Watanzania wanaoishi nchini Qatar wameiomba Serikali iangalie uwezekano wa kufungua
ofisi ya ubalozi nchini humo ili iwe rahisi kwao kufikisha matatizo yao na pia wawe
na uhakika wa masuala yao kushughulikiwa kikamilifu. Wametoa ombi hilo kwa nyakati
tofautiJumapiliusiku Desemba 20, 2014 wakati wakitoa hoja na matatizo yao mbele ya
Waziri Mkuu Mizengo Pinda ambaye yuko nchini Qatar kwa ziara ya kiserikali ya siku
tatu.
Akizungumza kwa niaba ya Watanzania waishio Qatar katika mkutano uliofanyika
kwenye hoteli ya Sheraton jijini Doha, Mwenyekiti wa Umoja wa Watanzania wanaoishi
Qatar, Bw. Said Ahmed Said alisema ubalozi wanaoutegemea kwa sasa hivi uko Saudi Arabia
ambako ni mbali na kwamba inakuwa vigumu kuwasilisha shida zote zinazowakabili Watanzania.
“Kwa
mfano kuna suala la fursa za watoto wetu kusomeshwa elimu ya juu na kulipiwa na Serikali
ya hapa. Inakuwa vigumu kupata hiyo fursa kwa sababu hakuna mtu wa kutusemea,”alisema
Bw. Said na kushangiliwa na wenzake. “Watoto wetu waliozaliwa hapa wakimaliza sekondari
hawawezi kwenda Chuo Kikuu chochote kwa sababu mfumo wa hapa hauwaruhusu.
Hata
wale tuliowaacha nyumbani huwezi kuwaleta wakasomea hapa kwa sababu ya huo mfumo.
Lakini wenzetu kutoka nchi nyingine wanapata hizo fursa kwa sababu wana quota yao.
Tunaamini tukiwa na ubalozi hapa nchini, tutaweza kupata fursa kama wenzetu,” alisema.
Watanzania
wengine waliochangia hoja ya kuwa na ofisi ni Bw. Abdallah Sima Abdalla (kutoka Zanzibar),
Bw. Hersi Mohammed Adam (kutoka Singida) na Bw. Iddi Ali Ameir ambaye pia anatoka
Zanzibar. Hata hivyo, Bw. Hersi Mohammed Adam ambaye amefanya kazi kwenye kampuni
ya uchimbaji mafuta ya Al Mazrui Oil Industries kwa miaka tisa, alisema kuna haja
ya kuwaleta Watanzania wengi wajifunze kazi ndogondogo zinazohusu uchimbaji mafuta
kwani wana fursa ya kufundishwa wakiwa kazini. “Kuna kazi ambazo hazihitaji vyeti
vya juu sana kama kusafisha mabomba ya gesi lakini pia ni za muhimu na zitawasaidia
wengi kupata ajira wakati kazi kama hizo zikianza nchini Tanzania,” alisema.
Akizungumzia
suala la kuwa na ubalozi, Waziri Mkuu alisema wazo lao ni la msingi ikizingatiwa kwamba
kuna Watanzania zaidi ya 300 wanaoishi Qatar. “Hili suala ni la Serikali na mimi naona
jibu la msingi ni kuwa na ofisi ya ubalozi hapa Doha kwa sababu mko wengi na tuna
mahusiano ya karibu sana na wenzetu,” alisema na kuahidi kulifuatilia kwa sababu amekwishajadiliana
na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Dk. Mahadhi Maalim ambaye
yuko kwenye msafara wa Waziri Mkuu.
Akizungumzia suala la ajira, Waziri Mkuu
aliwahakikishia Watanzania hao kwamba, Serikali ya Qatar imesharidhia mkataba wa kuruhusu
raia wa Tanzania waje kufanya kazi Qatar. “Sisi tulianzisha huu mkataba na wenzetu
hawa wameuridhia mwezi uliopita... naamini utatusaidia sana kwenye suala la ajira
za watu wetu lakini itabidi tuangalie ninyi ambao mlikuwepo zamani kabla mkataba haujasainiwa
tunawafaya nini,” alisema.
Wakati huo huo, Waziri Mkuu Pinda alitoa nakala
zipatazo 30 za Katiba Inayopendekezwa kwa Watanzania waishio Qatar na kuwataka waisome
na kutoa mapendekezo yao hasa katika eneo la uraia pacha. “Hakikisheni mnaisoma na
kujadili kwa kina eneo hili na kisha mtupe majibu yenu kwa sababu suala hilo liliibua
mjadala mkubwa ndani ya Bunge Maalum la Katiba wakati likijadiliwa,” alisema.
Waziri
Mkuu amefuatana na Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Dk. Titus Kimani; Waziri
wa Kilimo na Maliasili wa Zanzibar, Dk. Sira Ubwa Mamboya; Naibu Waziri wa Mambo ya
Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Dk. Mahadhi Maalim; Naibu Waziri wa Nishati, Bw.
Charles Kitwanga; Naibu Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Bw. Godfrey Zambi.
Wengine ni Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Bw. Abbas Kandoro, Mkuu wa Mkoa wa Mtwara,
Bi. Halima Dendego, wabunge wawili Bi. Amina Makilagi na Bw. Aeshy Hilali, Dk. Gideon
Kaunda wa TPSF na Bw. Shigela Malocha kutoka TPDC.