2015-01-10 15:01:50

Ukristo Mashariki ya Kati!


Kardinali Leonardo Sandri, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya Makanisa ya Mashariki anasema, historia ya Mashariki ya Kati, itakuwa na walakini mkubwa, ikiwa kama Ukristo utafutika huko kwa sababu ya madhulumu, chuki, uhasama na vita vinavyoendelea huko Syria na Iraq. Ukristo ni sehemu ya utajiri na vinasaba vya historia na maisha ya watu wa Mashariki ya Kati. RealAudioMP3

Licha ya magumu na machungu yanayoendelea kujitokeza huko Mashariki ya Kati, waamini na watu wote wenye mapenzi mema wanahamasishwa kuendelea kusali kwa ajili ya kuombea amani, kwani Yesu Kristo ndiye chemchemi ya tumaini katika maisha yao yote! Baba Mtakatifu ameendelea kuwatia moyo wa imani na matumaini Wakristo wanaoishi huko Mashariki ya Kati kwa kuwakumbuka daima katika sala na sadaka yake, pia kama alivyofanya hivi karibuni alipowaandikia barua Wakristo wa Mashariki ya Kati, tarehe 21 Desemba 2014.

Kanisa linatekeleza dhamana na wajibu wake, lakini pia, Jumuiya ya Kimataifa inapaswa kujifunga kibwebwe zaidi, ili kweli haki, amani na umoja viweze kupatikana tena huko Mashariki ya Kati, kwani kuna umati mkubwa sana wa watu wanateseka kutokana na vita, dhuluma na nyanyaso za kidini.

Hatima ya wakimbizi na wahamiaji ni kati ya changamoto kubwa zinazofanyiwa kazi na Kanisa huko Mashariki ya Kati, kwa kuitaka Jumuiya ya Kimataifa kuhakikisha kwamba, haki ya watu kuhama kutoka sehemu moja kwenda sehemu nyingine ili kusalimisha maisha yao, inaheshimiwa. Pale inapowezekana, wananchi wapewe nafasi ya kurudi tena katika nchi zao za asili ili kuendelea na maisha kama kawaida.

Baraza la Kipapa kwa ajili ya Makanisa ya Mashariki anasema Kardinali Sandri, linaendelea kutoa msaada wa hali na mali kwa Wakleri, ili kuweza kuwahudumia watu wanaohitaji msaada wa dharura, pamoja na kuendelea kuhimiza umuhimu wa kulinda na kudumisha uhuru wa kidini, kama anavyokazia Baba Mtakatifu Francisko anayeendelea kuwatia moyo kwa njia ya unyenyekevu, ubaba na moyo wa udugu; jambo ambalo linawapa faraja watu wengi zaidi katika shida na mahangaiko yao.

Vatican kwa kutumia njia ya kidiplomasia katika vikao mbali mbali ya kimataifa, limependa kuchangia kwa moyo mkuu upatikanaji wa suluhu ya kudumu huko Mashariki ya Kati, kwa kuitaka Jumuiya ya Kimataifa kushiriki kikamilifu, kwa kutambua mateso na mahangaiko ya watu huko Mashariki ya Kati. Matunda ya mchango huu yanaanza kuonekana kwa baadhi ya nchi kuonesha mshikamano wake wa dhati na watu wanaoteseka huko Mashariki ya kati pamoja na kuendelea kutoa hifadhi kwa wahamiaji na wakimbizi kutoka Syria. Lakini anasema Kardinali Sandri, watu wanataka kuishi kwa amani na utulivu katika nchi zao!

Baba Mtakatifu Francisko amekuwa akilaani vita, nyanyaso na madhulumu dhidi ya Wakristo huko Mashariki ya Kati na upande wa pili wa shilingi anakazia umuhimu wa majadiliano ya kidini katika ukweli, uwazi na mafao ya wengi; utu na heshima ya binadamu; mambo msingi yanayopaswa kusaidia mchakato wa ujenzi wa umoja, udugu na mshikamano wa dhati.

Vijana wanapaswa kufundwa ili kuheshimu zawadi ya maisha na utu wa binadamu. Ni wajibu wa viongozi wa dini kukemea na kulaani vikali mauaji ya watu wasiokuwa na hatia yanayofanywa kwa misingi ya misimamo mikali ya kiimani, ili kweli uhuru wa kuabudu, uweze kuheshimiwa na wengi. Ni jambo ambalo haliwezi kukubalika kuona kwamba, kuna watu wanaotumia dini kwa ajili ya mafao binafsi. Misimamo mikali ya kidini na vitendo vya kigaidi ni mambo yanayotishia amani, usalama na mfungamano wa kimataifa.

Kardinali Leonardo Sandri anakiri kwamba, diplomasia ya Vatican inafanya kazi zake kwa taratibu bila ya kukata tamaa, kama ilivyokuwa kwa Cuba na Marekani katika kipindi cha mika 53, wakipimana nguvu, lakini hatimaye, Serikali hizi mbili zimeanzisha mchakato wa ushirikiano wa kidiplomasia. Kanisa Katoliki huko Mashariki ya Kati linapenda kuendeleza mchakato wa majadiliano ya kidini na kiekumene, ili kulinda na kudumisha misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa kitaifa.

Kardinali Sandri anasema, Mwaka wa Watawa Duniani kama ulivyotangazwa na Baba Mtakatifu Francisko, ni fursa makini kwa Baraza lake kuendelea kuwafunda watawa wa Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume, ili kujisadaka zaidi kwa watu wanaoteseka huko Mashariki ya Kati, huku wakiwatangazia Injili ya Furaha, Upendo na Matumaini yanayobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa lake. Watawa watakuwa na nafasi ya kufanya mafungo, semina na makongamano kama sehemu ya maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani.

Watawa watambue kwamba, wao ni sehemu ya Injili iliyo wazi, inayosomwa na wengi kwa njia ya ushuhuda wa maisha na huduma kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii. Mwaka 2015 ni kilele cha Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 25 tangu kuchapishwa kwa Sheria za Makanisa ya Mashariki, kazi kubwa iliyofanywa na Mtakatifu Yohane Paulo II katika maisha na utume wake, kama sehemu ya mchakato unaopania kujenga na kuimarisha umoja wa Kanisa.
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.