Mpendwa msikilizaji wa kipindi chetu cha Kanisa la nyumbani, Tumsifu Yesu Kristo.
Mtaguso Mkuu wa II wa Vaticani unaendelea kukunong’onezea mambo mema, ili uweze kuwa
Mwamini hai, mwenye kujua na kutimiza wajibu wako vema ndani ya Kanisa. 00:11:58:46
Leo
tunalitazama agizo la Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican linaloitwa kwa lugha
ya Kilatini ‘Presybiterorum Ordinis’, ikimaanisha ‘daraja ya mapadre’. Ndanimwe imesheheni
utume na maisha ya mapadre, na pia wajibu wetu sisi kama waamini kwa mapadre. Kuna
wajibu wa kiroho na wajibu wa kijamii. Leo tutapigia mistari sana wajibu wetu wa kijamii
kwa mapadre wetu.
Kukukumbusha tu mpendwa msikilizaji katika Kanisa letu hili
zuri sana, kuna daraja tatu za wahudumu wa Daraja Takatifu. Daraja la kwanza ni Maaskofu,
hao huwekwa wakfu na Mama Kanisa, ili kulichunga kundi la Mungu. Maaskofu, wana utimilifu
wote wa Upadre. Ni kwa sababu hiyo, maaskofu peke yao ndio huweza kutoa sakramenti
ya daraja takatifu kwa wengine. Daraja la pili, ndilo la Mapadre. Hao hushirikiana
na Maaskofu katika masuala ya kichungaji.
Upadre ni daraja takatifu ngazi
ya pili. Na daraja la tatu ni Ushemasi. Hao humsaidia Askofu na Padre katika huduma
kwa kundi la Mungu. Kipindi kilichopita tulidadafua kidogo juu ya huduma ya Maaskofu
katika Kanisa. Leo tunawatazama Mapadre katika Kanisa kwa mwangwi wa hati hii tuliyokwishakuitaja.
Sura
ya kwanza inatueleza juu ya Upadre kama Utume ndani ya Kanisa. Utume huo unawaunganisha
Maaskofu na Mapadre kwa ajili ya kulihudumia taifa la Mungu. Askofu naye kimsingi
ni Padre, lakini ni Padre mwenye utimilifu wa upadre. Padre hupewa daraja hili na
Askofu. Na yeyote mwenye kupokea daraja la Upadre hapokei kwa ajili yake, bali kwa
ajili ya utume. Padre anapewa mamlaka na nguvu kwa ajili ya utume ndani ya Kanisa.
Utume kwa kunena siri za Kristo, kuadhimisha mafumbo ya Mungu kwa ajili ya wokovu
wa roho za watu.
Sura ya pili inafafanua zile kazi tatu za mapadre, ambazo
wanazishiriki kutoka kwa Askodu yaani kufundisha, kutakasa na kuongoza. Na kwa namna
ya pekee sura hii inaelekeza juu ya uhusiano wa Mapadre na Askofu wao uweje na pia
uhusiano kati yao, na tena uhusiano wao na waamini walei uweje.
Na katika sura
inayofuata, tunaona jinsi ambavyo sisi walei tunawajibika kwa Mapadre wetu. Kama wao
wanawajibika kwa maisha yao yote kwa ajili ya wokovu wa roho zetu, sisi nasi tunawajibika
kwa namna fulani kwa ajili ya usitawi na hali njema yao. Ndipo hati hii inatualika
sisi waamini kuwasaidia mapadre wetu kwa namna mbalimbali; iwe kwa maisha ya kiroho,
kuhusu elimu yao na kuhusu malipo ya haki na bima, hati inasema ‘ili wasije wakahangaika’.
Mwishoni mapadre wanatiwa moyo katika magumu yanayowakabili siku hizi, kwa kukumbusha
kinachojulikana kwa tu, kwamba na Kanisa wapo pamoja nao.
Mpendwa msikilizaji,
mara nyingi tumehimizwa juu ya kuwalea vizuri watoto wetu katika misingi ya imani
na maadili mema, ili mbegu njema ya wito wa huduma ya altare iweze kuwaka mioyoni
mwa watoto wetu, ikue na ichipue ili siku mmoja wajekuwa ni waadhimishaji na wagawaji
wa mafumbo ya Mungu katika Altare Takatifu ya Mungu. Na kuna baadhi ya sehemu ambako
kwa kweli kuna ukame wa miito. Hatupati mapadre kabisa. Waliopo ni wachache, hawatoshi
na pengine wamechoka vibaya.
Kwa njia ya tafakari ya hati hii, tukumbuke kwamba,
‘mapadre wanatoka kwetu wenyewe na kwa ajili yetu’. Ni wajibu wa kila moja ndani ya
Kanisa Takatifu, kuombea usitawi na udumifu wa miito mitakatifu ndani ya Kanisa. Na
kule kwenye familia zetu, kwenye ndoa zetu, tusikwepe wala kuogopa wajibu wa kuzaa
watoto na kuwatunza vyema. Utamaduni wa siku zetu hizi, unaangamiza miito kabisa.
