Jengo jipya kutumika katika kuwafunda Majandokasisi!
Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican katika Maadhimisho ya Siku kuu ya
Tokeo la Bwana, tarehe 6 Januari 2015, anatarajiwa kufungua Jengo jipya katika Chuo
cha Kipapa kwa ajili ya wanafunzi kutoka Marekani wanaofundwa kwenye vyuo mbali mbali
vya kipapa mjini Roma. Jengo hili jipya ni sehemu ya maboresho ya majengo ya Chuo
hiki yaliyojengwa kunako mwaka 1953, kwa ajili ya kutoa hifadhi kwa Majandokasisi
wanaojiandaa kwa ajili ya Daraja takatifu la Upadre.
Taarifa zinaonesha kwamba,
kutokana na kuongezeka kwa idadi ya miito, viongozi wa Kanisa waliamua kuongeza majengo
mengine, ili kuhakikisha kwamba, Majandokasisi wanapata majiundo makini katika maisha
yao ya kiroho, kiutu na kiakili, tayari kujisadaka kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake.
Jengo hili lina Kikanisa ambacho kimewekwa chini ya ulinzi wa Mtakatifu Yohane
Paulo II; hapa ni mahali pa sala na tafakari kwa ajili ya Waseminari. Kikanisa hiki
kinapambwa na picha za watakatifu ambao wamejipambanua kwa katika mchakato wa Uinjilishaji
mpya; Tafakari ya Neno la Mungu na Matendo ya huruma, kama ilivyokuwa kwa Mama Theresa
wa Calcutta.