2015-01-01 13:59:25

Simameni kidete kupambana na mifumo yote ya utumwa!


Baba Mtakatifu Francisko wakati wa Sala ya Malaika wa Bwana, katika Maadhimisho ya Siku kuu ya Bikira Maria Mama wa Mungu sanjari na Siku ya 48 ya kuombea amani duniani, kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican tarehe Mosi, Januari 2015 amemwelezea Bikira Maria kuwa ni mwanamke mnyenyekevu aliyekubali Neno wa Mungu kutungwa mimba tumboni mwake, kiasi kwamba, si rahisi kuweza kutenganisha Bikira Maria na Yesu!

Bikira Maria amemkiria Yesu Mwana wa Mungu ubinadamu wake, kiasi hata cha kuzaliwa chini ya sheria, ili aweze kumkomboa mwanadamu kwa njia ya sheria, inayomweka mtu huru na kuzaliwa tena kama mwana mpendwa wa Mungu, kwa njia ya mateso, kifo na ufufuko wake na kwa njia ya Ubatizo, aweze kufanyika kuwa ni mtoto mteule wa Mungu; tukio linalowaunganisha Wakristo kuwa viumbe hai katika Fumbo la Mwili wa Kristo, yaani Kanisa.

Siku ya kwanza ya Mwaka, iwe ni fursa ya kukumbuka ile Siku ya Ubatizo, pale waamini walipozaliwa upya kwa maji na Roho Mtakatifu, kwa njia ya Mama Kanisa na Bikira Maria ni mfano kamili wa umama huu. Ubatizo unawaunganisha na Mungu na hivyo kupokea upendo, upole na huruma kutoka kwa Mwenyezi Mungu, chemchemi ya amani ya kweli inayowafanya huru na wala si watumwa, bali ndugu, kauli mbiu ya ujumbe wa Siku ya Kuombea Amani Duniani kwa Mwaka 2015.

Watu wote wanahamasishwa kupambana na mifumo mbali mbali ya utumwa, ili kujenga na kudumisha udugu, kila mtu kadiri ya dhamana na madaraka aliyo nayo!

Mara baada ya Sala ya Malaika wa Bwana, Baba Mtakatifu Francisko amewatakia wote amani, furaha na baraka tele kwa Mwaka Mpya. Amewapongeza kwa namna ya pekee watoto kutoka Ujerumani, Austria na Uswiss ambao wametembea nyumba hadi nyumba kwa ajili ya kutafuta fedha ya kusaidia kugharimia miradi kwa ajili ya watoto wanaoishi katika mazingira magumu.

Baba Mtakatifu anawashukuru wote walioshiriki katika maandamano ya kuombea amani kitaifa, nchini Italia, yaliyofanyika Jimboni Vicenza, Kaskazini mwa Italia, ili kuombea amani duniani kote, utume ambao umetekelezwa na majimbo mbali mbali duniani. Baba Mtakatifu amewakumbuka pia wahanga wa vita kuu za dunia na kwamba, anatumaini kuwa hakutakuwepo tena na vita na badala yake, amani na udugu vitaweza kutawala kati ya watu.







All the contents on this site are copyrighted ©.