Ombeni hekima ya majadiliano, furaha na matumaini!
Baraza la Maaskofu Katoliki Argentina, katika ujumbe wake kwa Maadhimisho ya Siku
kuu ya Noeli linawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kutambua kwamba,
wanapendwa na kuthaminiwa na Mwenyezi Mungu na kwamba, hii iwe ni changamoto kwao
kutangaza na kudumisha amani ambayo kimsingi ni zawadi kubwa inayotolewa na Mwenyezi
Mungu katika Siku kuu ya Noeli.
Ujumbe wa
Malaika usikike tena mioyoni mwa watu “Amani duniani kwa watu wenye mapenzi mema”.
Maaskofu wa Argentina wanasema, Noeli ni kielelezo cha ukubali wa Mwenyezi Mungu kuendelea
kumsindikiza mwanadamu katika hija ya maisha yake hapa duniani, ili kujenga na kuimarisha
ulimwengu ambamo haki, amani, upendo na mshikamano vinaweza kutawala tena katika mioyo
ya watu.
Noeli ni kipindi cha kuimarisha umoja na udugu; msamaha na upendo;
uhuru na kiasi, kwa wazazi kusameheana na watoto wao na watoto pia kuthubutu kuomba
msamaha pale walipowakosea wazazi wao, tayari kuanza upya na kutembea katika mwanga
wa Kristo, Mfalme wa Amani. Noeli ni siku kuu ya mshikamano na upendo kwa maskini
na wale wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii.
Maaskofu wanawataka waamini
pamoja na watu wote wenye mapenzi mema, kuhakikisha kwamba, wanatoa kipaumbele cha
kwanza katika kukuza na kudumisha misingi ya haki na amani mioyoni mwao, sehemu ambayo
imeathirika kutokana na dhambi ya asili. Myumbo wa uchumi kimataifa inaendelea kusababisha
majanga makubwa katika maisha ya watu, kiasi kwamba, watu wanakumbatia utamaduni wa
kifo kwa kutema Injili ya Uhai, haki msingi kwa kila binadamu.
Biashara haramu
ya dawa za kulevya inaendelea kushamiri na kusababisha majanga kwa vijana na familia
nyingi; bila kusahau biashara haramu ya binadamu; mambo yanayodhalilisha utu na heshima
ya binadamu; huu ni uhalifu dhidi ya ubinadamu. Kumeibuka watu wenye misimamo mikali
ya kidini na kiimani wanaosababisha vifo, mateso na mahangaiko kwa watu wasiokuwa
na hatia.
Lakini ikumbukwe kwamba, chuki na uhasama ni giza linalofunga mlango
wa majadiliano na upatanisho kati ya watu. Rushwa na ufisadi wa mali ya umma ni majanga
ya kitaifa yanayohitaji toba na wongofu wa ndani kwa kujikita katika uadilifu, ukweli
na uwazi, bila kukumbatia uchu wa mali, ubinafsi na uchoyo. Waamini na watu wenye
mapenzi mema, wajitahidi kujenga na kuimarisha mshikamano wa upendo na udugu, kwa
kutafuta mafao ya wengi; utu na heshima ya binadamu.
Baraza la Maaskofu Katoliki
Argentina linahitimisha ujumbe wake kwa Siku kuu ya Noeli kwa kuwataka waamini kumwomba
Mwenyezi Mungu busara na hekima katika majadiliano; furaha na matumaini yasiyodanganya
kamwe!
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio
Vatican.