2014-12-26 11:18:17

Jengeni umoja na mshikamano unaojikita katika uwajibikaji; utu na heshima ya binadamu!


Mfalme Abdullah wa Pili wa Yordan, katika Maadhimisho ya Siku kuu ya Noeli, amewatumia salam na matashi mema Wakristo wote nchini mwake na kuwatakia kheri na fanaka kwa Mwaka Mpya wa 2015. Katika salam zake, Mfalme Abdullah wa Pili anawataka waamini na wananchi wote kwa ujumla kushikamana ili kujenga na kuimarisha umoja wa kitaifa; kuendeleza uzalendo unaofumbatwa katika uwajibikaji na mshikamano wa kijumuiya!

Kuna mabadiliko makubwa yanayoendelea kutokea katika ulimwengu wa utandawazi, baadhi ya mabadiliko haya yanaonesha ustawi na maendeleo kwa binadamu, lakini baadhi yake yanatia shaka na wasi wasi mkubwa kuhusu hatima na mustakabali wa maisha ya mwanadamu kwa siku za usoni. Kuna haja kwa Jumuiya ya Kimataifa kuendeleza majadiliano ya kidini na kiekumene, ili kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani na utulivu, kwa kuthamini hata tofauti zinazojitokeza kati ya watu.

Viongozi wa kidini nchini Yordan wanaendelea kukazia umuhimu wa wananchi kushikamana na kusaidiana ili kudumisha umoja wa kitaifa, pamoja na kuendelea kuwa ni nchi ya mfano kwa Waislam na Wakristo kuishi kwa amani na utulivu, licha ya tofauti zao za kidini na kiimani. Yordan imekuwa ni bandari ya salama na matumaini kwa watu wanaokimbia vita, nyanyaso na madhulumu ya kidini huko Mashariki ya Kati.

Wakimbizi na wahamiaji wanalipongeza Shirika la Misaada la Kanisa Katoliki, Caritas Yordan kwa kuwahudumia wakimbizi na wahamiaji kwa upendo na uvumilivu mkubwa, kiasi kwamba, watu wamefanikiwa kupata makazi, chakula na mahali salama zaidi kwa familia zao!







All the contents on this site are copyrighted ©.