2015-01-03 10:33:49

Kanisa linahitaji "majembe" yaliyoandaliwa barabara!


Mababa wa awamu ya pili ya Sinodi ya Maaskofu wa Afrka walikazia kwa namna ya pekee umuhimu wa majiundo makini ya Waseminari katika masuala ya kitaalimungu na maisha ya kiroho; bila kusahau mambo msingi ya makuzi ya kiakili na kiutu ya kila Mseminari. Mapadre wa baadaye hawana budi kukuza uelewa sahihi wa utamaduni wao bila ya kufungwa na ukabila au mahali anapotoka mtu. RealAudioMP3

Ni watu wanaopaswa kukita maisha yao katika tunu msingi za maisha ya Kiinjili, ili kuimarisha majitoleo na sadaka yao kwa Kristo na Kanisa lake. Lazima wajenge na kudumisha uaminifu kwa Kristo na Kanisa lake kwa njia ya maisha bora ya sala, tafakari ya Neno la Mungu, Sakramenti za Kanisa, daima wakijitahidi kuwa kweli ni watu wa Mungu wanaotafuta kuishi katika misingi ya haki, imani, upendo, udumifu na utaratibu. Waseminari hawana budi kukazia maisha ya kijumuiya, ili kupata majiundo makini yanayozingatia maisha ya mtu mzima: kiroho na kimwili.

Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita katika barua yake kwa Waseminari alikumbusha kwamba, maisha Seminarini ni muda wa matayarisho kwa maisha na wito wa Kipadre; ni muda wa kujifunza, kufanya maamuzi, malezi pamoja na makuzi ya kiutu na kiroho, ili hatimaye, waweze kukomaa katika maamuzi ya maisha yao ya baadaye kama Mapadre. Waseminari wanatakiwa wasiogope kufanya maamuzi magumu kwa kukumbatia maisha na wito wa Kipadre kwani kuna watu wengi wanawasindikiza kwa njia ya sala na sadaka zao

Baba Mtakatifu Francisko hivi karibuni katika ujumbe wake kwa Waseminari kutoka Ufaransa waliokuwa wanafanya hija yao ya maisha ya kiroho kwenye madhabahu ya Bikira Maria wa Lourdes, aliwataka kujikita katika udugu, sala; maisha na utume wa Kanisa.

Hivi karibuni, Padre Reginald Mrosso, Mkuu wa Shirika la Wamissionari wa Damu Azizi ya Yesu alizundua rasmi Mwaka wa Pili wa Malezi kwa Majandokasisi wa Shirika la Wamissionari wa Damu Azizi ya Yesu, Parokiani Chibumagwa, Jimbo Katoliki Singida, kwa kuwataka Waseminari hawa kudumisha umoja, udugu na upendo na kwamba, Familia ya Mungu inawajibika kukuza na kulea miito mitakatifu, kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa la Kristo.

Waseminari hawa wameanza mwaka huu wakati Shirika la linajiandaa kwa ajili ya maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 200 tangu Mtakatifu Gaspar Del Bufalo alipoanzisha Shirika la Wamissionari wa Damu Azizi ya Yesu. Shirika pia nchini Tanzania liko katika kipindi cha mpito, kuelekea katika ukomavu kwa kuwa ni Kanda kamili inayojitegemea, changamoto ya kukazia majiundo makini, ili kweli Shirika liweze kupata majembe ya nguvu katika mchakato wa Uinjilishaji wa kina unaogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili.

Padre Mrosso amewataka Waseminari hao kuanza kujizoesha kujisadaka kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake, tayari kujitoa bila ya kujibakiza katika kuwatangazia Watu wa Mataifa Injili ya Furaha; huku wakiwa kweli ni vyombo vya haki, amani, furaha na matumaini kwa walimwengu waliojikatia tamaa kutokana na kumezwa mno na malimwengu. Mwaka huu, Mafrateri walioanza mwaka wa pili wa malezi ni wanane; hawa ni wale waliohitimu masomo yao ya Falsafa na wako chini ya uongozi wa Padre Gregory Mkhotya, C.PP.S. Mkuu wa nyumba ya Malezi ya Mtakatifu Francisko Xsaveri, iliyoko Parokia ya Chibumagwa, Jimbo Katoliki la Singida.

Na Rodrick Minja,
Dodoma, Tanzania.








All the contents on this site are copyrighted ©.