2014-12-30 10:07:03

Siku kuu ya Bikira Maria Mama wa Mungu, 2015


Tarehe Mosi Januari, Siku kuu ya Bikira Mama wa Mungu, Theotokos, inayokwenda sanjari na maadhimisho ya Siku ya 48 ya Kuombea Amani Duniani, inayoongozwa na kauli mbiu “si tena kama mtumwa bali ndugu”, Baba Mtakatifu Francisko anatarajiwa kuongoza masifu ya kwanza ya jioni Jumatano tarehe 31 Desemba 2014, majira ya saa 11:00 kwa saa za Ulaya kwa ajili ya Siku kuu ya Bikira Maria Mama wa Mungu. RealAudioMP3

Katika masifu haya, kutakuwa na Ibada ya Kuabudu Ekaristi Takatifu, chanzo na kilele cha maisha na utume wa Kanisa na baadaye, waamini wataimba Utenzi wa shukrani, “Te Deum” kama alama ya kumshukuru Mungu kwa kufunga mwaka wa Serikali. Ibada hii itafungwa rasmi kwa baraka ya Ekaristi Takatifu.

Alhamisi, tarehe Mosi, Januari 2015, Baba Mtakatifu Francisko ataunfungua Mwaka kwa kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwa heshima ya Bikira Maria Mama wa Mungu na Siku ya Kuombea Amani Duniani, kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican. Ibada hii inatarajiwa kuanza saa 4:00 asubuhi kwa saa za Ulaya.

Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican itaendelea kukujuza yale yatakayojiri katika maadhimisho haya! Tafadhali usikose kumshirikisha jirani yako!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.