Leo ni siku ya furaha. Tunapokutana tunatakiana “Merry Christmas” na kupeana zawadi.
Nami zaidi ya kukutakia heri ya christmas, ninapenda pia kukupatia zawadi ya Krismasi.
Lakini naomba nikutonye kabla, kwamba zawadi hiyo ni siri. Ingawaje waswahili wanasema
“hakuna siri ya watu wawili,” ninakutahadharisha kuwa, pale utakapowalopokea pengine
hawatakuamini au wanaweza wakakuelewa vibaya.
Siri yenyewe ni kwamba “Umebahatika
sana kuwa na imani,” tena “imani kwa nafsi iliyo hai, ambayo ni Kristo mwenyewe Mwana
wa Mungu aliye hai.” Nafsi hiyo siyo ukweli wa kufikirika ulioandikwa kwenye msaafu,
bali ni nafsi halisi, iliyo uzima na ni mwongozo unaokupeleka kwenye utimilifu wa
maisha ya furaha kwanza, ya hapahapa duniani, halafu furaha ya mbinguni. Waswahili
wanasema: “Bahati ina miujiza, lakini haina ahadi.” Nafsi hiyo iliyo halisi, uzima
na mwongozo unaiona katika sikukuu ya leo.
Muujiza mmojawapo ni kule kuwezeshwa
kuelewa mambo ambayo wasio na imani hiyo hawawezi kamwe kuyaelewa. Wewe umebahatika
kujua maana ya mambo yatokeayo na kuweza tafsiri ya matendo ya kawaida ya maisha wanayofanya
watu. Hakika unaweza kusoma ishara za nyakati na kutambua maana ya matendo yafanyikayo
katika ulimwengu wa kisiasa, ulimwengu wa dini, wa mambo ya familia na hata kuyatafsiri
matatizo yako binafsi.
Nitakupa mfano unaohusu sikukuu ya leo. Unashuhudia
mwenyewe jinsi watu walivyohamasika kuandaa na kusherekea krismas. Wanavyokula mapochopocho,
wanatia viwalo vya pekee na kufurahi sana. Mataifa mengine kama vile Wajerumani wa
kusini leo wanakula keki maalumu ya Noeli inayoitwa Lebkuchen, na keki ya waitalia
inaitwa panettone. Kadhalika leo kuna kuvaa nguo za pekee za sikukuu. Watu wote tunavifurahia
vyakula na viwalo hivyo, lakini ni bahati ya walio na imani kwa Kristu tu ndiyo wanaofahamu
kwa nini wanafanya hivyo. Wengine wote ni ushabiki tu wa kula na kunywa basi, na pengine
sanasana wanajua sikukuu hizi ni za kufanya vizuri biashara zao.
Mfano
mwingine, ulitokea miaka kumi na nne iliyopita, pale jinsi watu walivyoisubiri na
kuishangilia Millenia mpya ya tatu. Ingawaje wote tuliona fahari kuwaona watu wote
dunia wakiisherekea miaka hiyo, lakini kwako wewe mkristu hukufurahia tu kule kubadilika
kwa tarehe na kuwa miaka 2000, bali sikukuu hiyo kwako ilieleweka vizuri zaidi, kwamba
ulikuwa ni ukumbusho wa mwanzo wa historia mpya na ya pekee ya dunia, miaka elfu mbili
toka kuzaliwa Kristo.
Utaigundua zaidi bahati uliyo nayo, pale utakapokutana
na mtu asiye na imani anapokabiliwa na matatizo mazito ya maisha anavyohaha na kukata
tamaa. Alama ya kukata tamaa unaiona jinsi anavyoyakabili matatizo yake, akitumia
nguvu na kudhulumu asijue anaongeza tatizo juu ya tatizo. Mtu huyo ameikosa nafsi
hai ya kuilalamikia na ya kujadiliana nayo matatizo yake.
Kumbe, wewe
umebahatika kuwa na nafsi hai ambayo ni Kristu aliyezaliwa, aliyekua, aliyeteswa na
kuuawa lakini akafufuka. Hivi kudhulumiwa kwake, mateso na kifo chake vyote vinapata
mwanya au nafasi ya kuwa na amani na upendo, hatimaye ni kuwa na furaha katika mateso.
Unaona bahati uliyo nayo, kwamba katika matatizo, katika madhulumu na kuonewa, wewe
unabaki kuwa na furaha, amani na upendo.
