2015-01-06 08:18:13

Watoto wanavyoguswa na shida na mateso ya watoto wenzao duniani!


Shirika la Kipapa la Utoto Mtakatifu nchini Ujerumani, limeendelea kuonesha hali ya kujali na kuguswa na mahangaiko ya watoto wenzao sehemu mbali mbali za dunia, kiasi kwamba, kipindi cha Noeli, wanakitumia kwa ajili ya kukusanya fedha kwa ajili ya kuwasaidia watoto wanaoishi katika mazingira magumu na hatarishi sehemu mbali mbali za dunia.

Watoto hawa wanatekeleza utume huu kwa zaidi ya miaka hamsini na saba. Kampeni ya Mwaka 2015 inaongozwa na kauli mbiu "Kupeleka na kuwa baraka. Lishe bora kwa watoto nchini Ufilippini na duniani kote". Watoto wametembelea nyumba mbali mbali nchini Ujerumani, ili kuomba mchango kwa ajili ya kuwasaidia watoto wenzao sehemu mbali mbali za dunia kama kielelezo cha upendo na mshikamano wa kidugu.

Watoto hawa wamekuwa wakichangia kwa kiasi kikubwa katika mikakati ya mshikamano wa upendo, kwa ajili ya watoto wanaoishi katika mazingira magumu na hatarishi sehemu mbali mbali za dunia. Takwimu zinaonesha kwamba, kuna zaidi ya watu millioni 842 wanasumbuliwa kwa baa la njaa na utapiamlo duniani. Kuna watoto millioni 2.6 chini ya umri wa miaka mitano wanaofariki dunia kutokana na utapiamlo wa kutisha.

Shirika la Kipapa la Utoto Mtakatifu nchini Ujerumani linajihusisha pia katika kuwasaidia watoto yatima, waliofiwa na wazazi wao kutokana na ugonjwa wa Ukiwmi; watoto wanaoishi mazingira hatarishi kiasi kwamba hawana tena fursa ya kuendelea na masomo; hawana fursa ya kupata maji safi na salama; wote hawa wanaonjeshwa upendo kutoka katika mfuko wa fedha zinazochangishwa na watoto hawa kutoka Ujerumani. Majimbo mbali mbali Barani Afrika pia yanaendelea kuwekeza katika malezi na majiundo ya utume wa watoto, ili kuwajengea uwezo wa kuwa ni Wamissionari kwa ajili ya watoto wenzao, ambao hawakubahatika kama wao!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.