Wakatoliki nchini Uingereza wameamua kujitosa kimasomaso katika mchakato wa Uinjilishaji
mpya!
Kardinali Vincent Nichols, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Uingereza na Wales
anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema, kuunga mkono changamoto inayotolewa
na Baba Mtakatifu Francisko kwa kujikita katika mchakato wa Uinjilishaji, kwa kuwatangazia
Watu wa Mataifa, Injili ya Furaha.
Wakristo wote wanapaswa kushiriki kikamilifu
katika azma ya Uinjilishaji kwani hii ni sehemu ya wajibu wao msingi. Lengo ni kuwawezesha
Wakristo kutekeleza wajibu wao wa Kimissionari kwa njia ya ushuhuda wa maisha adili
na yenye mvuto. Parokia ishirini na mbili zimetengwa maalum ili kuhamasisha waamini
kushiriki katika mradi huu mkubwa wa Uinjilishaji kwa ajili ya Mwaka 2015.
Watu
wana kiu ya kusikiliza Neno la Mungu sanjari na kuonjeshwa imani inayojikita katika
matendo. Maaskofu wanataka kutekeleza kwa matendo changamoto inayotolewa na Baba Mtakatifu
Francisko katika Waraka wake wa kichungaji, Injili ya Furaha, kwa kujikita katika
dhamana ya Uinjilishaji, ili kuwashirikisha watu furaha inayobubujika kutoka kwa Kristo
na Kanisa lake.
Tarehe 11 Julai 2015 kutafanyika mkesha wa sala na kongamano
la kitaifa kuhusu Uinjilishaji mpya! Waraka wa Injili ya Furaha ni dira na mwelekeo
mpya unaotolewa na Baba Mtakatifu Francisko katika mchakato wa Uinjilishaji mpya,
kwa kujitahidi kukutana na Yesu katika uhalisia wa maisha ya kila siku.
Parokia
mbali mbali zinapania kuwashirikisha waamini walei ili kuunda kikosi kazi kitakachohamasisha
mchakato wa Uinjilishaji mpya, mwaliko na changamoto kwa waamini kushiriki kikamilifu
katika mradi huu mkubwa, kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa.