Qatar kuwekeza katika kilimo, gesi, mafuta na ajira nchini Tanzania
Waziri Mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda amesema Watanzania watanufaika na kipato na
maarifa ya teknolojia ya kisasa kutokana na ajira ambazo watapata katika nchi ya Qatar
baada ya mkataba kusainiwa hivi karibuni. Ametoa kauli hiyo Jumapili, Desemba 20,
2014, jijini Doha, Qatar wakati akizumgumza na waandishi wa habari ili kuwapa taarifa
fupi juu ya mambo yaliyojiri kwenye mazungumzo yake na Waziri Mkuu wa Qatar, Sheikh
Abdulla Nasser Al Thani.
Katika mazungumzo hayo ambayo yalifanyika ofisini
kwa Sheikh Abdulla, Waziri Mkuu Pinda amesema wamekubaliana kutoa ajira kwa Watanzania
kwa sababu nchi hii inahitaji wafanyakazi wengi kwenye sekta mbalimbali na raia wake
ni wachache. “Hivi sasa wapo Watanzania wanaofanya kazi hapa lakini ni wachache mno.
Mazungumzo yalishaanza siku za nyuma. Tukisaini mkataba katika muda mfupi ujao, tutajua
ni idadi gani wanahitajika na wanaweza kuja kila baada ya muda gani,” alifafanua Waziri
Mkuu.
“Hapa Qatar kuna uwekezaji mkubwa umefanyika, kwa hiyo wanahitaji watu
wa kufanya kazi... kwenye mahoteli, viwandani, na kikubwa hapa ninachokiona watu wetu
watapata kipato lakini pia watapata ujuzi kwa maana ya maarifa yanayoendana teknolojia
ya kisasa,” aliongeza.
Akeleza mambo mengine ambayo wamekubalina kushirkiana
kama nchi rafiki, Waziri Mkuu alisema kuna mambo makuu manne likiwemo hilo la ajira.
“La kwanza ni Kilimo. Hapa Qatar ni jangwa kila mahali. Wamekubali kuja kuwekeza kwenye
kilimo, ufugaji na uvuvi kwa sababu sisi tuko karibu nao zaidi kuliko Marekani au
Brazil.” “Wanaweza kupata mchele, matunda, nyama kwa maana ya machinjio na viwanda
vya kusindika nyama lakini pia katika uvuvi wa samaki. Tunayo bahari ila mitaji yetu
ni midogo. Kwa hiyo wamekubali kuangalia eneo hilo pia,” alisema.
Alisema eneo
la pili ni la gesi na mafuta. “Wamekubali kutusaidia utalam ili tushirikiane nao katika
namna kutumia gesi kwenye ngazi ya chini hasa viwanda kwa sababu wenzetu wana uzoefu
wa muda mrefu. Hata kwenye mafuta wameonyesha kuwa wako tayari,” alisema.
Eneo
la tatu alilitaja kuwa ni kutoa fursa ya ajira kwa Watanzania na la nne ni TEHAMA.
“Hawa wenzetu wamechanganya TEHAMA na sayansi na sasa wana Jiji la Sayansi na Teknolojia.
Chini ya makubaliano tutakayofikia, watu wetu watakuja kujifunza masuala ya gesi na
mafuta.”
Alisema wamekubaliana na Sheikh Abdulla al Thani kuunda timu ya pamoja
baina ya nchi zao ili ifanye kazi ya kuainisha ni maeneo gani wanataka waanze nayo
kwanza kulingana na mahitaji. “Nimemuahidi nikifika nyumbani nitaandika barua ili
mchakato wa kuunda timu uanze rasmi,” alisema.
Jumapili mchana, Waziri Mkuu
Pinda atakuwa na mazungumzo ya Kiserikali na Mawaziri wa Kazi na Ustawi wa Jamii;
Uchukuzi; Miundombinu na Uwekezaji wa Qatar. Naibu Mawaziri atakaokutana nao ni wa
Uchumi na wa Nishati.