2014-12-25 11:05:06

Ugonjwa wa Ebola umepelekea tena baa la njaa!


Shirika la Kilimo na Chakula la Umoja wa Mataifa, FAO linasema kwamba, ugonjwa wa Ebola unaendelea kutishia usalama wa maisha ya wananchi wengi Afrika Magharibi na kwamba, kuna watu zaidi ya millioni moja wanaotishwa na baa la njaa kutokana na janga lililosababishwa na ugonjwa huu.

Hii inatokana na baadhi ya nchi jirani kuamua kufunga mipaka ya nchi zao kwa kuhofia maambukizi ya ugonjwa wa Ebola kutoka katika maeneo yaliyoathirika zaidi, hali ambayo imepelekea pia myumbo wa uchumi katika nchi kadhaa huko Afrika Magharibi. FAO na Mpango cha Chakula wa Umoja wa Mataifa, unaitaka Jumuiya ya Kimataifa kuunganisha nguvu, ili kuokoa maisha ya maelfu ya watu huko Afrika Magharibi, wanaokabiliwa na baa la njaa!

Baraza la Maaskofu Katoliki Sierra Leone, linawaomba waamini pamoja na wasamaria wema kuguswa na mahangaiko ya wananchi walioathirika kutokana na ugonjwa wa Ebola kwa kuchangia kwa hali na mali, ili kusaidia huduma zinazotolewa na Kanisa kwa waathirika wa janga la Ebola. Vituo vya afya vinavyomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa Katoliki nchini Sierra Leone kwa sasa vinahitaji msaada mkubwa, ili kuviwezesha kutekeleza utume wake, vinginevyo, hali itakuwa ni mbaya zaidi, si tu kwa sababu ya ugonjwa wa Ebola, bali kwa kutambua kwamba, hata magonjwa mengine nyemelezi yanaendelea kushika kasi kutokana na hofu ya kuambukizwa ugonjwa wa Ebola.

Ebola ni ugonjwa ambao kwa sasa unatishia mshikamano na mfungamano wa kimataifa!









All the contents on this site are copyrighted ©.