2014-12-25 08:12:40

Mwanga angavu wa Mtoto Yesu uvunjilie mbali giza katika mioyo ya watu!


Watu wale waliokwenda katika giza wameona nuru kuu; wale waliokaa katika nchi ya uvuli wa mauti, nuru imewaangazia. Malaika wa Bwana akawatokea ghafla, utukufu wa Bwana ukawang’aria pande zote. RealAudioMP3

Hivi ndivyo Liturujia ya Neno la Mungu inavyosikika wakati wa kesha la Siku kuu ya Noeli, yaani kuzaliwa kwa Mkombozi, asili ya mwanga unaopenya na kuondoa giza. Uwepo wa Yesu Kristo miongoni mwa watu wake unaondoa uzito wa kushindwa na huzuni ya utumwa na hivyo kuwakirimia tena watu furaha.

Hivi ndivyo Baba Mtakatifu Francisko alivyosema wakati wa mahubiri yake, kwenye Ibada ya Misa Takatifu, Kesha la Noeli, iliyofanyika kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican. Anasema, hata waamini wakati wa mkesha huu wamekuja Nyumbani kwa Bwana kwa kupitia kwenye giza linaloifunika dunia, lakini kwa kuongozwa na mwanga wa imani unaoangazia mapito yao, wakiwa wamejazwa na matumaini ya kukutana na mwanga mkuu. Kwa waamini kufungua mioyo yao, wanauwezekano wa kutafakari muujiza wa Mtoto mwenye nuru inayoangaza mawio kutoka juu.

Baba Mtakatifu anasema, giza limeendelea kumwandama mwanadamu katika historia ya maisha yake tangu siku ile Kaini alipomwaga damu ya ndugu yake Abeli kutokana na wivu usiokuwa na mashiko, mauaji, vita, chuki, uhasama na kinzani zimeendelea kusikika katika uso wa dunia. Lakini kwa subira na unyenyekevu mkuu, Mwenyezi Mungu ameendelea kumsubiri kwa uaminifu na uvumilivu mkuu mwanadamu aliyemuumba kwa sura na mfano wake, licha ya mwanadamu kukengeuka.

Katika historia, mwanga unaofukuza giza umeonesha kwamba, Mwenyezi Mungu ni Baba mwenye uvumilivu unaojikita katika uaminifu kiasi cha kushinda giza na uasi wa mwanadamu, kiini cha Habari Njema katika kesha la Noeli. Mwenyezi Mungu ni mwingi wa huruma na uvumilivu, anayevuta subira, kama ilivyokuwa kwa Baba mwenyehuruma, alipokuwa anamngojea Mwana mpotevu, ili aweze kurejea tena nyumbani.

Baba Mtakatifu anasema, Nabii Isaya anatabiri kwamba, Mwanga angavu utavunja giza na Mtoto Yesu anazaliwa na kupokelewa kwenye mikono pendelevu ya Bikira Maria na upendo kutoka kwa Mtakatifu Yosefu pamoja na mshangao wa wachungaji kutoka kondeni. Ni mtoto aliyelazwa kwenye pango la kulishia wanyama, kielelezo cha hali ya juu kabisa cha upendo na unyenyekevu wa Mwenyezi Mungu, aliyejitwalia unyonge, mateso, mahangaiko, matarajio na mipaka ya mwanadamu. Mwanadamu kutoka katika undani wa maisha yake, alikuwa anatafuta faraja ya Mungu anayemwangalia kwa jicho pendelevu, anayekubali mapungufu ya mwanadamu na kuridhika na udogo wake.

Baba Mtakatifu Francisko anawaalika waamini katika mkesha wa Noeli, kujiuliza ikiwa kama kweli, wamefanikiwa kuipokea huruma ya Mungu, kwa kumwachia nafasi, ili aweze kuwafikia au wamekuwa ni kikwazo? Lakini jambo la msingi kwa waamini kumwachia nafasi Mwenyezi Mungu ili aweze kumtafuta ili aweze kumbembeleza kwa upendo pamoja na kujiuliza swali la msingi, ikiwa kama kweli waamini wanampenda Mwenyezi Mungu.

Baba Mtakatifu Francisko anaendelea kuwahoji waamini, ikiwa kama bado wana ujasiri wa kupokea kwa wema magumu na mateso yanayowazunguka katika maisha au pengine wameamua kuchukua njia ya mkato, isiyofumbata tunu msingi za Kiinjili? Baba Mtakatifu anasema, dunia hii inahitaji huruma ya Mungu. Changamoto za maisha hazina budi kukabiliwa kwa njia ya wema na upole, kwa kutambua kwamba, Mwenyezi Mungu amejinyenyekesha na kujifanya kuwa mdogo, ili aweze kukutana vyema zaidi na binadamu.

Huu ni mwaliko wa kumfungulia mioyo yao, kwa kumwomba ili aweze kuwasaidia kuwa kama alivyo, awajalie neema ya upole wanapokabiliana na changamoto pamoja na magumu katika maisha; awajalie kuonja ukarimu wakati wa shida na uvumilivu wakati wa kinzani.

Baba Mtaakatifu Francisko anahitimisha mahubiri yake kwa kusema kwamba, waamini katika kesha la Siku kuu ya Noeli, wanatafakari mwanga angavu, ulioonekana na watu wa kawaida kabisa, wale ambao walikuwa wamejiandaa kwa ajili ya kupokea zawadi ya Mungu. Tofauti kabisa na watu waliokuwa na kiburi pamoja na majivuno; wale wanaotunga sheria kwa ajili ya mafao yao binafsi; watu wanaojifungia katika ubinafsi wao. Waamini wanapoangalia Pango la Mtoto Yesu, wamwombe Bikira Maria ili awawezeshe kumwona Mtoto Yesu!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.