Papa Francisko ni mjenzi wa madaraja yanayowaunganisha watu!
Askofu mkuu Thomas Wenski wa Jimbo kuu la Miami, Marekani amewapongeza Marais wa Marekani
na Cuba kwa kufanya maamuzi makubwa kwa kurejesha tena uhusiano wa kidiplomasia baina
ya nchi hizi mbili; tukio ambalo linaacha kumbu kumbu ya kudumu katika maisha ya watu.
Marais wa Cuba na Marekani wanapongeza jitihada za makusudi zilizofanywa na
Baba Mtakatifu Francisko ambaye amejielekeza zaidi katika ujenzi wa madaraja yanayowakutanisha
na kuwaunganisha watu kwa ajili ya ustawi na maendeleo yao: kiroho na kimwili.
Baba
Mtakatifu Francisko amekuwa ni mjumbe na chombo cha amani na majadiliano kati ya watu,
kama ilivyokuwa kwa Mtakatifu Francisko wa Assisi. Kanisa Katoliki kwa miaka mingi
limekuwa likipinga vikwazo vya uchumi dhidi ya Cuba kwamba, vilikuwa vimepitwa na
wakati.
Ni matumaini ya Askofu mkuu Wenski kwamba, Serikali ya Cuba itaendeleza
mchakato wa maboresho ya mahusiano ya kidiplomasia na Marekani, kwa kujikita katika
kulinda, kutetea na kudumisha haki msingi za binadamu pamoja na demokrasia. Rais Barack
Obama wa Marekani amesikika akisema kwamba, kuombea Cuba ianguke si siasa njema, kwani
Cuba inahitaji kufanya mabadiliko yatakayowakirimia wananchi wake matumaini, amani
na maendeleo ya kudumu.