2014-12-30 10:03:44

Ujumbe wa Papa Francisko kwa Siku ya Kuombea Amani Duniani 2015


Mama Kanisa tarehe Mosi, Januari 2015 anaadhimisha Siku ya Kuombea Amani Duniani inayoongozwa na kauli mbiu “si tena kama mtumwa, bali ndugu”. Maadhimisho haya yanakwenda sanjari na Siku kuu ya Bikira Maria Mama wa Mungu. RealAudioMP3

Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake kwa Maadhimisho ya Siku ya Kuombea Amani Duniani, anaugawa ujumbe wake katika sehemu kuu mbili, zenye utangulizi unaonesha mpango wa Mungu katika maisha ya mwanadamu.

Sehemu ya kwanza, Baba Mtakatifu anapembua kwa kina na mapana mambo mbali mbali kuhusiana na utumwa katika historia ya maisha ya mwanadamu; sababu zake msingi na sehemu ya pili anaihamasisha Jumuiya ya Kimataifa kutafuta suluhu ya pamoja itakayoiwezesha Jamii ya mwanadamu kupambana fika na kashfa ya utumwa ambayo ni uhalifu dhidi ya ubinadamu.

Baba Mtakatifu anaanza utangulizi wa ujumbe wake kwa kumtolea Mwenyezi Mungu sala, ili vita, kinzani na mateso yanayosababishwa na binadamu yaweze kupata ukomo wake; anasali kwa ajili ya kuombea wale wote ambao wameguswa kwa namna ya pekee na mlipuko ya magonjwa na majanga asilia na kukumbusha kwamba, mwanadamu ameumbwa kwa ajili ya kujenga na kudumisha mahusiano na jirani zake kwa kuzingatia msingi wa haki na mapendo.

Hapa Baba Mtakatifu anawataka watu kutambua na kuheshimu: utu, uhuru na hali ya mtu kujitegemea, hali ambayo inapaswa kuonesha mahusiano kati ya watu kwa kukazia kwa namna ya pekee kabisa: heshima, haki na upendo. Udugu unaopata chimbuko lake kwa kumwongokea Kristo ni kifungo muhimu katika maisha ya kifamilia na kijamii, hali inayoonesha umoja katika utofauti ulioko kati ya wanandugu, walioumbwa kwa sura na mfano wa Mungu, wakiwa na asili na utu sawa.

Baba Mtakatifu anasema, dhambi inapoharibu mshikamano huu wa kidugu, hapo utamaduni wa utumwa unajipenyeza na kutoa nafasi kwa mtu kumkataa jirani yake, nyanyaso na madhulumu zinapoonekana; utu na heshima ya binadamu vinatoweka na haki msingi za usawa katika taasisi zinamong’onyoka. Kutokana na mapungufu yote haya, Jumuiya ya Kikristo haina budi kuwa ni kielelezo cha umoja kati ya ndugu kwa kuonesha umoja katika utofauti bila kuathiri utu wala kumtenga mtu yoyote kutoka katika Familia ya Mungu. Hii ni kwa sababu wote ni watoto wateule wa Mungu wanaoimarishwa kwa kifungo cha udugu katika Kristo.

Sehemu ya kwanza, katika Ujumbe wa Kuombea Amani Duniani kwa Mwaka 2015, Baba Mtakatifu Francisko anaangalisha juu ya mabadiliko makubwa ambayo yamejitokeza katika historia ya mwanadamu kwa kutambua utu na heshima ya binadamu na kwamba, utumwa ni kitendo kinachodhalilisha na kufisha utu na heshima ya binadamu; jambo ambalo limepelekea utumwa kupigwa marufu kutoka katika uso wa dunia na kwamba, ni marufuku mtu kuingizwa katika utumwa, sheria ambao bado inaacha maswali mengi bila ya kuwa na majibu muafaka.

Baba Mtakatifu anasema hata leo hii, kuna watu wanalazimika kuishi katika mazingira ya utumwa, kwani kuna mifano hai inayoonesha kwamba, kuna watu wanafanyishwa kazi za kitumwa; wahamiaji wananyimwa haki zao msingi; wanadhulumiwa na kunyanyaswa; wanawekwa kizuizini katika mazingira hatarishi; wananyanyaswa na kudhulumiwa na waajiri kwa kudhibiti mikataba na vibali vya kuishi ugenini.

Kuna wanawake, wasichana na watoto ambao wametumbukizwa katika biashara haramu ya ngono; wengine wanauzwa kama biadhaa na kulazimishwa kufunga ndoa za shuruti. Kuna baadhi ya watu wanatumbukizwa katika biashara haramu ya viungo vya binadamu; watoto wanapelekwa mstari wa mbele kama chambo katika mapigano ya kivita; kuna baadhi ya watoto wanaolazimishwa kuuza dawa haramu za kulevya na wengine wanaasiliwa kinyume cha sheria za kimataifa. Kuna baadhi ya watu wametekwa nyara na kufungwa na vikundi vya kigaidi.

Baba Mtakatifu anasema, hizi zote ni sura za utumwa mamboleo na kwamba, zina sababu nyingi ambazo zimepelekea kuendelea kuwepo kwa biashara na utumwa mamboleo. Sababu msingi ni dhambi inayoathiri moyo wa binadamu kiasi hata cha kuukataa ubinadamu wa mtu mwingine, hali inayowafanya baadhi ya watu kuwanyanyasa na kuwatumisha binadamu wenzao kama bidhaa na njia ya kujinufaisha binafsi.

