Kardinali Polycarp Pengo, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Dar es Salaam, Jumatatu tarehe
29 Desemba 2014 ameongoza Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kumbu kumbu ya Watoto
Mashahidi waliouwawa kikatili na Mfalme Herode, aliposikia kwamba, kuna Mfalme amezaliwa
mjini Bethlehemu.
Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake kwa Siku kuu
ya Noeli aliwakumbuka kwa namna ya pekee, watoto wanaoendelea kufutiliwa mbali na
upanga wa Herode kutokana na magonjwa, ukatili, nyanyaso na vita na hata wakati mwingine
mbele ya macho ya waamini na Jumuiya ya Kimatifa.
Shirika la Kimissionari
la Kipapa la Utoto Mtakatifu, Jimbo kuu la Dar es Salaam, kila mwaka linaadhimisha
kumbu kumbu ya Watoto Mashahidi kama siku yao maalum, inayowakusanya watoto kutoka
katika Parokia zote za Jimbo kuu la Dar es Salaam, ili kumzunguka Kardinali Polycarp
Pengo, aweze kuwatia shime na ari ya kuwa ni Wamissionari kati ya watoto wenzao.
Kardinali
Pengo katika mahubiri yake, amewataka watoto kuiga mfano bora wa Mtoto Yesu katika
maisha na makuzi yao, kwa kutambua, nafasi, dhamana na utume wao ndani ya Kanisa na
ulimwengu katika ujumla wake. Watoto wakiandaliwa barabara wanaweza kutekeleza mambo
makubwa katika maisha na utume wa familia na wala si watu wa kutumwa peke yake.
Bikira Maria na Mtakatifu Yosefu walipompeleka Mtoto Yesu, Hekaluni, alibaki nyuma,
akiwafundisha wakuu wa makuhani kama sehemu ya utekelezaji wa mapenzi ya Baba yake
wa Mbinguni. Hata wazazi wake waliporudi Hekaluni na kumkuta akiwa amezungukwa na
wakuu wa Makuhani, wazazi wake hawakuwa na wasi wasi, bali walishangaa, Je, mtoto
huyu atakuwa ni wa namna gani? Yesu alikuwa anafundisha na kujibu maswali kwa ufundi
mkubwa, kiasi cha kuwaacha wataalam na mabingwa wa Maandiko Matakatifu wakiwa wameshikwa
na bumbuwazi.
Kardinali Pengo amewataka watoto kuwa macho na makini katika
mazingira na makundi yanayowazunguka, kwani yanaweza kuwatumbukiza katika mambo ambayo
yanaweza kumong’onyoa maadili na utu wema, kwa kuwapotosha katika maisha yao! Watoto
wamweke Kristo mbele ya macho yao, wanapokabiliana na changamoto za maisha; daima
wajitahidi kumshirikisha katika maamuzi na maisha yao ya kila siku. Kwa kufikiri na
kutenda kadiri ya Yesu, watoto hawa wanaweza kuwashangaza wengi, kwani watatambulikana
kutokana na tofauti yao na watoto wengine.
Kardinali Pengo amewataka watoto
kuachana na tabia mbaya zinazowafanya baadhi yao kuwa ni wadokozi, kukosa maadili
na kuwa na lugha chafu za matusi. Watoto watambulikane kwa kumuiga na kuishi kama
Mtoto Yesu, ili waweze kuwapiga bumbuwazi, wale wanawazunguka katika maisha. Watoto
waongozwe katika maisha yao na hekima pamoja na mapenzi ya Mungu.
Kardinali
Pengo amehitimisha mahubiri yake, kwa kuwatakia watoto wote tunza ya Mtoto Yesu, ili
aweze kukaa pamoja nao, kwa kuwaongoza na kuwaimarisha katika imani, matumaini na
mapendo kwa Mungu na jirani.
Na Padre Agapito Mhando, Idhaa ya Kiswahili
ya Radio Vatican.