Nafasi ya Bikira Maria katika historia ya ukombozi!
Katika maandalizi ya michezo kwa ajili ya kusherehekea sikukuu ya Noeli, mtoto Silvia
alipewa kucheza nafasi ya Mama Maria. Lakini kumbe moyoni mwake hakuwa amefurahishwa.
Kadiri maandalizi ya mchezo kwa ajili ya sherehe za Krismasi zilivyokaribia, mwalimu
wake aligundua shida fulani katika uso wa Silvia. Naye hakusita kumwuliza kulikoni.
Naye bila kusita akasema, ningependa zaidi kucheza nafasi ya malaika kuliko ya Maria.
Sijisikii kufanana na Maria Mama wa Mungu. Huyu mtoto aliona ni afadhali kushika na
kucheza nafasi ya malaika kuliko kucheza nafasi ya Maria Mama wa Mungu.
Leo
tunasikia sehemu ya maandiko matakatifu juu ya kupashwa habari Bikira Maria kuwa atakuwa
Mama wa Mungu. Kwamba atamzaa Yesu, yaani, mkombozi wa wanadamu.
Tunaendelea
na tafakari yetu ya majilio -kipindi cha kumbukumbu na matumaini. Tunakumbuka aliyofanya
Mungu na kutumainia ujio wake kama alivyoahidi. Katika Jumapili ya kwanza ya Kipindi
cha Majilio – Tulikumbushwa tuwe macho, tukeshe. Kipindi cha majilio ni katekesi fupi
ya ufahamau wa mpango wa Mungu wa ukombozi.
Bila kuamini tukio la kuzaliwa
Bwana itakuwa vigumu kuishi imani inayotokana na matukio ya mpango huo. Siyo rahisi
kuamini Yesu aliyepo bila kuutambua na kuukubali huo mpango mzima. Kwamba alizaliwa,
akaishi kati yetu, akateswa, akafa, akazikwa, akafufuka na kupaa mbinguni. Kuukataa
ukweli huu ni sawa na kusherekea kuzaliwa kwa mtu ambaye hajazaliwa. Itakuwa ni maigizo
tu bila ukweli wowote.
Katika Jumapili ya Pili ya Kipindi cha Majilio - Kila
mtu alialikwa aingie kucheza. Utamu wa ngoma ni kucheza, siyo kuangalia.. Mfano wa
mpiga muziki Paganini ambaye baada ya kucheza muziki kwa muda mrefu aling’amua baadaye
kuwa muziki unatoka moyoni na si kwenye chombo anachotumia kupiga muziki. Mfano wa
Yohana mbatizaji unajibu wasiwasi wetu - yeye aliingia kuicheza ngoma.
Katika
Jumapili ya tatu ya Kipindi cha Majilio – Yesu yuko wapi? Kumbe Yesu yuko kati yetu
- Yoh 1,26 – Yohane akawajibu akisema mimi nabatiza kwa maji katikati yenu amesimama
yeye msiyemjua ninyi. Yohani anaongea waziwazi juu ya uwepo wa Kristo kati yetu. Wajibu
wetu sisi wakristo ni kuendelea kumshuhudia huyo Kristo.
Katika Jumapili hii
ya nne ya kipindi cha Majilio – tunaona haja ya kuwa na unyenyekevu na usikivu ili
kusikia vizuri Mungu anasema nini. Katika sauti zote ambazo Maria angeweza kusikia
hapa duniani aliitegea sikio sauti ya Mungu na kwa kutii kwake ameokoka yeye, na sisi
tumepata kumjua Mungu.
Mtu mmoja alifananisha safari ya majilio kama mtu anayesafiri
na katika safari yake anaingia kwenye shimo refu. Kwa kawaida kama shimo ni refu na
huko mbele kuna mwanga basi kinachoonekana kwa mbali ni kamwanga kadogo sana. Unapokaribia
mwisho kabisa unaanza kuuona ukweli yaani mwanga wenyewe ambao mwanzoni ulikuwa kidogo.
Mfano huu uko wazi kwenye masomo yetu ya leo.
Katika somo la kwanza - tunasikia
habari ya maisha ya Waisraeli jangwani. Kila wanapokaribia kukata tamaa, Mwenyezi
Mungu anafanya jambo kubwa kwao. Na hata baadaye katika mazingira yao mapya, mapambano
yanaendelea. Halafu tunaona Daudi - analindwa na Mungu, anapata pumziko toka kwa Mungu,
toka pande zote, na hali ya utulivu waliyoahidiwa Waisraeli siku waliyoingojea inapatikana
– katika Kum 12:9 – Daudi sasa aweza kupumzika.
Mungu, anamfanya maarufu katika
ulimwengu huu. Nyumba yake na ufalme wake utakuwa hauna mwisho. Hata hivyo pamoja
na shida na matatizo yote ya Daudi, lakini ahadi ya Mungu inabaki palepale. Pamoja
na giza lote, mwishoni kuna mwanga wa Mungu.
Injili ni ushuhuda wa utimilifu
wa hiyo ahadi ya Mungu. Miaka hiyo mingi iliyopita inakamilika katika Maria. Huyu
Yesu, Mwana wa Mungu aliye hai anachukua nafasi ya Daudi baba yake na ufalme wake
utakuwa hauna mwisho. Katika 1 Kor 15,25 tunasoma hivi; maana sharti amiliki yeye
hata awaweke maadui wake wote chini ya miguu yake. Na katika Isa. 7,14 tunasoma hivi;
kwa hiyo Bwana mwenyewe atawapa ishara, tazama bikira atachukua mimba, atazaa mtoto
mwanamume naye atamwita jina lake Imanueli. Fiat ya Maria, yaani nitendewe ulivyonena
ni itikio la mwanadamu linalofanya hilo liwezekane leo. Unyenyekevu wake unamwokoa
yeye na sisi pia.
