2014-12-29 09:03:32

Tangazeni Injili ya Familia kwa njia ya ushuhuda wa maisha!


Katika maadhimisho ya Siku kuu ya Familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu, iliyoadhimishwa na Mama Kanisa jumapili tarehe 28 Desemba 2014, ni sehemu ya maandalizi ya kina kwa ajili ya maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu kuhusu familia, itakayofanyika mjini Vatican kuanzia tarehe 4 hadi tarehe 25 Oktoba 2015. RealAudioMP3

Katika mahojiano maalum na Radio Vatican, Askofu Joseph Mlola wa Jimbo Katoliki Kigoma, Tanzania, anawataka waamini kutambua kwamba, wao kimsingi wanaunda Familia ya Mungu, Kanisa dogo la nyumbani, changamoto na mwaliko kwa kila mwamini kujisikia kuwa ni sababu ya umoja, mshikamano na mapendo ndani ya familia, sanjari na kuendelea kuiga mfano bora kutoka kwa Familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu.

Askofu Mlola anawataka wanafamilia kujenga na kudumisha tunu msingi za maisha ya ndoa na familia, kwa kujikita katika tabia njema ya: kusamehe na kusahau; ya kutoa na kupokea msamaha; ya kumwomba na kumshukuru Mungu pamoja na jirani, kwani falsafa ya neon asante ni kuomba tena!

Askofu Mlola anazitaka familia kuwa na ujasiri, moyo na utamaduni wa kusahihishana na kurekebishana kwa imani, mapendo na udugu, ili familia ziweze kuwa wamoja kama ilivyokuwa kwa Familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.