Watawa na ujenzi wa utamaduni wa kusikilizana kwa makini!
Baraza la Kipapa la Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume, Jumanne, tarehe 16 Desemba
2014 limezindua taarifa ya kazi ya kitume iliyofanywa kwenye Mashirika ya Kitawa na
Kazi za Kitume yenye hadhi ya Kipapa na Kijimbo nchini Marekani kwa kuwahusisha watawa
wengi kuanzia mwaka 2009 hadi mwaka 2012.
Taarifa hii imewasilishwa kwa waandishi
wa habari mjini Vatican na Kardinali Joao Braz de Avis, Rais wa Baraza la Kipapa la
Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume pamoja na viongozi waandamizi kutoka katika
Baraza na Mashirika ya Kitawa na kazi za kitume. Mkutano huu umehudhuriwa pia na viongozi
wa watawa kutoka Marekani. Watawa wamepewa kwa mara nyingine tena fursa ya kugundua
ndani mwao mpango wa kazi ya ukombozi na matunda ya mawasiliano kati ya watawa, viongozi
wa Kanisa na waamini walei.
Majadiliano ya kina yanayoendelea kati ya watawa
yanapania kuimarisha na kudumisha uaminifu wao kwa Kristo na Kanisa mintarafu karama
za waanzilishi wa Mashirika yao. Kardinali De Avis anasikitika kusema kwamba, kuna
baadhi ya Mashirika ya kitawa yalikataa kuonesha ushirikiano, ingawa bado kuna nafasi
ya kuendeleza majadiliano katika ukweli, uwazi na heshima kwa mashirika kama haya!
Baraza
la Kipapa la Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume linaendelea kufanyia kazi mapendekezo
yaliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko kwa kuhakikisha kwamba, watawa wanashirikishwa
kikamilifu katika mchakato wa kujadili, kuamua na kutekeleza masuala yanayohusu maisha
na utume wa watawa ndani ya Kanisa. Maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani ni fursa
nyingine ya kujipatanisha, ili watawa waweze kuwa kweli ni mashuhuda angavu, wanaoonesha
mvuto na mashiko katika umoja na udugu.
Kwa upande wake Askofu mkuu Rodriguez
Carballo, Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume
amefafanua kwamba, Mashirika yaliyohusika zaidi ni yale yanayotekeleza wito na utume
wake nchini Marekani kwa kuwa na Makao yake makuu; Makao makuu ya kanda au nyumba
ya malezi na kwamba, jumla ya Mashirika 405 yametembelewa na kukaguliwa na Sr. Mary
Clare Millea, kiongozi wa kitume aliyekuwa ameteuliwa na Baraza la Kipapa kutekeleza
dhamana hii kwa kushirikiana na jopo la watawa.
Jopo hili limefanya upembuzi
yakinifu kuhusiana na uelewa kuhusu maisha ya kitawa na kazi za kitume nchini Marekani
mintarafu majadiliano ya kina. Utamaduni wa kusikiliza watawa kwa makini ni kati ya
mambo yaliyopewa kipaumbele cha pekee katika utekelezaji wa dhamana hii, ili kutambua
utajiri wa urithi wao, changamoto zilizopo, matumaini yao kwa siku za usoni na mazingira
ya maisha na utume wa Kanisa mahalia!
Ukaguzi huu umefanyika katika hatua kuu
nne: kwa kufanya majadiliano ya kina na wakuu wa Mashirika ya kitawa na kazi za kitume
na baadaye wakuu wa Mashirika walipewa dhamana ya kujaza taarifa kuhusiana na ubora
wa maisha ya kitawa, kijumuiya na kitume kwa kila mtawa. Sr. Millea amewasilisha taarifa
ya jumla kuhusiana na Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume nchini Marekani: kuhusiana
na mwelekeo wa Mashirika haya.
Hii imekuwa ni fursa ya kukuza na kudumisha
majadiliano, umoja na udugu kati ya watawa, viongozi wa Kanisa na waamini walei na
wengi wa wakuu wa Mashirika ya kitawa wamekubaliana kimsingi na upembuzi yakinifu
uliofanywa na Jopo hili. Watawa wamechunguza dhamiri zao mbele ya Neno la Mungu; majadiliano
ya maisha ya kiroho mintarafu maisha, ushuhuda na utajiri kutoka kwa waanzilishi wa
Mashirika haya bila kusahau mchango wao katika nyaraka mbali mbali za Kanisa.
Watawa
wanakiri kwamba, kumekuwepo na mshikamano wa dhati kati ya watawa wa kike na upendo
wa kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake; mambo yanayooneshwa
pia na wakleri pamoja na waamini. Watawa wanaendelea kuhamasishwa kuchangia kwa hali
na mali utajiri mkubwa walionao watawa katika Mashirika yao, kwa ajili ya ustawi,
maendeleo na huduma kwa Kanisa. Watawa wanasema, wataendelea kushikamana kulinda na
kutetea utu na heshima ya binadamu; kwa kukuza uhuru wa kidini na kidhamiri.
Na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.