2015-01-08 11:29:42

Mshikamano wa upendo na udugu kwa Wakristo Mashariki ya Kati!


Ujumbe wa Maaskofu Katoliki kutoka Ulaya, Marekani na Afrika ya Kusini, wanaoratibu shughuli za misaada kwa Nchi Takatifu, (HLC2015) kuanzia tarehe 10 hadi tarehe 15 Januari 2015 wanatembelea Nchi Takatifu kama kielelezo cha mshikamano umoja, upendo na udugu kwa ajili ya Wakristo huko Mashariki ya Kati, hasa kipindi hiki ambako Ukanda huu umegeuka kuwa ni uwanja wa fujo na kinzani za kisiasa na kijamii!

Askofu Duarte da Cunha, Katibu mkuu wa Shirikisho la Baraza la Maaskofu Katoliki Ulaya anasema, pengine watu wamekuwa na mazoea ya kuona mashambulizi, vita na mateso ya watu yalisimuliwa kwenye vyombo vya habari na kusahau kwamba, mambo haya yamechangia kwa kiasi kikubwa kwa Mashariki ya Kati, kuwekwa pembezoni mwa mikakati ya Jumuiya ya Kimataifa. Maaskofu wanapenda kuwaonesha Wakristo na watu wote wenye mapenzi mema ujumbe wa amani na matumaini yanayojikita katika ushuhuda wa maisha, kwa kuwa karibu zaidi na wale wote wanaoteseka pamoja na maskini pamoja na kuwatia shime wafanyakazi wa Mashirika mbali mbali ya misaada yanayosimamiwa na kuongozwa na Kanisa Katoliki.

Wakiwa Nchi Takatifu wajumbe hawa watatembelea na kukutana na viongozi pamoja na Wakristo wanaoishi kwenye Ukanda wa Ghaza, ili kuangalia huduma zinazotolewa katika shule na vituo vya afya kwa ajili ya wananchi. Watatembelea pia mji wa Hebron na Sderot, ambayo imeharibiwa hivi karibuni kutokana na kupigwa kwa makombora. Watatembelea pia mji wa Cremisan, ambao kuna ukuta unaotenganisha familia za Kikristo zinazoishi katika miji ya Beit Sahour na Beit Jala.
Ujumbe huu utakapokuwa mjini Bethlehemu utatembelea na kujionea shughuli mbali mbali zinazofanywa kwa ajili ya kuwasaidia watoto wenye ulemavu na wanaoishi kwenye mazingira hatarishi; wazee wanaotunzwa na kuhudumiwa na Kanisa. Watatembelea na kukagua huduma zinazotolewa kwenye shule za visiwi na vipofu; nyumba ya wanawake wajane. Wajumbe wanatarajiwa kukutana na kuzungumza na Maaskofu mahalia.

Taarifa zinaonesha kwamba, Baraza kuu la Shirikisho la Makanisa Katoliki Ulaya, linatarajiwa kufanya mkutano wake wa Mwaka kuanzia tarehe 11 hadi tarehe 16 Septemba 2015. Huu ni mkutano unaowashirikisha Maaskofu Katoliki kutoka katika Nchi 43 za Bara la Ulaya.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.