Yesu Kristo ni chemchemi ya furaha ya kweli kwa mwanadamu!
Kipindi cha Majilio ni wakati muafaka wa kujiandaa kikamilifu katika maisha ya kiroho
kwa ajili ya ujio wa Yesu Kristo na kwa namna ya pekee, kukiishi kipindi hiki kwa
kuwa ni watu wenye furaha inayobubujika kutoka kwa Yesu, kwani kwa Yesu, furaha imefika
nyumbani na wala hakuna mchezo!
Binadamu anahitaji kuonjeshwa furaha na kwamba,
Mkristo anaalikwa na Mama Kanisa kuhakikisha kwamba, anaishuhudia furaha kwa kuwa
karibu na Mwenyezi Mungu ambaye yuko daima katika maisha ya waja wake. Kwa njia ya
Fumbo la Umwilisho, mwanadamu amepata mbegu ya uwepo wa Ufalme wa Mungu, changamoto
na mwaliko wa kuwaonesha wengine ile furaha inayobubujika kutoka kwa Kristo na utimilifu
wa furaha hii ni katika maisha yenye uzima wa milele!
Hii ni sehemu ya tafakari
iliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko, wakati wa Sala ya Malaika wa Bwana, kwenye
Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, Jumapili tarehe 14 Desemba
2014. Baba Mtakatifu anasema, Yesu Kristo ni chemchemi ya furaha ya watu wake na kwamba,
bila Yesu, hakuna furaha ya kweli, kwani Yesu aliyeteseka, akafa na kufufuka anaendelea
kutenda kazi katika maisha na utume wa Kanisa kwa njia Neno la Mungu na Sakramenti
za Kanisa.
Wakristo wanahamasishwa na Mama Kanisa kuhakikisha kwamba, wanapokea
na kukumbatia ndani mwao, uwepo endelevu wa Mungu kati yao sanjari na kuwasaidia wengine
kuonja uwepo huo wa Mungu kati yao kama alivyofanya Yohane Mbatizaji. Waamini wawaongoze
watu kumwendea Yesu kwani yeye ndiye lengo kuu la maisha kwa binadamu anayetafuta
furaha ya kweli.
Baba Mtakatifu anasema, waamini wanaweza kuwa kweli ni Wamissionari
wa Furaha kwa kusali bila kuchoka; kwa kumwomba Roho Mtakatifu; kwa kutafuta mema
na kuachana na mabaya. Ikiwa kama huu ndio mtindo na mfumo wa maisha, basi hapana
shaka kwamba, Habari Njema ya Wokovu inaweza kuingia katika Familia na kuwasaidia
watu wengi zaidi, ili kupata amani na utulivu wa ndani hapa pale wanapoelemewa na
magumu katika maisha.
Baba Mtakatifu anawataka waamini kuonesha uso wa furaha
na tabasamu, kwani ndani mwao kuna chemchemi ya amani na utulivu, hata wakati wa shida
na magumu katika maisha na kwamba, imani si kizuizi cha shida! Lakini jambo la msingi
ni kutambua kwamba, katika mahangaiko yote haya, bado Mwenyezi Mungu yupo pamoja na
wajawake. Mungu ndiye anayewakirimia watoto wake amani.
Waamini wanachangamotishwa
na Mama Kanisa kuhakikisha kwamba, wanamshuhudia Kristo, Neno wa Mungu, anayeyaangazia
mapito ya mwanadamu; kwa kuangalia matendo yanayoadhimishwa kwa njia ya Sakramenti
za Kanisa, kama kielelezo cha faraja na upendo kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwa kila
binadamu. Bikira Maria anasema Baba Mtakatifu Francisko ni sababu ya furaha ya waamini,
anayewasaidia kuondokana na utumwa wa maisha ndani na nje ya binadamu.
Baba
Mtakatifu Francisko mara baada ya Sala ya Malaika wa Bwana aliwapongeza watoto, familia
na vyama vya kitume vilivyokuwa vimekusanyika kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu
Petro kwa ajili ya kubariki Sanam za Mtoto Yesu, zitakazowekwa kwenye mapango yaliyoandaliwa
kwenye familia na parokia. Amewatakia heri na baraka tele katika Maadhimisho ya Siku
kuu ya Noeli na kwamba, wanaposali mbele ya Pango la Mtoto Yesu, wamkumbuke hata yeye
katika sala zao.
Ni muhimu sana ikiwa kama wanafamilia watapata nafasi ya
kujitenga na mambo ya dunia, ili kupata muda wa kusali. Ndiyo maana Baba Mtakatifu
ameamua kuwazawadia waamini na watu wote wenye mapenzi mema waliofika kwenye Uwanja
wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, Jumapili tarehe 14 Desemba 2014, kuwapatia
zawadi ya kitabu cha sala kwa ajili ya matukio mbali mbali ya maisha, ili kuitakatifuza
siku kwa kuzungumza na Mwenyezi Mungu, ili kweli furaha ya Yesu iweze kupata makazi
yake kati ya watu!
Baba Mtakatifu Francisko amelipongeza Kanisa nchini Poland
wanapoadhimisha Mwaka wa Upendo, kama kielelezo cha mshikamano wa kidugu kwa kuwasha
mishumaa.
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio
Vatican.