2015-01-01 08:16:31

Jubilee ya miaka 450 ya Mji wa Rio de Janeiro!


Jubilee ya miaka 450 tangu kuundwa kwa mji wa San Sebastiano Rio de Janeiro, Brazil, kumbu kumbu ya maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani kwa mwaka 2013 na miaka 50 tanu Mwenyeheri Papa Paulo VI alipowasha taa kwenye Sanamu ya Kristo Mfalme, iliyotundikwa kwenye kilele cha Mji wa Rio de Janeiro ni matukio ambayo yamegusa sakafu ya moyo wa Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake kwa wananchi wa Brazil, wanaoadhimisha kumbu kumbu ya matukio haya muhimu katika historia yaliyozinduliwa katika mkesha wa Mwaka Mpya 2015.

Baba Mtakatifu anasema miaka 450 si haba! Hii ni historia ya watu wenye ujasiri na furaha na kamwe hawakuacha kutikiswa na magumu ya maisha, bali wameendelea kuonesha ushuhuda wa imani tendaji kwa Kristo na Kanisa lake, kama alivyofanya Mtakatifu Sebastiani, Mlinzi wao. Hii ni historia inayojikita katika imani na matumaini kwa Mwenyezi Mungu pamoja na kuendelea kuonesha uchaji, huku wakitumainia huruma yake.

Baba Mtakatifu anawapongeza kwa kubahatika kuwa na mji wenye maajabu yanayowashangaza wengi, lakini pia kuna umaskini unaotia giza uzuri na maajabu ya mji huu, kutokana na ukosefu wa usawa kijamii; kuna uhalifu wa kutisha, ukosefu wa haki pamoja na kundi kubwa la watu ambao wanatamaduni maalum; yote haya yasiwafanye watu kupoteza matumaini, kwani Mwenyezi Mungu yupo pamoja nao na kwamba, Yesu Mkombozi hawezi kamwe kufumbia macho mateso na mahangaiko ya watu wake.

Mikono yake wazi, inawachangamotisha waamini na watu wenye mapenzi mema kuvuka vikwazo vya kinzani, ili kujenga mji unaosimikwa katika umoja, mshikamano, haki na amani! Watu wajenge utamaduni wa kujadiliana, ili kudumisha umoja na mshikamano wa kitaifa, kwani kila mwananchi analo jambo ambalo anaweza kuchangia katika mchakato wa ujenzi wa utamaduni wa haki na udugu. Watu wanaweza kujifunza kujenga moyo wa ukarimu na mshikamano kutoka kwa watu wa kawaida kabisa. Brazil bado ina mchango mkubwa katika ustawi na maendeleo ya ulimwengu.

Mwishoni, Baba Mtakatifu Francisko anamshukuru Kardinali Oran Tempesta kwa kumpatia nafasi ya kutoa ujumbe kwa wananchi wa Brazil wakati huu wanapoadhimisha Jubilee ya miaka 450 tangu kuanzishwa kwa mji wa Rio de Janeiro. Anawatakia wote heri na baraka kwa Mwaka Mpya wa 2015, anawaomba kumsindikiza kwa sala na sadaka zao katika maisha na utume wake.







All the contents on this site are copyrighted ©.