2015-01-08 11:01:23

Iweni ni vyombo vya Injili ya Furaha!


Katika maadhimisho ya Siku kuu ya Tokeo la Bwana, tarehe 6 Januari 2015, Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican, aliwasilisha salam na matashi mema kutoka kwa Baba Mtakatifu Francisko kwa ajili ya ufunguzi wa jengo linalotumika kwa ajili ya majiundo ya majandokasisi kutoka Marekani wanaosoma katika taasisi na vyuo mbali mbali vya kipapa mjini Roma.

Kuna uhusiano mkubwa kati ya majiundo na Khalifa wa Mtakatifu Petro, kwani wote wanaofunda na kufundwa chuoni hapo wanahamasishwa kuwa ni mashahidi wa Fumbo la Pasaka, sanjari na kujitahidi kuwa ni wachungaji wema na watakatifu. Ni mwaliko wa kuendelea kusali kwa ajili ya Baba Mtakatifu pamoja na wasaidizi wake wa karibu, ili aweze kuliongoza Kanisa la Kristo, daima akiongozwa na mwanga angavu ambao ni Kristo mwenyewe!

Kama ilivyokuwa kwa Mamajusi, walipofika wakagundua kwamba, kwa hakika Yesu ni mwanga wa wema, ukweli na uzuri, jambo ambalo waliwashirikisha wengine mara baada ya kufanya hija yao mjini Bethlehemu na hivyo kuvuruga njama za Mfalme Herode za kutaka kumwangamiza Mtoto Yesu wakati ule. Waamini waendelee kumtolea Yesu zawadi ya: dhahabu, uvumba na manemane, bila kusahau shida na magumu wanayokumbana nayo katika maisha, kwani Yesu kwa hakika ni mwanga angavu.

Kardinali Pietro Parolin anawataka majandokasisi kuhakikisha kwamba, wanajitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake, kwa kutambua kwamba, Kristo ndiye Mkombozi wa ulimwengu. Leo hii kuna watu wengi ambao wanaendelea kulia na kuomboleza kutokana na vita, dhuluma, nyanyaso na kinzani zinazowaelemea walimwengu. Bado kuna mamillioni ya watu wanakabiliwa na umaskini wa hali na kipato; njaa na maradhi.

Haya ni mambo ambayo yanahitaji kushughulikiwa kwa njia ya sala na mshikamano wa udugu na upendo kati ya watu; kwa kuendelea kutoa nafasi kwa Yesu Kristo Mkombozi wa dunia, ili aweze kuwaletea mageuzi katika maisha yao, mintarafu mwanga wa haki, amani na mshikamano.

Kardinali Parolin anawapongeza vijana ambao kwa hiyari yao wenyewe wametambua kwamba, wanaitwa na Mwenyezi Mungu ili kushiriki katika Ukuhani wa Kristo kwa njia ya Daraja Takatifu la Upadre. Seminari ni mahali ambapo Mama Kanisa anapatumia kwa ajili ya majiundo makini ya mihimili ya Uinjilishaji: kiroho, kimwili, kiutu na kimaadili.

Majandokasisi wanapohitimisha majiundo yao makini, wanapaswa kuwa kweli ni vyombo vya ujenzi wa Ufalme wa Mungu, ili kuwatangazia Watu wa Mataifa Injili ya Furaha. Huu ndio utume unaopaswa kufanyiwa kazi na wale wote ambao wamepewa dhamana ya Kuinjilisha. Mwishoni, Kardinali ameyaweka majengo mapya chini ya ulinzi na usimamizi wa Bikira Maria Mama wa Mungu, ili aweze kuwasimamia na kuwaongoza kwa kufuata mfano wa Mwanaye Mpendwa Yesu Kristo.

Waamini wote wanapaswa kushiriki kikamilifu katika kazi ya ukombozi, kwa kuonesha uaminifu, mapendo, imani na matumaini, kama ilivyokuwa kwa Miamba ya Injili, iliyomwaga damu yao kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake, ili kweli Kristo nyota angavu aendelee kung'ara katika maisha ya watu na vipaumbele vyao! Tukio hili limehudhuriwa na viongozi kadhaa kutoka ndani na nje ya Vatican, wafadhili na waamini.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.