Katika somo la pili - Rum. 16:25 – tunaalikwa tufurahi pamoja
na Paulo mtume - sasa na atukuzwe yeye awezaye kuwafanya imara sawasawa na injili
yangu na kwa kuhubiriwa kwake Yesu Kristo. Hii ni imani inayookoa, inayofufua inayotia
uhai. Kwa kifupi katika somo hili tunaona kuwa Kristo anakamilisha ufunuo. Ni nini
maana yake kwetu? Au tunadaiwa nini sisi? Tunadaiwa utii wa imani, na upendo unaotuwajibisha
pamoja. Katika hilo tutapata uhuru wa kweli na ukombozi mkamilifu.
Yesu ndiye
ufunuo wa hiyo siri. Tukiwa bado katika fumbo hilo tunakumbushwa haja ya kuendelea
kusonga mbele kumwendea Bwana ili tukutane naye na azaliwe tena leo katika maisha
yetu.
Katika jumapili hii, tumekaribia mno kuona waziwazi ahadi za Mungu kiasi
kwamba tunamwona Bwana hapa mbele yetu. Tuangalie matayarisho mbalimbali tuliyofanya.
Tayari tunasikia habari ya kupashwa habari Bikira Maria kuwa atakuwa mama Mungu na
itikio lake na majukumu ya huyo Mungu ajaye atakuwa mfalme juu ya nyumba ya Yakobo
milele na bila mwisho.
Makutano ya Maria na malaika ni alama ya imani hai.
Imani ni zaidi ya kusoma kilichoandikwa au kusadikishwa tu. Ni makutano kati ya kinachoonekana
na kisichoonekana. Mt. Luis 1X wa Ufaransa, alikuwa akisaini hati za ofisi siyo
kama Mfalme Luis IX, ila kama Luis wa Poissy. Alipoulizwa sababu ya kufanya hivyo
alisema – Poissy ni mahali nilipobatizwa ila katika basilica la Rheims nilitawazwa
mfalme. Aliendelea kusema, nafikiria zaidi mahali nilipobatizwa kuliko pale nilipotawazwa
mfalme. Ni kitu kikubwa zaidi kuwa mtoto wa Mungu kuliko kujulikana kama mtawala.
Ubatizo wangu ni pasi ya kuingia utukufu wa milele lakini ufalme wangu utapotea mara
tu baada ya kifo.
Fumbo la Kristo linaokoa. Tuwajibishwe na ushuhuda huu ili
tuweze kuishi vizuri zaidi imani yetu. Mtakatifu Agustino anasema Maria aliyejaa neema
alimchukua Yesu katika moyo wake kabla ya kumchukua tumboni. Hakika sisi hatuwezi
kumzaa mwokozi. Kwanza tayari keshazaliwa. Twaweza kumwonesha hapa ulimwenguni kwa
kuwa watu wake Mungu. Mungu atuita kwanza kama Maria, halafu hutupatia utume fulani
wa kufanya. Tukijibu wito huo, twamwonesha Mungu hapa duniani. Ndilo jibu kubwa na
la pekee tuwezalo kumrudishia Mungu na watu wake tunaposherehekea sikuku ya Noeli
mwaka huu na wakati wote.
Angalia alichofanya Daudi kujenga ufalme, halafu
anatambua kuwa hajafanya mengi kwa ajili ya Mungu. Anataka kumjengea nyumba Mungu.
Katika somo la kwanza tunaona nabii Nathan anamwangalisha mfalme Daudi kuwa si yeye
atakayejenga nyumba ya Bwana, yaani hekalu, bali ni Mungu mwenyewe atakayemjengea
Daudi nyumba. Aidha Mungu anatambua mawazo na nia yake na anajenga yeye nyumba ya
ufalme wake.
Aidha tunatambua kuwa Mungu hahitaji nyumba ya kujengwa na mawe.
Yeye ahitaji kupokelewa nasi na kumshuhudia hapa ulimwenguni. Jambo zuri zaidi katika
ahadi hiyo ya Mungu ni kwamba huo ufalme mpya utatawala milele. Maagizo haya yanadokeza
kuwa katika kizazi chake atazaliwa mtoto wa pekee atakayependekezwa na Mungu. Uchaguzi
huu ni wa kwanza katika mfululizo wa maagizo juu ya masiya mwana wa Daudi - Isa: 7:14,
Mik. 5,1, Hag 2,3 na katika Agano Jipya – Mdo: 2,30 yanaeleza uchaguzi huu kuwa ni
Kristo.
Kwa mfano katika Mt. 12: 46-50 tunasoma habari juu ya jamaa za kweli
za Yesu. Jibu la Yesu litusaidie pia kutafakari mwito wa Yesu kwetu sisi. Yesu ategemea
wafuasi wake wawe si tu kaka na dada, bali wale wanaomshuhudia yeye na kushika Neno
lake. Mama yake pia katika Lk. 1,38 – anasema, tazama mimi ni mjakazi wa Bwana na
iwe kwangu kama ulivyosema, kisha malaika akaondoka akaenda zake. Hili jibu la Maria
ni zuri sana na linatupa changamoto sote kuwa tayari kutimiza mapenzi ya Mungu.
Angalia
alichofanya Maria - mimi ni mtumishi wa Bwana. Ujio wa Kristo ni ushindi dhidi ya
ulimwengu geugeu. Msimamo wa Mama Maria unaleta ukombozi kwa ulimwengu, pamoja na
Maria twaweza kuimba sifa ya Mungu - moyo wangu wamtukuza Bwana na roho yangu inafurahi
katika Mungu mwokozi wangu. Yeye daima aliendelea kukua katika imani.