2015-01-05 08:11:43

Rushwa, ufisadi na mmong'onyoko wa maadili ni majanga ya kitaifa!


Baraza la Maaskofu Katoliki Ghana katika ujumbe wake kwa ajili ya Maadhimisho ya Noeli na Mwaka Mpya 2015, linasema, rushwa na ufisadi wa mali ya umma; biashara na matumizi haramu ya dawa za kulevya sanjari na kuporomoka kwa kanuni na tunu msingi za kimaadili na utu wema; ni mambo ambayo yanatishia amani, usalama, umoja na mshikamano wa kitaifa nchini Ghana.

Haya ni mambo ambayo yanawagusa wananchi wengi na kwamba, si rahisi mtu kujitutumua kwamba, kamwe hausiki na “majanga haya ya kitaifa”. Maaskofu wanakiri kwamba, hata baadhi ya viongozi wa Kanisa wametikiswa na majanga haya katika maisha na utume wao. Kwa hakika wanasema Maaskofu, bila “majanga haya ya kitaifa” Ghana ingekuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi.

Baraza la Maaskofu Katoliki Ghana linasema kwamba, kuna haja kwa wananchi wote wa Ghana katika ujumla wao kusimama kidete kupinga kwa nguvu zote tabia ya kumong’onyoka kwa tunu msingi za kimaadili na utu wema; kwa kusimama kidete ili kushuhudia tunu msingi za maisha ya kiroho na kiutu kila mwamini kadiri ya imani yake.

Leo hii nchini Ghana, ulevi wa kupindukia, biashara ya ngono, utoaji wa mimba, utumiaji haramu wa dawa za kulevya, rushwa na ufisadi ni mambo ya kawaida kabisa, kiasi kwamba, mwananchi anayekwenda kinyume cha mwlekeo huu wa kijamii, anaonekana kuwa ni kituko! Dhamiri za watu zinaanza kuharibika kiasi kwamba, watu wanashindwa kuona ubaya wa dhambi na badala yake, fedha imewekwa mbele kwa mambo mengi!

Yote ni mambo ambayo yanaendelea kubomoa misingi ya ustawi na maendeleo ya wananchi wa Ghana! Hapa kuna haja ya kubadilisha mwelekeo kwa kujikita katika kanuni maadili na utu wema, kila mtu akijitahidi kuwa kweli ni shuhuda wa imani yake. Maaskofu wanawahamasishwa wananchi kujenga na kuimarisha utamaduni wa msamaha, ukweli na upatanisho badala ya kuendekeza tabia ya kutaka kulipizana kisasi!

Baraza la Maaskofu linapenda kuwaonya Mapadre na Watawa kusimama kidete katika misingi ya Kiinjili, utu na maadili mema na kamwe wasikubali kumezwa na malimwengu kwa kuthamini na kupenda mno fedha na mali; mambo ambayo yanaweza kuwaletea hatari katika utekelezaji wa majukumu yao katika maisha na utume wa Kanisa. Wasipokuwa makini wanaweza kujikuta “wakila kwenye nyumba za wajane na maskini” wanaowaendea kutafuta suluhu ya matatizo na changamoto za maisha.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.