2015-01-02 10:09:32

Simameni kidete kutangaza Injili ya Uhai


Umoja wa wanavyuo wa Kanisa Katoliki (Tanzania Movement Of Catholic Students – TMCS), wamesema wanakubaliana na mafundisho ya Kanisa katika uzazi salama kwa kutumia njia za asili badala ya kukumbatia utamaduni wa kifo unaofumbatwa katika sera za uzuiaji na utoaji mimba, mambo ambayo yanakwenda kinyume kabisa cha haki msingi za binadamu na chanzo cha kutoweka kwa amani na utulivu. Vijana wanapaswa kujengewa uwezo wa kusimama kidete kutangaza Injili ya Familia kwa kujikita katika maadili na utu wema!

Mratibu wa TMCS Mathias Kabyemela, alitoa kauli hiyo wakati akitoa ufafanuzi kuhusu mafunzo ya siku tatu wa wanachama 210 wa TMCS waliokuwa wamekutanika hivi karibuni katika ukumbi wa St. Claver nje kidogo ya mji wa Dodoma. Kabyemela alisema umoja wao unaamini na utaendelea kuamini kuwa njia za asili ndizo zinazofaa kwa vijana wa Kitanzania katika kupanga uzazi kuliko kutumia njia za kisasa ikiwemo sindano za kuzuia mimba.

Alisema Umoja wao ambao unaunganisha vyuo vya kati na vyuo vikuu 103 nchini Tanzania, umekuwa ukifanya kazi ya kutoa elimu kwa vijana wasomi ambao nao hutumia nafasi zao kutoa elimu kwa vijana wenzao mara warudipo vijijini na katika makazi yao. “Huu kwetu ni mkutano wa sita ingawa TMCS inatimiza miaka 30 sasa, lakini bado tunaunga mkono msimamo wa Kanisa katika suala zima la kupanga uzazi tukijua kuwa kutumia kalenda ndyo njia sahihi zaidi kuliko vitu vingine,” alisema Kabyemela.

Kuhusu umoja huo alisema umefanikiwa kwa kiasi kikubwa katika kuwaunganisha vijana wa Tanzania na nje ambao wanafanya kazi ya kuinjilisha kwa ushirikiano mkubwa. Nchini Tanzania alisema wameganya uongozi wa umoja huo katika kanda 14 ambazo wanaziita ni majimbo na maeneo hayo yana uongozi kwa kila chuo kwa ajili ya uwakilisha jambo linalofanya huduma yoa kuwa nyepesi zaidi.

Akitoa mada katika warsha hiyo, Padri Aman Nyoni, aliwataka vijana kujitambua na kutumia nafasi walizonazo kuwaelimisha wenzao ambao hawakubahatika kupata elimu ya kutosha kuhusiana na Injili ya Uhai, ili waweze kusimama kidete, kulinda, kutetea na kuendeleza Injili ya Uhai kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao adili na manyofu yanayosimikwa katika dhamiri nyofu, Neno la Mungu na Mafundisho ya Kanisa.

Padre Nyoni alisema suala la usiri ndilo ambalo linawapelekea wasichana wengi wengi kujikuta wakitumbukia katika ujauzito kwani wanakuwa hawana elimu ya kutosha kuhusu maisha na maumbile yao.

Naye mlezi wa Umoja huo kwa kanda ya Tabora ambaye pia alikuwa akikaimu nafasi ya ulezi taifa katika mkutano huo Padri Josephat Mande, alitaja lengo la mikutano hiyo ni kuwafunda vijana katika Uinjilishaji katika nyakati hizi za ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya teknolojia, ili vijana waweze kuwa macho na kamwe wasikubali kumezwa na malimwengu, kwani huko watakiona cha mtema kuni!

Na Rodrick Minja,
Dodoma, Tanzania.








All the contents on this site are copyrighted ©.