Katika Maandiko Matakatifu tunasoma yafuatayo: "Mara akaongozwa na Roho kwenda jangwani,
akakaa huko siku arobaini akijaribiwa na shetani" (Marko 1:12-13).Yesu anaenda Jangwani
na kukaa huko kwa muda wa siku arobaini. Lengo la kwenda jangwani si kujaribiwa ila
kujiandaa kwa kazi iliyokuwapo mbele yake, kazi ya kumkomboa mwanadamu. Yesu alikwenda
kutafakari kazi yake yote na yale yatakayompata katika kazi hiyo. Yesu alikwenda kutengeneza
dira ya utekelezaji wa kazi ya ukombozi. Nasi tunapoanza Mwaka Mpya 2015 tunahitaji
kuingia katika 'jangwani' la kiroho na kimaisha ili kujitengenezea dira ya utekelezaji
kwa mwaka mzima. Tujiwekee malengo binafsi, malengo ya familia, Jumuiya, kanda, kigango,
parokia, jimbo na mahali pa kazi. Ni kipindi cha kujiwekea malengo ya kiroho, kiuchumi
na kijamii. Mathalani. Mfano : KIROHO: Jipangie mwaka huu unataka kufika wapi?
Panga mambo yako ya kukua kiroho;tafakari ya Neno la Mungu; sala binafsi, sala za
familia, ushiriki wako katika Jumuiya, kanda, kigango, parokia na kijimbo. Panga kushiriki
mafungo ya kiroho, semina za kiroho, hija na matendo ya huruma. Ushiriki wako katika
vipindi vya Kwaresma, Pasaka, Majilio na Krismas n.k. KIUCHUMI: Tengeneza dira
ya kiuchumi mwanzoni mwa mwaka kwa kupanga unataka kufika wapi kiuchumi mwaka huu.
Usiache suala la uchumi likuendeshe bali wewe ulitawale kwa kufuata utakachojipangia
mwanzoni mwa mwaka. Utajikuta unafanya mambo mengi kwa mpangilio hadi unafurahia maisha.
Panga bajeti ya mwaka mzima; mapato na matumizi yako yaandike ili yakuongoze. Bajeti
yako iwe shirikishi ili itekelezeke, isiwe siri yako. Shiriki au ongoza kupanga bajeti
ya mwaka ya familia, jumuiya, parokia, jimbo na mahali pa kazi. Iheshimu bajeti hiyo.
Bajeti yako ianze na matumizi ili ikuongoze kupanga mapato. Kama mapato ni madogo
kulingana na matumizi; fanya ubunifu, fikiria fursa mpya na zifanyie kazi, pia punguza
matumizi yasiyo ya lazima, kadi za michango isiyo ya lazima, vikao visivyo na tija
vitakavyokugharimu n.k. Wakati mwingine ni heri ya lawama kuliko fedheha! Panga
zaka yako, sadaka, majitoleo, michango ya Jumuiya, mavuno ya parokia, mavuno ya jimbo
n.k usikurupuke kila siku na kwenda kutoa 'makombo' hayana nafasi mbele ya Mungu ni
sawa na kujiletea 'laana' maishani mwako. Mambo mengine muhimu ya kupanga katika
dira ya mwaka huu ni pamoja na kushiriki matukio muhimu ya kijamii. Ni mwaka wa kura
za maoni ya kupata katiba ya nchi yetu, usithubutu kupanga kutokushiriki, huo ni wajibu
wa kila raia wa Tanzania. Kushiriki uchaguzi mkuu wa madiwani, wabunge na Rais.
Ili tupate viongozi wazuri, wachamungu, waadilifu na wakweli, jitokeze ili uchaguliwe
na/au uchague kiongozi atakayetufaa kuiongoza jamii na nchi yetu. Mwaka wa Familia
utafungwa rasmi mwaka huu, Je, umeambulia nini kiimani? Umejiwekea mikakati gani ya
kutengeneza mapungufu yaliyo ndani ya familia yako? Shiriki vyema semina za mwaka
wa familia. Huu pia ni Mwaka wa Watawa Duniani, Je, unashiriki namna gani katika kuhamasisha,
kukuza na kulea miito mitakatifu ndani ya Kanisa? Huu ni mwaka wa uchaguzi wa viongozi
wa Kanisa - walei kuanzia ngazi ya Jumuiya ndogondogo hadi Taifa. Jitokeze uchaguliwe
na uchague viongozi hao. Shiriki kikamilifu kwani kanisa linakuhitaji. Yote hayo
yanatuhitaji kwenda 'jangwani' ili kujipanga. Tumshirikishe Mungu kupitia sala na
mafungo. Tumkabidhi Mungu malengo yetu ya mwaka 2015. Tujitathmini mara kwa mara juu
ya utekelezaji wa malengo hayo. Tuache kuishi kwa mazoea, mwaka 2015 tuwe wahalisia,
tusibahatishe! Tuepuke mikwaruzano, tuongeze furaha na ufanisi. Tuwe 'Kristu' katika
maisha yetu ya kila siku ili kuisaidia jamii. Tuache kulalamika lalamika, tuchukue
hatua. Wapendwa, Heri ya Mwaka Mpya 2015! Na Antipasi Shinyambala! Dar es
Salaam, Tanzania.