Wengi wanapenda kuwa na mtoto mmoja tu, au wawili. Sasa katika familia tukizaa mtoto
mmoja, nani atakuwa Padre na nani atakuwa Daktari na nani atakuwa Askari? Tulitazame
hilo neno, kwa jicho wajibifu!
Lakini pia, tukumbuke, Mapadre wana wajibu wa
kutulisha sisi kwa neno na kwa sakramenti kwa njia ya maadhimisho ya altare na kwa
njia ya ushauri wao mwema kwetu. Kila Padre aliyewekwa wakfu, ni kuhani mkuu anayempendeza
Bwana katika maadhimisho Matakatifu. Ndiyo maana katika mafundisho yetu maalumu ya
ndani sana, tunaelekezwa kwamba, hata kama Padre anaonekana hapendezi katika macho
yetu kwa sababu iwayo yoyote, lakini Padre huyo akiadhimisha mafumbo matakatifu kwa
ajili ya taifa ya Mungu, taifa la Mungu linabarikiwa kweli.
Padre huyo akiwabariki,
mnabarikiwa kweli. Kwa nini?? Kwa sababu padre yoyote hufanya kazi katika Nafsi ya
Kristo na kwa jina la Kanisa! Mungu mwema na mwenye huruma, hutumia hata viumbe wanyonge
na wadhaifu sana kwa ajili ya wokovu wa watu wake. Kwa mantiki hiyo sisi waamini,
tujitahidi na tujitume sana kuwatunza na kuwasaidia mapadre wetu. Msaada wa kwanza
kabisa ni sala. Tuwaombee kila mara. Shetani anajua vizuri sana nguvu na mamlaka ya
Padre kuliko mwamini anavyojua. Ndiyo maana mapadre daima huelekezewa mashambulizi
mbalimbali na shetani. Shetani anataka kumpiga sana mchungaji ili kondoo watawanyike.
Ndio hapo tunapoomba na kusihi sana utume wa sala kwa ajili ya mapadre wetu.
Wakati
mwingine sisi waamini tunashika utume wa kuwasemasema, kuwakorofisha, kuwakwaza na
hata kuwabinafsisha na kuwaangusha mapadre wetu badala ya kuwaongoza. Hapo tunamsaidia
shetani ili kufanikisha miradi yake. Tuwaombee, na tuwape nafasi ili watuchunge vema.
Pamoja
na wajibu wetu wa kuwaombea, kadiri ya hati hii sisi waamini tunao wajibu wa kijamii
kwa mapadre wetu, yaani kuwasaidia katika mahitaji yao ya maisha. Kuwakimu katika
maisha yao. Huwa inakuwa aibu sana mapadre wetu wanapoonekana kuchoka na kuchakaa
na kuhangaika kwa maisha duni na ya tabu, yenye damu tupu na vidonda, wakati waamini
tupo, tunasitawi vizuri katika majumba ya kifahari, tunakula na kunywa huku mapadre
wetu wapiga miayo ya kukata tamaa.
Hapa mwito unatolewa kwa waamini wote kujiuliza:
tunawatunzaje mapadre wetu? Familia zetu zinachangia nini kwa maisha ya mapadre wetu?
Katika umoja wetu sisi kama Parokia, hatushindwi kuwatunza mapadre wetu. Kuwajengea
nyumba nzuri ya kisasa ya kuishi, kuhakikisha wanakula vizuri, wanavaa vizuri hadi
Altareni, wanalala mahali pazuri na zaidi kuwahakikishia matunzo mazuri ya afya kwa
kuwaandalia bima za afya, na mwisho kujitahidi kuwawekea akiba ya uzeeni.
Yaani
mapadre wetu katika uzee wanatia huruma mno kwa jinsi tunavyowatelekeza katika umasikini
na upweke mkuu. Kuna aina fulani ya kumwachia Askofu wajibu wote wa kuwatunza mapadre
waliopo kazini na wazee. Na hiyo hali duni ya mapadre wawapo kazini na uzeeni ni moja
ya sababu-mlenda zinazochangia kuzorotesha miito.
Sote tuamke kabisa, tujitathimini
na tuchukue wajibu wa kuwasaidia Mapadre wetu kwa mfumo sahihi unaojumuisha waamini
wote katika Parokia. Namna mojawapo ya kumshukuru Mungu kwa zawadi ya mapadre katika
Kanisa ni kuwatunza. Sisi waamini tunaamini kwamba tunaweza kabisa ila hatujaamua
kuanza kutekeleza kikamilifu wajibu huu.
Endapo Padre wa parokia yetu ataonekana
amekondakonda kwa njaa, ni aibu yetu sisi waamini wake, tena aibu kubwa sana! Tukivitunza
vyema vyombo hivi vya Mungu, Mungu naye atatubariki zaidi. Tusisahau kuwapelekea mapadre
wetu zawadi ya Heri ya Noeli na Mwaka Mpya; kabla ya kupeleka zawadi hakikisha umefuata
sheria, kanuni na taratibu za kodi, vinginevyo unaweza kusababisha majanga! Nami
nikikutakia heri tele na baraka tele kwa sherehe za Noeli na Mwaka Mpya 2015 Kutoka
katika Studio za Radio Vatican, ni mimi Padre Pambo Martini Mkorwe, OSB.