Askofu mkuu Dieudonnè Nzapalainga wa Jimbo kuu la Bangui ambaye pia ni Rais wa Baraza
la Maaskofu katoliki Jamhuri ya Watu wa Afrika ya Kati anasema, wananchi wamechoka
na vita, kinzani na misigano ya kijamii, wanataka kuona tena: haki, amani, upendo
na mshikamano wa kitaifa vinatawala sanjari na kudumisha utawala wa sheria, ili kulinda
usalama wa raia na mali zao.
Wasi wasi bado umetanda kiasi cha kudhohofisha
mchakato wa utoaji wa huduma na uzalishaji mali. Watu wanapaswa kubadilika na kuachana
na maovu tayari kuanza ukurasa mpya wa maisha, kwa kujikita katika misingi ya haki,
amani, msamaha na upatanisho wa kweli. Badala ya kuendelea kuendekeza kinzani na migogoro
ya kidini, watu wajiimarishe katika kukuza umoja, udugu na mshikamano, kwa kuheshimiana
na kuthaminiana hata katika tofauti zao.
Vijana ni kundi ambalo linatumiwa
na wanasiasa waliofilisika kwa mafao yao binafsi, changamoto kwa Kanisa kuanzisha
mbinu mkakati wa shughuli za kichungaji utakaoliwezesha Kanisa kuwasikiliza vijana
kwa makini na kuwasaidia kwa hali na mali katika majiundo yao awali na endelevu, kwa
kuwajengea dhamiri nyofu inayowawajibisha mbele ya Mungu na Jamii inayowazunguka.
Vijana wengi wanatafuta furaha ya kweli katika maisha, wakisaidiwa kwa njia
ya tunu msingi za Kiinjili, wanaweza kuwa watu wema na watakatifu. Vijana wafundwe
kuwa ni vyombo vya haki, amani na upatanisho; mambo msingi yanayopewa kipaumbele cha
kwanza na Mama Kanisa wakati huu wa Kipindi cha Noeli.
Askofu mkuu Nzapalainga
anasema, Jumuiya ya Kimataifa bado ina dhamana kubwa ya kuwasaidia wananchi wa Afrika
ya Kati ili kukabiliana na changamoto zilizopo kwa sasa, ili nchi yao isigeuzwe kuwa
ni pango la wevi, mafisadi na wanyang'anyi. Lakini wananchi wanakumbushwa kwamba,
amani kimsingi ni wajibu wa wananchi wa Afrika ya Kati na kwamba, Jumuiya ya Kimataifa
inachangia pale ambapo wananchi wenyewe wameonesha nia ya kuanza ukurasa mpya, vinginevyo
ni sawa na kumpigia mbuzi, gitaa!