Katika wakati huu, ambamo tunaekea kilele cha sikukuu ya kuzaliwa Bwana wetu Yesu
Kristo, Makala "Dunia Mama" kwa mara ingine, anawakaribisha kutafakari pamoja, heshima
na wito wa mwanamke kama mama. Nani kama Mama....ingawa mikono yake ni midogo na
nyororo, huduma yake ni kubwa na yenye nguvu za ajabu!i
Mwanamke ameumbwa
na asili ya kupenda.Huwapenda viumbe na kuvihudumia, kama tunavyoona katika maisha
yakila siku. Kwa mwanamke, kazi na huduma ni pete na chanda, kama ilivyokwisha
thibitishwa kisayansi pia kwamba, kuna tofauti kubwa katika hulka na hisia asilia,
kati ya mwanamke na mwanamme. Mwanamke kaumbwa na asili ya upendo wa kipekee katika
kuhudumia binadamu wengine. Mwanamke hutimiza wajibu huu, huhudumia kwa furaha,
hufurahia kubeba mimba kwa muda wa miezi tisa tumboni mwake matumaini, akivumilia
hali zote za masumbufu na kujinyima kwingi, akiwa amejawa na upendo na matumaini mapya,
ya kuongeza binadamu mwingine duniani. Ni maumbile ya ajabu aliyoumbwa nayo mwanamke.
Maumbile yaliyojaa upendo asili.
Na ndiyo maana, hushangaza sana pale linaposikika
tukio la Mama kumuua mtoto wake. Hata hivyo, ukichimba kwa ndani kiini cha matukio
mengi ya aina hiyo, utaona kwamba, ukatili huo ulilenga kusahihisha tabia ya mtoto
husika, mtoto aliye onekana kuwa na tabia sugu isiyompendeza mama katika mambo fulani
fulani. Mfano Mama kumchoma kwa moto mikono ya mtoto wake kwa sababu mtoto kaiba
nyama chunguni, au kadokoa mlo kabla ya wengine. Adhabu hiyo ya mama kwa mara nyingi
hulenga zaidi katika kurekebisha tabia ya mwanae , asije kuwa mwizi, au pengine mtoto
kutokuwa sikivu katika kufuata masharti na kanuni za kijamii. Kweli adhabu kama hizo,
hazifai,ni upendo unaopita kiasi, katika kurekebisha kasoro. Vitabu na Maandiko
Matakatifu ya Kanisa , tangu agano la kale, agano Jipya na nyaraka mbalimbali za Kitume
za Mapapa na Kanisa, mna maelezo ya kutosha juu ya heshima na wito wa mwanamke katika
kuwa Mama. Vyote huonyesha waziwazi juu ya heshima ya mwanamke katika maisha ya binadamu
na pia katika mpango wa wokovu wa Mungu kwa binadamu. Tunasoma katika Kitabu cha
Isaya juu ya utabiri wa kuzaliwa kwa Mkombozi na mwanamke “Tazama Bikira atachukua
Mimba atazaa mtoto mwanamme naye atamwita jina lake Emanueli” Is 7:14. Vivyo hivyo
imeandikwa katika Injili ya Matayo habari hii ya Mkombozi wa dunia kuzaliwa na mwanamke
, Mama Bikira Maria (tz Mt 1:22-23)”. Binti Mtukufu wa Sayuni aliye bora sana Mkingiwa
dhambi ya asili , nyakati zilipotimia kwa mpango wa wokovu kutimizwa , Mwana wa
Mungu alitwaa maumbile ya binadamu ili amkomboe binadamu katika dhambi zake kwa fumbo
la mwili wake.
Vivyo hivyo mafundisho ya Kanisa , kama ilivyoainishwa katika
Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican, yatuonyesha waziwazi juu ya huruma ya Mungu kwa
binadamu, iliyotufanikisha pia kuitwa wana wa Mungu, kupitia Mpango wake mtimilifu
wa kumwilisha mwanae pekee, nafsi ya pili ya Utatu Mtakatifu Yesu Kristo, ndani
ya tumbo la Mwanamke , aliyeteuliwa tangu milele, awe mama ili kwamba , kama vile
mwanamke alivyoshiriki katika mauti , kadhalika mwanamke asaidie kuuleta uzima. Kwa
namna ya pekee Mama wa Yesu anauzalia ulimwengu uzima wenyewe , yeye atengenezaye
yote upya , naye alitajirishwa na Mungu, karama za kustahili jukumu hili kubwa la
kumzaa mwana wa Mungu. Mwanamke anapata heshima hii katika asili yake ya kuwa na
upendo wa kuhudumu wengine. Mwanamke anakuwa katika kiini cha tukio hili la wokovu
kwa binadamu.
Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican unasema, Mungu kwa namna ya
kipekee alimshirikisha mwanamke katika siri hii ya uumbaji wa maisha , ndani ya tumbo
la mwanamke. Mwanamke mja mzito, anapata kujazwa na furaha ya ajabu ya maisha
haya mapya yanayokua polepole ndani mwake, na kwa hisi za kipekee huendelea kutambua
kinachoendelea ndani yake. Katika mwanga wa "mwanzo wa maisha ", mama anapokea na
kukipenda kama mtu, kiumbe kilicho ndani ya tumbo lake . Baba Mtakatifu Yohana
Paulo II katika waraka wake wa Hadhi ya Mwanamke,”Mulieris Dignitatem” akitazama
kwa makini utume wa wanawake katika Injili, aliandika kwamba, kwa mara nyingi wanawake
waliokutana au kuandamana na Yesu katika safari zake za kutangaza Habari njema ya
wokovu mijini na vijijini , walipata neema nyingi kutoka kwake. Yesu aliwataja wanawake
kama mfano katika kuupata ukweli juu ya ufalme wa Mungu. Tuna mifano ya sarafu iliyopotea
( Lk 15: 8-10), mfano wa chachu (Mt 13:33), mfano wa wasichana wenye busara na wapumbavu
(Mat 25: 1-13), mwanamke mjane , aliyetia sarafu mbili za shaba katika sanduku la
sadaka n.k. Katika mifano hiyo, Yesu anaonyesha heshima zake kwa wanawake hawa,
kama mfano wa kuigwa na kila mtu mwenye kuwa na imani. Na pia Yesu anaonyesha utetezi
kwa wanawake, wanaogandamizwa na mifumo ya kijamii na kisheria (Lk 18: 1-7).
