu ataelekea kwenye Kanisa kuu la Bikira Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili na hapo ataadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya Familia ya Mungu nchini Ufilippini na jioni atakutana na Familia katika Uwanja wa Mall, ulioko Jijini, Manila.

Jumamosi tarehe 17 Januari 2015, Baba Mtakatifu anatarajiwa kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu huko Tacloban, karibu na Kiwanja cha Ndege, Ibada itakayoanza saa 2: 15 na baadaye mchana, Baba Mtakatifu atapata chakula cha mchana na baadhi ya wahanga wa tufani ya Yolanda, tukio litakalofanyika kwenye Makao makuu ya Jimbo Katoliki Palo. Jioni, atabariki na kuzindua Kituo cha Maskini cha Papa Francisko na baadaye atazungumza na Wakleri, Watawa, Waseminari na Familia za wahanga wa tufani ya Yolanda, baadaye jioni atarejea kwa ndege Manila.

Jumapili tarehe 18 Januari, 2015 asubuhi, Baba Mtakatifu atakutana na kuzungumza na viongozi wa dini nchini Ufilippini; baadaye atakutana na vijana kutoka Ufilippini na jioni atadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye Uwanja wa Riz.

Jumatatu tarehe 19 Januari, 2015 Baba Mtakatifu atakuwa anahitimisha hija yake ya kichungaji Barani Asia na ataagwa na baadaye kuanza safari ndefu ya kurejea tena mjini Vatican anakotarajiwa kuwasili majira ya saa 11: 45 jioni, kwenye Uwanja wa ndege wa Ciampino. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican itakuwa nawe bega kwa bega kukujuza yale yatakayokuwa yanajiri katika hija hii ya kichungaji, ukiwa na haraka zako chungulia kwenye mtandao wetu.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.