Dumisheni misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa kitaifa! Matusi hayana tija!
Askofu Evaristo Chengula wa Jimbo Katoliki Mbeya, Tanzania, amewaasa wanasiasa nchini
Tanzania kuacha dhana potofu ya kukiuka maadili mema kwa kutoa lugha za matusi majukwaani
wakiamini kuwa ndiyo mwanasiasa bora katika jamii,jambo ambalo siyo kweli bali ni
kukengeuka na kupotoka kimaadili. Ni wajibu wa vyama vya kisiasa kuhakikisha kwamba,
vinajitahidi kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani, utulivu na mshikamano wa
kitaifa, kwa ajili ya mafao ya watanzani wote, bila kuwakatisha watu tamaa kwa vurugu
na kinzani zisizokuwa na mvuto wala mashiko!
Askofu Chengula aliyasema hayo
wakati wa ibada ya mkesha wa Sikukuu ya Noeli, tarehe 24 Desemba 2014 uliofanyika
katika Kanisa kuu la Mtakatifu Anthony wa Padua, Parokia ya Mbeya mjini. Anasema viongozi
wa Serikali na vyama vya siasa, wanatakiwa kuwaletea matumaini watanzania na kuwa
kiongozi anayetukana wenzake katika majukwaa ya kisiasa, ni wazi kuwa hata naye akipata
madaraka makubwa basi ataendelea kuwa hivyo, jambo ambalo siyo sahihi.
"Viongozi
wetu wanatakiwa wamjue Yesu Kristo, ili wawe na roho ya kuleta matumaini kwa watanzania
wote kwa kuhakikisha wanavunja utengano wa ukabila, udini, udugu ama eneo analotoka
mtu ili watanzania wote waweze na furaha, upendo na mshikamano, kwa kusaidiana wakati
war aha na shidaā€¯ anasema Askofu Chengula. Aliongeza kwa kuwataka watanzania kutimiza
wajibu wao barabara kwa kuanzia katika ngazi ya mtu binafsi, familia na jamii kwa
ujumla, ili kujenga na kuimarisha utamaduni wa haki, amani, upendo na mshikamano wa
dhati, hasa wakati huu watu wanapojikuta wakimezwa mno na utandawazi unaogubikwa katika
ubinafsi.
Askofu Chengula akiangalisha kwenye uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika
nchini Tanzania mwaka 2015, ameitaka Serikali kuangalia mfumo wa kuandikisha watu
katika Daftari la kudumu la wapiga kura kwa kulifanyia maboresho zaidi, kwa kutoa
muda wa kutosha, ili watanzania wenye sifa za kupiga na kupigiwa kura waweze kutumia
vyema haki yao Kikatiba kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya taifa. Muda ukiwa finyu,
watu wengi watajikuta wanashindwa kujiandikisha na hivyo kupoteza haki yao ya kushiriki
katika demokrasia. Kasoro zilizojitokeza katika zoezi la kuandikisha wananchi katika
Daftari la wapiga kura zifanyiwe maboresho zaidi, ili hata kura ya maoni kuhusu muswada
wa Katiba Mpya inayopendekezwa, iweze kuwashirikisha watanzania wengi zaidi.
"Tunawaomba
viongozi wetu watutengenezee njia ili kuufanya uchaguzi mkuu mwakani (2015), uweze
kwenda vizuri zaidi" alisema Askofu Chengula. Alisema kabla ya kuzaliwa kwa Yesu
Kristo zaidi ya miaka 2000 iliyopita, watu walitembea katika giza kuu na walikaa katika
ulimwengu wa kuonewa na kumwaga damu, lakini sasa wameona mwanga mkuu, changamoto
na mwaliko kwa waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuwa kweli ni wajenzi wa misingi
ya haki, amani, upendo na mshikamano kati ya watu.
Bado kuna vita, nyanyaso
na madhulumu katika misingi ya kidini, mambo yanayowafanya baadhi ya watu kukosa haki
yao ya kuwa na uhuru wa kuabudu. Hii ni changamoto kubwa kwa Serikali kuhakikisha
kwamba, inazingatia utawala wa sheria na Katiba inatekelezwa kwa ajili ya mafao ya
wengi. Chokochoko za kidini ni hatari kwa ustawi na maendeleo ya watu.
Yesu
Kristo aliyezaliwa mjini Bethlehemu ni Mfalme wa haki na amani anayekuja kulifukuza
giza katika maisha ya mwanadamu, changamoto na mwaliko kwa waamini na watu wote wenye
mapenzi mema, kuhakikisha kwamba, wanaruhusu mwanga wa Kristo uweze kuwaangazia ili
watembee katika upya wa maisha kwa kuachana na maisha ya kale yanayojikita katika
dhambi na mauti! Noeli kiwe ni kipindi cha haki, amani, upendo na mshikamano, kwa
kuwajali maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii! Na Thomposn Mpanji, Mbeya,
Tanzania.