Zingatieni utawala wa sheria na haki, ili kukemea maovu!
Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Tanzania Bwana George Masaju amewakumbusha watumishi
wa umma katika sekta ya sheria kufanya kazi kwa ushirikiano, uzalendo, maadili, utii
wa sheria ili kulinda maslahi ya taifa. Bwana Masaju, ambaye ameteuliwa na kuapishwa
hivi karibuni na Rais Jakaya Kikwete kushika wadhifa huo, amefafanua kuwa watumishi
wa umma wanapozingatia uzalendo katika utendaji wao, wanapata nguvu ya kusimama na
kukemea maovu.
Bw. Masaju ameyasema hayo Jumatano, Januari 7, 2015 jijini
Dar es Salaam alipokuwa akizungumza na viongozi wa Wizara ya Katiba na Sheria alipokwenda
kubadilishana nao mawazo. “Sisi kama Wizara kwa ujumla wetu, tunapaswa kuwa mfano
wa uzalendo katika taifa hili ili tunaposimama mbele ya watu, tuwe na nguvu kwa kuwa
tupo safi,” amesema Mwanasheria Mkuu wa Serikali ambaye kabla ya uteuzi huo, alikuwa
Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
Akizungumza katika mkutano huo, Waziri
wa Katiba na Sheria Dkt. Asha-Rose Migiro alimpongeza Bw. Masaju kwa heshima aliyopewa
na Rais Jakaya Kikwete na kuahidi kuwa yeye na Wizara itaendelea kumpa ushirikiano
wa kutosha katika kutekeleza majukumu yake. “Tunakupongeza kwa heshima kubwa uliyopewa
na Mheshimiwa Rais na sisi kama wasimamizi wa sera, tutaendelea kutoa ushirikiano
kwako kama tulivyofanya kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali aliyetangulia,” alisema Waziri
Migiro.
Aidha, Waziri Migiro aliahidi kuongeza ushirikiano katika kuimarisha
kada ya Mawakili wa Serikali pamoja na watumishi wengine ili kuongeza ufanisi katika
utoaji haki. Bw. Masaju aliteuliwa kuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali tarehe 2 Januari
mwaka huu na kuapishwa tarehe 5 Januari. Kabla ya uteuzi huo, alikuwa Naibu Mwanasheria
Mkuu wa Serikali. Aidha, Bw. Masaju amewahi kuwa Mshauri wa Sheria wa Rais wa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania.