Askofu msaidizi Titus Mdoe wa Jimbo kuu la Dar es Salaam, Jumamosi, tarehe 10 Januari
2015 anatarajiwa kutoa Daraja la Ushemasi kwa Watawa wanne wa Shirika la Wamissionari
wa Damu Azizi ya Yesu, C.PP.S., Ibada itakayoadhimishwa kwenye Parokia ya Mtakatifu
Nicholaus, Kunduchi, Mtongani, Jimbo kuu la Dar es Salaam.
Hawa ni Majandokasisi
waliohitimu masomo yao ya falsafa na taalimungu na tarehe 9 Januari 2015 wamepokelewa
rasmi kuwa ni Wamissionari wa Shirika la Damu Azizi ya Yesu, katika Ibada iliyoongozwa
na Mheshimiwa Padre Reginald Mrosso, C.PP.S. Mkuu wa Shirika la Wamissionari wa Damu
Azizi ya Yesu, Vikarieti ya Tanzania.
Yafuatayo ni mahubiri aliyoyatoa katika
Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kuwapokea Frt. Lauriano Januari Mushi, Innocent
Emmanuel Miku, John Eleuteri Mlay pamoja na Emmanuel Joseph Makusaro kuwa Wamissionari.
Ibada hii imefanyika kwenye Parokia ya Mtakatifu Nicholaus, Kunduchi, Mtongani, Jimbo
kuu la Dar es Salaam.
Katika barua yake kwa ajili ya Maadhimisho ya Mwaka wa
Watawa uliozinduliwa Jumapili ya kwanza ya Kipindi cha Majilio Nov. 2014 na unaotarajiwa
kufungwa rasmi tarehe 2 Feb. 2016, Siku kuu ya kutolewa Bwana Hekaluni sanjari na
Siku ya Watawa Duniani, Baba Mtakatifu Francisko anaanza na maneno haya; napenda kusema
neno moja kwenu na neno hilo ni furaha. Popote walipo watawa, ipo pia furaha. Wale
wote waliosikia sauti ya Bwana wanaalikwa kufurahi: wimbo wetu wa katikati leo unatualika
tufurahi kwa sababu sisi ni watu wa ufufuko na watu wake Mungu – Zab. 95: kwa sababu
dunia imeuona wokovu wa Mungu. Ninyi vijana wapendwa mko hapa kwa sababu mnaamini
katika huo ufufuko, katika huo uzima wa milele wa kimungu.
Leo tunamshukuru
Mungu kwa sababu ndugu zetu hawa wamefikia hatua hii kubwa katika maisha yao ya wito
na ya Kanisa kwa ujumla katika kumtumikia Mungu na watu wake. Tunasoma maneno haya
katika - Zab. 100:3 – jueni kwamba Bwana ndiye Mungu, ndiye aliyetuumba, nasi tu watu
wake, taifa lake na kondooo wa malisho yake. Ufahamu huu ni muhimu sana katika maisha
ya mwanadamu ye yote. Ni chanzo cha wito mbalimbali katika maisha ya kawaida na katika
kanisa. Ye yote yule anayetambua Mungu ni nani, atapata mwelekeo wa kimungu katika
maisha yake. Asiyetambua hilo, hupoteza mwelekeo wa kimungu katika maisha yake.
Mtume Paulo katika - 1 Tim. 6:15-16 – anaandika hivi – wakati wake mwenye heri
atalidokeza tokeo la yeye aliye peke yake mtawala, Mfalme wa wafalme, Bwana wa mabwana,
Yeye peke yake hawezi kufa. Amekaa katika mwanga usiosogeleka. Hakuna mwanadamu aliyemwona,
wala awezaye kumwona. Heshima na enzi ya milele ni yake. Amina. Tunaona kuwa ufalme
na utawala wa kweli ni wake.
Ufahamu huu unatupelekea kutambua kuwa tumeitwa
kumtumikia yeye tu na si kitu kingine cho chote kile – Mt. 4:10 – Yesu akamwambia,
nenda zako shetani, kwa maana imeandikwa– umwabudu Bwana Mungu wako, ukamtumikie yeye
peke yake. Na katika Kumb. 6:13 – ndiye Bwana Mungu wako utakayemwogopa, ndiye utakayemtumikia
na kuapa kwa jina lake.
Somo la kwanza toka Nabii Isaya – “Injili ya Ufalme
wa Mungu” - mwandishi anaandika neno hili wakati Waisraeli wamekuwa huru toka Babeli
- linaelezea habari ya ukombozi. Waisraeli wanatoka katika utumwa. Wanafurahi. Nanyi
pia tafakarini sana hali yenu – mjiweke huru kwa ajili ya Mungu. Yule aliyeufahamu
ukombozi wa Mungu, anajiweka huru kwa ajili yake. Nanyi kuweni huru siku zote kwa
ajili ya kumtumikia Mungu na mumtumikie kwa furaha siku zote za maisha yenu. Nabii
Isaya– anatambua kuwa thamani ya maisha iko katika uhuru wa kimungu. Huo ndio uhuru
wa kweli na wenye kuleta wokovu.
