Sheria dhidi ya ugaidi, ilikuwa ni kinyume cha Katiba ya Nchi!
Mahakama kuu ya Kenya imetamka kwamba, sheria mpya iliyokuwa imetungwa Bungeni hivi
karibuni kuhusiana na mchakato wa kulinda na kudumisha ulinzi na usalama nchini Kenya
ni kinyume cha Katiba ya Nchi. Mahakama kuu imetoa uamuzi huu baada ya muungano wa
vyama vya upinzani nchini Kenya kukata rufaa Mahakama kuu, ili kupinga sheria iliyokuwa
imepitishwa na Bunge, mwezi Desemba 2014.
Mahakama inasema, sheria hii mpya
ilikuwa inakiuka haki msingi za binadamu kwa kisingizio cha kutaka kupambana na vitendo
vya kigaidi ambavyo kwa Mwaka 2014, vimeitikisa Kenya na hivyo kupelekea watu wengi
kupoteza maisha pamoja na mali zao kutokana na mashambulizi ya kigaidi. Mahakama pia
imefuta idadi ya wakimbizi wa kisiasa waliokuwa wanaomba kibali cha uraia wa Kenya.
Muswada wa sheria ulipitishwa mara moja na Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya sanjari
na kufuta Mashirika kadhaa Yasiyokuwa ya Kiserikali kwa kutuhumiwa kushirikiana na
magaidi pamoja na kutolipa kodi kwa Serikali.Wachunguzi wa mambo wanasema, muswada
wa sheria iliyokuwa imepitishwa, ulikuwa ni hatari kwa ukuaji wa demokrasia na uhuru
wa mtu kujieleza kadiri ya Katiba ya nchi.