Vijana wa Jumuiya ya kiekumene Taizè kutoka katika nchi mbali mbali za Ulaya, ambao
kuanzia tarehe 29 Desemba hadi tarehe 2 Januari mwaka 2015 wanakutanika awamu ya thelathini
na saba nchini Jamhuri ya Watu wa Czech, inayoadhimisha Jubilee ya Miaka 25 tangu
demokrasia ilipojereshwa tena nchini humo, baada ya Wakristo wengi kupoteza maisha
yao kutokana na imani yao kwa Kristo na Kanisa lake.
Hili ni kundi la watu
lililonyanyaswa na kudhulumiwa, lakini bila kukata tamaa, kiasi kwamba, njia ya uhuru
na demokrasia ikapatikana. Vijana wa Jumuiya ya Kiekumene ya Taizè wanahamasishwa
kushiriki katika hija hii kwa njia ya sadaka ya maisha yao, huku wakijiachilia na
kujifunza kutoka kwa Bikira Maria aliyekubali kuwa ni Tabernakulo ya kwanza ya Neno
wa Mungu aliyefanyika mwili! Injili ya uhai haina budi kukuzwa na kuendelezwa katika
undani wa maisha ya vijana.
Hii ni sehemu ya ujumbe wa Baba Mtakatifu Francisko
ulioandikwa kwa niaba yake na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa vatican kwa
ajili ya maadhimisho ya Siku ya 37 ya Vijana wa Jumuiya ya Kiekumene ya Taizè kwa
mwaka 2015. Baba Mtakatifu anawahamiza vijana kujikita katika mchakato wa sala, majadiliano
ya kidini na kiekuemene, ili kweli waweze hatimaye, kuwa ni chumvi ya dunia na mwanga
wa mataifa pamoja na kutambua kwamba, Yesu Kristo ana matumaini makubwa kwa vijana.
Baba
Mtakatifu anawakumbusha vijana kwamba, mapungufu yao ya kibinadamu na umaskini unaowaandama
kisiwe ni kikwazo, bali waendelee kumwamini Roho Mtakatifu anaishi na kutenda ndani
mwao, changamoto na mwaliko wa kupokea ujumbe wake kwa moyo mkuu, ili dunia iweze
kuwa ni mahali pazuri pa kuishi kwa kujikita katika umoja na Mwenyezi Mungu pamoja
na mshikamano wa kidugu.
Baba Mtakatifu anawaambia vijana kwamba, anawaamini
kwa kukirimiwa vipaji mbali mbali pamoja na ugunduzi, ili kweli Injili ya Furaha iweze
kuwafikia na kusikilizwa na watu wengi zaidi katika nchi zao. Inapendeza kuwaona vijana
wakichakarika kwa ajili ya kushuhudia imani yao na kumtangaza Yesu katika mitaa, barabara
na sehemu mbali mbali za dunia.
Vijana ni jeuri ya Kanisa, wanaolihamasisha
Kanisa kusonga mbele katika kukamilisha mchakato wa umoja kamili kati ya Wakristo.
Baba Mtakatifu Francisko anapenda kuchukua fursa hii kuwatakia kheri na baraka tele
katika maadhimisho haya!
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili
ya Radio Vatican.