WHO IS A CONSECRATED PERSON?
He is
a person who has an experience of God and especially as an Absolute. One who deeply
aware of his encouter with God and having received a special gift which is divine
and trinitarian. This is more than reading or hearing about God (Cf. Mk 8:27-29 –
ungamo la Petro – baada ya Yesu kuwauliza – watu wasema mimi ni nani? ). And because
in encoutering God he knows himself, then the experience of his weakness, fragility
and suffering leads him to see God as an Absolute — God is all, man is nothing. Hence,
the first task of consecrated person is to reveal the primacy of God to the world.
All vocations reveal the mystery of Christ: the lay vocation reveals the face of Christ
facing towards the world, the priestly vocation reveals the face of Christ facing
towards the community and the consecrated vocation reveals the heart of Christ turned
towards the Father. The consecrated person lives for God and only for God. The first
value of our vows is to sing the primacy of God in our lives.
Waraka wa Kitume
Injili ya Furaha,“Evangelii Gaudium” uliochapishwa na Baba Mtakatifu Fransisko unatoa
kipaumbele cha kwanza kwa furaha ya Injili, kwa kuwaalika waamini kushirikisha furaha
yao inayopata chimbuko kutoka katika huruma na upendo wa Mungu kwa wanadamu. Katika
mwono huu, Kristo ni kiini cha Injili na kwamba, Kanisa linaalikwa kufanya mageuzi
makubwa kama sehemu ya Uinjilishaji.
Baba Mtakatifu Francisko anaendelea kusema
– furaha ya Injili inajaza mioyo na maisha ya wale wanaokutana na Kristo. Pamoja na
Yesu Kristo, furaha inazaliwa upya tena. Sura ya 4 – mwanzoni - ya waraka wa Pili
wa Mtume Paulo kwa Wakorintho – inazungumzia juu ya watumishi kwa ajili ya Kristo.
Mstari wa sita – kwani Mungu aliyesema, Mwanga ung’ae kutoka gizani, ndiye yeye anayeng’aa
mioyoni mwetu tupate kwa mwanga wake kuutambua utukufu wa Mungu uliopo usoni mwa Yesu
Kristo. 2 Kor. 4: 6…. Mnaalikwa muwe mwanga wake Kristo. Kwa maisha yenu na ushuhuda
wenu wa maisha, Kristo aendelee kuonekana duniani. Maisha haya mnayotaka kufuata yawe
changamoto kwa wale wote ili wanapowaona ninyi wazidi kumpenda na kumtumikia Mungu
Baba.
Katika barua kwa mwaka wa watawa – Baba Mtakatifu Francis anamtaja wazi
Mtakatifu Francisko wa Assisi kama mfano wa kuigwa, yeye aliyefanya Injili iwe njia
yake ya maisha, akafanya imani ikakua na akahuisha kanisa na jamii, akaifanya iwe
ya kindugu zaidi, lakini daima akiongozwa na Injili na ushuhuda wa maisha yake. Nanyi
yapokeeni na yatimizeni mapenzi ya Bwana kama mtakatifiu Francis. Na imani yenu ionekane
katika matendo yenu. Lengo lenu liwe tu ni kutangaza habari njema kwa kila kiumbe.
Neno la Mungu katika somo la Injili leo liwaongoze na kuwatafakarisha sana - Yesu
ndiye masiha aliyepakwa mafuta, ambaye kadiri ya maandiko ya manabii ‘ndiye aliyepelekwa
kuwatangazia maskini habari njema na kuutangaza mwaka wa Neema – Lk. 4, 18-19, pia
katika Isa. 61: 1-2 - ‘Roho wa Bwana yu juu yangu, kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri
maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, na vipofu
kupata kuona tena, kuwaacha huru waliosetwa, na kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa.
Baada ya kusoma, akafunga kile kitabu, akampa mtumishi, kisha akaketi, watu wote wakamkodolea
macho. Naye akaanza kuwaambia, andiko hili mlilolisikia limetimia leo’.
Nanyi
ingieni katika programu hii ya kimasiha ya Yesu Kristo. Yaani muwe watangazaji mahiri
wa ufalme wake na kuutangaza daima mwaka wa Bwana. Ujumbe huu bado u hai hata leo.
Msijihangaishe na lo lote lile lililo nje ya programu hii. Katika kumfuata Kristo
– Baba Mtakatifu katika barua yake kwa Maadhimisho ya Mwaka wa Watawa anaendelea kusema
– kuweni na mwanga na furaha, ng’aeni furaha. Isa. 66: 10-14 – shangilia pamoja na
Yerusalemu, pigeni vigelegele kwa ajili yake, enyi nyote mnaomlilia, furahini, furahini
pamoja naye ninyi nyote mlioomboleza kwa ajili yake Ili mpate kunyonya na kushibishwa
maziwa ya faraja yake, na kufurahishwa kwa maziwa yake matukufu.
