2015-01-08 07:57:59

Makovu ya ubinadamu!


Baba Mtakatifu Francisko alipokutana na kuzungumza na wafanyakazi mbali mbali wa Vatican, kama sehemu ya mchakato wa kutakiana kheri na baraka kwa Kipindi cha Noeli na Mwaka Mpya 2015 amewataka wafanyakazi hawa kutumia neema na baraka ya kipindi hiki kwa ajili ya kuganga na kutibu madonda yaliyojitokeza katika hija ya maisha yao pamoja na kujitakasa, ili kuanza mchakato wa maisha mapya. RealAudioMP3

Baba Mtakatifu katika hotuba yake kwa wafanyakazi wa Vatican amekazia zaidi: umuhimu wa maisha ya kiroho, kifamilia, upendo kwa Mungu na jirani, kazi pamoja na kutibu mapungufu ya mtu binafsi.

Hii ni nafasi murua kabisa Familia ya Mungu inapoendelea kuwasindikiza Mababa wa Sinodi kwa sala, tafakari na mchango wao kwa ajili ya Sinodi ya Maaskofu kuhusu Familia, itakayoadhimishwa hapa mjini Vatican kuanzia tarehe 4 hadi tarehe 25 Oktoba, 2015 kwa kuongozwa na kauli mbiu “wito na utume wa Familia katika Kanisa na Ulimwengu mamboleo”, Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican inapenda kukukumbusha tena ujumbe wa Baba Mtakatifu, ili uweze kuumwilisha katika maisha yako ya kila siku!

Kwanza kabisa Baba Mtakatifu anawataka wafanyakazi kuhakikisha kwamba, wanashughulikia kwa ud ina uvumba maisha yao ya kiroho ambayo yanapaswa kujikita katika: Sala, Sakramenti pamoja na tafakari ya Neno la Mungu inayomwilishwa katika matendo ya huruma, Baba Mtakatifu anasema mahusiano ya karibu na Mwenyezi Mungu ni uti wa mgongo wa maisha na utambulisho wa kila mwamini. Ikiwa kama mwamini atatindikiwa na mambo haya, maisha yake yako hatarini, anaweza kunyauka na hatimaye, kukosa dira na mwelekeo wa maisha.

Baba Mtakatifu anasema, kuna haja kwa waamini na watu wenye mapenzi mema kujikita zaidi na zaidi katika maboresho ya tunu msingi za maisha ya ndoa na familia, kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa malezi na makuzi ya watoto wao. Wazazi wahakikishe kwamba, wanatenga muda wa kukaa pamoja na watoto wao, ili kuwajengea matumaini ya kesho iliyo bora! Baba Mtakatifu anasema, haitoshi kuwapatia watoto fedha kibao na simu za viganjani wakadhani kwamba, hapo wamemaliza wajibu wao!

Baba Mtakatifu anawataka waamini kuhakikisha kwamba, wanaboresha mahusiano yao na jirani zao, ili kweli familia ziweze kuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi, kushuhudia na kutangaza Injili ya Familia, kwa njia ya imani tendaji. Maisha ya wanafamilia yajikite katika imani, wema, mapendo na matumaini; kwa kuonesha ukarimu na kusaidiana kwa hali na mali.

Pale ambapo familia zimeonesha mtafaruku, waamini wawe na ujasiri wa kutibu madonda haya kwa njia ya mafuta ya huruma, upendo na mshamaha kwa kutambua kwamba, kukosa na kukoseheana ni sehemu ya ubinadamu, kusamehe na kusahau ni kuanza mchakato wa maisha ya uzima wa milele. Waamini wajitahidi kuponya madonda waliyowatendea wengine, kwa njia ya toba na wongofu wa ndani.

Baba Mtakatifu anasema, kazi na ajira ni kielelezo cha ut una utumilifu wa maisha ya mwanadamu na kwamba, kazi ndilo jina lako haswaaa!Baba Mtakatifu anawahimiza wanafamilia wanaofanya kazi, kutekeleza wajibu huu nyeti kwa unyenyekevu mkubwa, weledi, juhudi, bidii na maarifa, daima wakionesha moyo wa shukurani kwa Mwenyezi Mungu anayewakirimia nafasi hii.

Ni changamoto kwa wafanyakazi kujiepusha na majungu, utovu wa nidhamu, uchu wa mali na madaraka; mambo ambayo wakati mwingine ni sababu ya kutoweka kwa amani na utulivu kati ya jamii ya watu, kiasi cha kuwatumbukiza watu katika majanga na maafa makubwa. Watu wajiepushe kulipiza kisasi kwani hali hii ni kwenda kinyume kabisa cha haki ya Mungu, kwani Mwenyezi Mungu ndiye mwenye kipimo na hakimu mwenye haki. Watu waondokane na uvivu, jamvi la shetani; kiburi na majivuno. Wafanyakazi waoneshe ukomavu kazini kwa kukuza na kudumisha maadili badala ya kutaka kuwapaka wenzao kwa matope, mambo ambayo ni hatari kwa ustawi na maendeleo ya jamii.

Jamii ijifunze kuwahudumia maskini, wanyonge na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii; hawa ni watoto ambao bado hawajazaliwa, wazee, wagonjwa, wageni, wakimbizi na wahamiaji. Kipindi cha Noeli, kiwe ni kielelezo cha imani, upendo na mshikamano wa dhati; kipindi cha kushirikishana furaha inayobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa lake; kwa kutambua kwamba, Mwana wa Mungu yuko pamoja na watu wake. Yesu Kristo, Mwana wa Mungu aliyejifanya maskini kwa ajili ya maskini, anaendelea kuwashangaza wanadamu kwa kujifunua kwa watoto wadogo na maskini na kwamba, Kristo Yesu, amekuja ili kuhudumia na kujisadaka kwa ajili ya wokovu wa wengi.

Noeli ni kipindi cha Amani, zawadi kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu; inayopaswa kulindwa, kudumishwa na kuendelezwa. Baba Mtakatifu anathubutu kuomba msamaha kutokana na mapungufu yake ya kibinadamu, changamoto na mwaliko kwa waamini kuombana msamaha, ili kuanza hija ya maisha mapya katika haki, wema na utakatifu wa maisha!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican








All the contents on this site are copyrighted ©.