2015-01-10 09:12:27

Shule Katoliki ni moto wa kuotea mbali!


Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani kuanzia tarehe 25 hadi tarehe 31 Januari 2015 litaadhimisha Juma la shule Katoliki Marekani, linaloongozwa na kauli mbiu "Shule Katoliki: Jumuiya ya imani, maarifa na huduma".

Askofu George Joseph Lucas, Mwenyekiti wa Tume ya Elimu Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani anasema, elimu ni sehemu muhimu sana ya maisha na utume wa Kanisa katika mchakato wa Uinjilishaji, unaolihamasisha Kanisa kujikita katika kuwafunda watu tunu msingi za maisha ya kiroho, kiutu na kimaadili, ili waweze kuwa kweli ni mashuhuda wa Kristo na Kanisa lake!

Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani linabainisha kwamba, shule za Kikatoliki ni mahali muafaka pa majiundo endelevu ya kiimani katika maisha ya waamini na watu wote wenye mapenzi mema. Hapa ni chimbuko la miito mitakatifu ya maisha ya ndoa, upadre na utawa, kwa hakika ni sehemu muhimu sana ya maisha na utume wa Kanisa, unaowashirikisha watu mbali mbali katika utekelezaji wake.

Takwimu zinaonesha kwamba, asilimia 99% ya wanafunzi wanaopata masomo yao kutoka katika shule za Kikatoliki wanahitimu masomo yao kwa ubora na viwango vya hali ya juu kabisa. Asilimia 87% ya wanafunzi wanaohitimu masomo yao katika sekondari zinazomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa Katoliki wanaendelea na masomo yao katika taasisi za elimu ya juu na vyuo vikuu ndani na nje ya Marekani.

Kanisa Katoliki nchini Marekani lina jumla ya shule 6, 600 zinazowahudumia wanafunzi millioni 2.1 kwenye majiji, miji na vijiji nchini Marekani. Wanafunzi wanapewa elimu makini itakayowasaidia kupambana na changamoto za maisha pamoja na kuwajengea ujuzi na maarifa na ufanisi kazini. Wachunguzi wa masuala ya elimu nchini Marekani wanasema, kwa hakika shule za Kanisa Katoliki zinatoa elimu makini kwa wanafunzi na wazazi wengi wanapenda kuwapeleka watoto wao huko, ili waweze kufundwa si tu kiakili, bali kiutu na kimaadili pia!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.