Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili IV ya Kipindi cha Majilio
Ni mara nyingine tena tunakutana kushirikishana furaha na mapendo ya Mungu kwa njia
ya Neno lake. Ni Dominika ya nne ya Majilio, tunapoelekea sherehe za Noeli, sherehe
za kuzaliwa Mtoto Yesu, Mtoto Emanueli yaani Mungu pamoja nasi. Katika masomo ya Misa,
Dominika ya nne tunapata ujumbe ukituambia kuwa, Yesu ndiye Masiya wa kweli tuliyehaidiwa
tangu zama za mababu zetu.
Katika somo
la kwanza kutoka kitabu cha pili cha Samweli tunapata ujumbe wa kuzaliwa kwa Yesu
Kristo katika ukoo wa Daudi na kwa jinsi hiyo ukoo wa Daudi utatawala milele. Mfalme
Daudi anawaza kumjengea nyumba mwenyezi Mungu lakini badala yake Mungu anamwambia
Nabii Nathani akamwambie Daudi kuwa yeye hawezi kumjengea nyumba Mungu, bali Mungu
mwenyewe atamjengea nyumba Daudi.
Ndiyo kusema katika ukoo wa Daudi atazaliwa
Mwana wa Mungu. Na hivi ukoo huu utakuwa na jina kuu kupita majina mengine na mwisho
nyumba ya Daudi na ufalme wake vitathibitishwa milele. Habari hii haiwezi kuwa habari
ya kawaida bali kuzaliwa kwa Masiya, Mkombozi wa ulimwengu.
Ni katika mantiki
hiyo ya kukuzwa kwa ufalme wa Daudi yaani kuzaliwa Masiya, Mtume Paulo anatoa shukrani
kwa Mungu kwa zawadi hiyo kubwa ya kumpata mkombozi. Anawakumbusha Warumi wamtukuze
yeye tu, ambaye huwafanya imara, aliye hekima kamilifu peke yake. Kwa jinsi hiyo,
atuonya nasi daima kumtukuza Mungu na kumpa sifa, yeye peke yake na aliye mweza wa
yote.
Mwinjili Luka anakaza ujumbe tunaoupata katika somo la kwanza. Tunamwona
malaika Gabrieli akipeleka ujumbe wa Mungu kwa mwanamwali Bikira Maria kwamba atamzaa
Mwana wa Mungu. Mwanamwali huyu alikuwa ameposwa na Yusufu wa ukoo wa Daudi. Anashangaa
habari ya malaika Gabrieli, lakini kwa neema ya Mungu anaitika: Nitendewe kama ulivyonena.
Mungu anamjengea nyumba mfalme Daudi na ufalme wake na nyumba yake vinathibitishwa
milele.
Kumbe sasa ufalme wa Daudi uliokuwa wa muda unachukuliwa na mfalme
mwenyewe wa milele aliyekuwa amempa mfalme Daudi kutawala kwa muda, Mfalme huyu ni
Kristu Masiya. Mpendwa, ni kwa mantiki ya ufalme mpya nasi tunaalikwa kujiweka katika
ufalme huo na si tu kujiingiza huko tu, bali kujiachia kuongozwa na ufalme huo yaani
Yesu Kristo Mkombozi, dira na kiongozi wa ulimwengu mpya.
Mpendwa, habari hii
ya furaha ni kwa ajili yako, malaika anapiga hodi kwako kila mara akisema utampokea
Bwana katika Ekaristi takatifu! Yakupasa kuitikia ukisema nitendewe kama unavyotaka!
Habari ya furaha ya kuzaliwa Masiya umeipata tangu Dominika ya I ya Majilio na ukaendelea
nayo mpaka sasa! Unasemaje? Mimi nasema Bwana nitendewe kama ulivyonena, njoo Masiya
ukae nasi, njoo ukatuokoe, ushukie Masiya kuwaokoa watumwao! Emanueli kaa nasi Bwana.
Ninakualikeni
kumpenda Mama Bikira Maria ambaye alikuwa Tabernakulo ya kwanza akimbeba mtukuka Mwana
wa Mungu, mkombozi wa ulimwengu. Ni kwa njia ya Bikira Maria mtoto Emanueli, mkate
wa Mbinguni umetufikia.
Tumsifu Yesu Kristo na Maria.
Tafakari hii
imeletwa kwako na Padre Richard Tiganya, C.PP.S.