Maana, Bwana
asema hivi; nitatiririsha amani na utulivu pande zote kama mto; nao utukufu wa mataifa
kama kijito kifurikacho. Nanyi mtapata kunyonya, mtabebwa kifuani, na kubembelezwa
juu ya magoti yake, mfano wa mwana anayefarijiwa na mama yake, ndivyo nami nitawafariji,
nanyi mtafarijiwa moyo katika Yerusalemu. Kwa kuona hayo, moyo wenu utafurahi, na
mifupa yenu itasitawi mfano wa majani mabichi na mkono wa Bwana utajulikana kwa watumishi
wake, nayo ghadhabu yake kwa maadui zake.
Wote watakaoshiriki karamu hii ya
Bwana na mwaliko huu mtakatifu watapata uzima wa milele. Ninyi mnataka kuingia katika
karamu hii. Furahini pamoja na Bwana na furaha hiyo izae matunda katika maisha yenu.
Naye Mtakatifu Gaspari anatupa changamoto nyingine katika maisha ya ufuasi.
Alipoanzisha Shirika la Wamisionari wa Damu Azizi ya Yesu alialika wafuasi wake wawe
na upendo mkuu akisema ‘upendo ni kifungo kwa wamisionari wake’. Wakifungwa na upendo,
Gaspari aliamini Wamisionari wake wataweza kueneza kwa maisha yao Tasaufi ya damu
azizi. Tena watakuwa tayari kutoa huduma ya Neno la Mungu. Akinukuu maneno toka waraka
wa Paulo kwa waefeso 1;6-8 – Atukuzwe Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo …katika
yeye ametuchagua kabla ya kuwekwa misingi ya ulimwengu kusudi tuwe watakatifu na bila
doa mbele yake katika upend.
Mtakatifu Gaspari aliamini kuwa upendo ukiwepo
kazi ya Mungu itaendelezwa. Nasi tumwaminio tutapata uzima wa milele. Katika maisha
yake alieneza sifa na utukufu wa neema hizi za Mungu, neema ambayo inatoka kwa mwanae
mpendwa Kristo Yesu. Kutoka kwake Kristo tunaona ukombozi wetu na tuna msamaha wa
dhambi. Nanyi muwe na upendo mkuu kwa Mungu Baba na Mwanae anayewajalia roho ya kutaka
kumtumikia yeye kwa ulimwengu wa leo wenye changamoto nyingi za maisha.
Ninyi
leo mnakuwa Wamisionari wanashirika. Mtakatifu Gaspari hakuona ibada kwa Damu azizi
ya Yesu kama ibada nyingine ya kawaida, bali aliona ni kama kiini kabisa cha dini.
Mtakatifu Gaspari mwenyewe anasema, ‘ni njia salama ya kufikia utakatifu binafsi na
chachu ya maisha mapya ya jumuia na nguvu imara ya kazi ya kitume.
Pengine
twaweza kujiuliza kama Kristo alishamwaga damu yake kwa ajili yetu sote, nafasi yangu
ni ipi leo katika kuutangaza upendo huu wa Kristo? Kwa nini nihangaike kufanya mengi
kama Kristo tayari ameshatukomboa? Waraka wa mtume Paulo kwa Wakolosai 1:24 unatupatia
jibu “ nayatimiliza katika mwili wangu yale yaliyopungua katika mateso kwa ajili ya
mwili wake yaani kanisa lake”
Nihitimishe homilia hii nikinukuu tena maneno
ya Baba Mtakatifu Francis katika barua yake kwa Mwaka wa Watawa, akisema – nataka
niseme neno moja kwenu, nalo ni furahini. Po pote walipo watawa na watu wa maisha
ya wakfu, waseminari, wanaume na wanawake, vijana, ipo furaha, ipo daima furaha. Ni
furaha ya upya, furaha ya kumfuata Kristo, furaha ambayo Roho Mtakatifu atupatia.
Siyo furaha ya ulimwengu. Somo la pili la leo linatoa mwelekeo – Ebr. 13:12-15, 20-21-
habari juu ya maisha mapya katika ufufuko.
Sisi tumepatanishwa na Mungu kwa
njia ya kifo cha mwanawe, tumeokolewa kwa ufufuko wake. Sisi ni viumbe vipya. Ni watu
wa ufufuko. Mnapoaanza maisha mapya katika shirika letu na ndani ya kanisa – jitahidini
nanyi kuwa wapya katika yote – ishini maisha ya ufufuko. Maneno ya Petro Mtume yawaongoze“tuishi
kama watakatifu kwa mfano wa Mungu aliyetuita katika imani”.