Ndugu yangu, binadamu wa leo siyo
kwamba hana imani, la hasha, anayo imani, tena imani kubwa sana. Watu wengine wanayo
imani kubwa kukushinda wewe unayejidhani unayo imani ya msimamo mkali wa dini yako.
Angalia wenzako walivyo na imani kwa matangazo ya biashara, matangazo ya vipodozi
vya urembo, matangazo ya dawa za kuongeza ukubwa wa maumbile, kuna imani juu ya chama
cha siasa na sera zake hata kama zinatuongoza porini au zinazamisha jahazi. Kuna watu
wana imani kubwa sana kwa maagizo ya mganga wa kienyeji hata wakikuagiza kuua.
Tofauti
iliyopo kati ya imani zao na yako ni kwamba, imani ya mkristu imejengwa katika Mungu
aliye nasi “Emmanuel”. Huyo ni Mungu aliye hai, Mungu mwema na mwenye haki, Baba wa
Bwana wetu Yesu Kristu. Kama alivyopenda kusema Paulo mtume: “Utaonanana naye huyo
Mungu unapoonana na Yesu wa Nazareti.” Hakuna aliyemwona Baba ila Mwana… na yule ambaye
Mwana apenda kumfunulia.” (Mt. 11:27).
Tofauti nyingine ni kwamba wewe
uliye na imani kwa nafsi hai ya Kristu, unakuwa huru. Hakuna kitakachokutisha, hakuna
kutishwa na masherti ya mganga, wala mateso, wala kifo. “Mkishika neno langu katika
neno langu, ninyi ni wanafunzi wangu; mtauelewa ukweli, nao ukweli utawaweka huru”
(Yo. 8:31-32). Kwa hiyo “Pale alipo Roho wa Bwana, hapo pana uhuru” (2Kor. 3:17).
Tofauti
nyingine ni kwamba wewe umebahatika kujua maana ya sherehe ya leo kuwa sikukuu hii
siyo ukumbuko, bali ni sherehe za utimilifu wa unabii. Unabii uliokuwa ni sauti ya
maandamano ya mgomo dhidi ya mambo ya ulimwengu huu, dhidi ya kuonewa, dhidi ya ubabe.
Ubabe huo unadokezwa mwanzoni tu mwa Injili ya usiku wa Noeli lilipopitishwa tangazo
la kiubabe: “Kukatokea tangazo toka kwa Kaisari Augusto la kuhesabu watu wote duniani.”
Kuhesabu watu maana yake watu walio nafsi hai, wanashushwa hadhi hadi kufikia kiwango
cha kuwa bidhaa inayoweza kuhesabiwa. Binadamu hujulikani kwa jina bali kwa nambari,
hiyo ndiyo senza.
Wakati huo watu wanapodhalilishwa hivyo ndipo mtoto
anazaliwa. HapoMungu anaianzisha historia mpya Betlehemu, pahala palipokuwa pa mwisho
kabisa duniani, tena anazaliwa kizizini na anajionesha kwa wachungaji watu wanyonge
wa mwisho, na anakubali kuzaliwa na kulelewa na binti mdogo na mnyonge Maria.
Ndugu
yangu, ni wewe peke yako unaposherekea Noeli hii ndiye unayeweza kujua mtoto huyu
ataishije na ataishia wapi. Ukiijua siri hiyo utaweza pia kutambua sherehe za leo
zinataka kutufundisha nini katika maisha yetu. Aidha, utaelewa pia maana ya kusherekea
hata sikukuu ya kuzaliwa kwako na maisha yako yalivyo na hatima yake. Siri niliyokupa
unaweza kuigundua vizuri zaidi kuwa ni siri iliyo wazi pale utakapouangalia uso wa
mama baada tu ya kujifungua mtoto wake.
Furaha aliyo nayo baada ya uchungu
mkuu wa kujifungua, hiyo inakuwa ni siri yake mwenyewe. Nadhani hata malaika walipoyaangalia
macho ya Maria baada ya kujifungua mtoto Yesu hawakuelewa kitu. Pengine hata Maria
mwenyewe ingawa alifurahi lakini hakuelewa sana maana ya uzao ule, hasa tunaposikia
kwamba “akayaweka yote moyoni mwake, akiyatafakari.” Ila kwa uhakika maana halisi
ya noeli alikuja kuifahamu alipokuwa chini ya msalaba. Nawe utatambua zaidi maana
ya Noeli yatakapokupata. Naomba unitunzie siri, na Heri sana kwa sikukuu ya Noeli.