Mambo mengine ni umaskini, ujinga, ukosefu wa fursa za ajira, biashara haramu ya binadamu na matumizi haramu ya mitandao ya kijamii inayowafanya vijana wa kizazi kipya kuwa watumwa pamoja na kuvutiwa kujiunga katika makundi ya kivita, uhalifu, matumizi ya nguvu pamoja na kujihusisha na vitendo vya kigaidi.

Baba Mtakatifu anasema sababu nyingine zinazopelekea uwepo wa utumwa mamboleo ni pamoja na rushwa na ufisadi unaojipenyeza katika vyombo vya ulinzi na usalama kwa kushirikiana na magenge ya uhalifu wa kitaifa na kimataifa, hapa ut una heshima ya binadamu vinawekwa rehani na badala yake, fedha inapewa kipaumbele cha kwanza.

Katika sehemu ya pili ya Ujumbe kwa Siku ya Kuombea Amani Duniani, Baba Mtakatifu Francisko anaihamasisha Jumuiya ya Kimataifa kushikamana kwa dhati katika mapambano dhidi ya utumwa mamboleo kwa kujenga na kuimarisha utandawazi wa udugu. Biashara haramu ya binadamu na utumwa mamboleo ni mambo ambayo yanapata mwanya kutokana na baadhi ya watu kutojali. Lakini, Baba Mtakatifu anasema, kuna kundi kubwa la Watawa wa Kike linalofanya utume wake katika hali ya ukimya, ili kuwasaidia waathirika wa utumwa mamboleo sanjari na kuvunjilia mbali mnyororo wa utumwa unaonyanyasa, dhulumu na kuwatesa watu kiasi hata cha kuwanyang’anya hati na vitambulisho vyao.

Baba Mtakatifu anasema kwamba, kwa njia ya ujasiri, uvumilivu na udumifu, Mashirika ya kitawa yameendelea kuwa karibu zaidi na waathirika wa utumwa mamboleo; kwa kuwasaidia, kuwapatia ushauri nasaha na hatimaye, kuwaingiza tena katika jamii husika. Jumuiya ya Kimataifa haina budi kulivalia njuga tatizo hili, ili kuzuia uhalifu, kuwalinda wahanga pamoja na kuwawajibisha watuhumiwa wa vitendo hivi vinavyodhalilisha utu na heshima ya binadamu. Hapa kuna haja ya kuwa na umoja na mkakati wa kimataifa kwa kuhakikisha kwamba, sheria kuhusu wahamiaji, ajira, kuasili pamoja na mgawanyo wa maeneo ya kazi zinatekelezwa kikamilifu, kwa kulinda, kuheshimu na kutetea utu wa binadamu.

Kuna haja ya kuwa na sheria zinazosimikwa katika haki na zinazolinda haki msingi za binadamu bila kutoa mwanya kwa wala rushwa na mafisadi kuendelea “kupeta, huku wakila kuku kwa mrija” bila ya kuwajibishwa kikamilifu. Wanawake wanapaswa kuheshimiwa na kuthaminiwa kutokana na dhamana yao ndani ya Jamii; waajiri wahakikishe kwamba, wafanyakazi wanatekeleza wajibu wao katika mazingira bora zaidi, kwa kulipwa ujira stahiki, bila ya kujihusisha na biashara haramu ya binadamu.

Taasisi na Mashirika ya kitaifa na kimataifa yajifunge kibwebwe kuhakikisha kwamba, yanavunjilia mbali magenge ya uhalifu wa kimataifa, kwa kuwawajibisha wahusika. Walaji watambue wajibu wao wa kijamii kwani tendo la kununua linafumbata kanuni maadili na mafao ya kiuchumi.

Baba Mtakatifu Francisko anasema, Vatican itaendelea kusimama kidete kupinga biashara na utumwa mamboleo kwa kukazia utandawazi wa kidugu badala ya kuendeza utandawazi usiojali wala kuguswa na mahangaiko ya binadamu wengine. Mtakatifu Bhakita awe ni mfano wa matendo ya kidugu kwa wale wanaoishi katika utumwa. Watu wanapaswa kuhamasishwa kuona nyanyaso na dhuluma wanazofanyiwa watu wanaotumbukizwa katika biashara haramu ya binadamu zinakoma na kamwe wasibezwe.

Baba Mtakatifu Francisko anahitimisha ujumbe wake kwa Siku ya Kuombea Amani Duniani kwa Mwaka 2015 kwa kuwataka waamini na watu wote wenye mapenzi mema kutojihusisha na matendo yanayodhalilisha utu na heshima ya binadamu; waone na kuguswa na mateso pamoja na mahangaiko ya binadamu ambao wanapokwa uhuru na utu wao; watu wawe na ujasiri wa kugusa mateso na mahangaiko ya Kristo kwa njia ya wahanga hawa.

Utumwa mamboleo ni changamoto ya kimataifa inayoonesha utandawazi usiojali wala kuguswa na mateso ya watu; uhalifu ambao unapaswa kudhibitiwa kwa kujenga utandawazi wa mshikamano na udugu, ili kuwapatia wahanga wa vitendo hivi matumaini katika maisha yao!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.