Mtakatifu
Yohana Paulo 11 anaendelea kusema, katika mafundisho yote ya Yesu , tunaona kwamba,
kamwe Yesu hakuwa na ubaguzi dhidi ya wanawake. Kinyume chake, maneno yake na kazi
zake daima huonyesha heshima na sifa kwa wanawake. Wakati Yesu akitembea katika
njia yake ya Mateso kuelekea Golgotha, aliwageukia wanawake na kuwaambia, “enyi
binti wa Yerusalemu , msinililie mimi”, (Lk 23:28). Yesu anaonyesha huruma yake
kwa wanawake, hata wale waliokuwa wametenda dhambi , hakuwadharau au kuwabeza, lakini
kwa upole na unyenyekevu aliwataka wageuze maisha yao.
Mpendwa, kuna matukio
mengi tu yaliyotajwa katika Injili , ambamo tunaona wanawake wengi, wa umri tofauti,
maisha tofauti , wagonjwa, au mateso kimwili, waliokutana na Yesu, kama yule mwanamke
aliyegusa vazi la Yesu, au mama mkwe wa Simon , ambaye " alikuwa na homa amelala
kitandani ana homa kali, binti wa Yairo, mwanamke Mjane , mwanamke Mkanaani na
kadhalika. Matukio yote haya yanatuonyesha kwamba, imani na unyenyekevu na upendo
na ukuu wa roho aliyo nayo mwanamke hata katika safari ya maisha ya kiroho. Yesu
alimwambia mwanamke Mkanani , aliyemwita Yesu Unirehemu Bwana , binti yangu amepagwa
sana na pepo, Yesu alimjibu, Mama , imani yako ni kubwa , na iwe kwako kama utakavyo
(Mt 15:28).
Katika mwanga wa Injili , tunaona kwamba, mwanamke ameinuliwa
, si tu kimwili lakini kwa kila asikilizaye Neno la Mungu na kulishika , anapata hadhi
ya kuitwa pia mwana wa Mungu. Kwa hiyo historia ya binadamu, kupitia uzao wa mwanamke
, daima inakuwa na uhusiano na Mkataba na Mungu, kwa njia ya Mama wa Mungu.
Katika
Injili ya Yohane 1: 12 imeandikwa , bali wote walio mpokea aliwapa uwezo wa kufanyika
watoto wa Mungu , ndio wale waliaminio jina lake, waliozaliwa si kwa damu wala si
kwa mapenzi ya mwili wala mapenzi ya Mtu, bali kwa Mungu. Na pia katika waraka wa
Mtume Paulo kwa Warumi, ameandikwa, historia ya kila mwanadamu inapitia katika nguzo
hii ya mwanamke, kwenye siri ya kuitwa watoto wa Mungu (Rum 8: 19).
Kwa maelezo
hayo, Dunia Mama anatoa mwaliko , kwetu sote, tutazame maisha yetu ya kawaida mahali
popote tulipo, tulinganishe mahangaiko ya kuhudumia ndani ya familia, kati ya baba
na mama . Ukweli ni kwamba Mama daima hutumia muda wake kuihudumia familia katika
mambo ya kawaida madogomadogo lakini msingi sana katika maisha ya kawaida ya familia.
Utaona ni kweli mwanamke kazaliwa na upendo wa ajabu katika kuhudumia wengine. Tazama
jinsi anavyo hangaika kuhakikisha familia inapata mlo wake wa kila siku tena kwa
wakati waliouzoea. Tazama jinsi mama anahudumia watoto na wagonjwa. Tazama jinsi
wanavyowainamia wasiojiweza, na kuwapa kila msaada wanaohitaji? Mikono yake midogo
na laini, muda wote ikijishughulisha na utoaji wa huduma, na zaidi huwa wakati wa
madhimisho ya Siku Kuu kana hii ya ya Noel , anahangaika huko na kule, walau siku
hiyo, mazingira ya familia yapendeze, watoto wavae vizuri , wapate mlo tofauti na
siku zote,angalau pilau na chapati zisikosekane.
Mpendwa ,tafakari yetu
haina maana ya kusahau ukarimu na wema wa Baba, lakini basi ni mwaliko wa kutathimini
kwa makini heshima ya Mwanamke ndani ya Familia, kama ufunguo wa maisha bora. Dunia
Mama leo hii, inawasihi nyote katika Siku Kuu hii ya Noel, tunapo mpongeza Mama Maria
kwa kutuzalia Mtoto Yesu, Mkombozi wetu , basi pia tusisahau kununua zawadi hata
kama ni dogo tu , kwa ajili ya kumpongeza mama nyumbani , kwa huduma yake ya kila
siku, inayotuwezesha kusonga mbele na Maisha. Jamani nani Kama Mama! Tumheshimu
na kumpa upendo wote kwani ni mastahili yake.