2014-12-15 09:00:41

Tafuteni furaha ya kweli katika: Sala, Neno la Mungu na katika Matendo ya Huruma!


Jumapili ya tatu ya Kipindi cha Majilio ni mwaliko kwa Wakristo kushuhudia furaha inayopata chimbuko lake kutoka kwa Kristo; furaha ambayo inapaswa kumwilishwa kila siku katika maisha ya Mkristo, kwani hii ni furaha inayomkirimia mwamini: utulivu wa ndani na amani ya kudumu, hata pale anapokumbana na vizingiti vya maisha, kwani amani ni zawadi kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu, inayomwajibisha binadamu.

Mtakatifu Paulo anawaalika Wakristo kuwa daima ni watu wa furaha kwa kusali ili kuomba, kushukuru, kutukuza na kusifu. Wakristo watambue kwamba, wanatumwa kuwatangazia Watu wa Mataifa Habari Njema ya Wokovu kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao.

Wakristo wamepakwa mafuta ili kuwahubiri wanyenyekevu Habari Njema; kuwaganga waliovunjika moyo, kuwatangazia mateka uhuru wao na wafungwa kufunguliwa kwao pamoja na kutangaza Mwaka wa Bwana. Huu ndio wito ambao Wakristo wanapaswa kuufanyia kazi, ili kuwamegea wengine furaha inayobubujika kutoka kwa Kristo!

Hii ni sehemu ya mahubiri yaliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko, Jumapili jioni wakati alipofanya hija ya kichungaji kwenye Parokia ya Mtakatifu Yosefu iliyoko Aurelio, Jimbo kuu la Roma. Anasema, furaha ya Mkristo ijikite katika: Sala na Tafakari ya Neno la Mungu pamoja na kumwilisha ujumbe huu katika matendo ya huruma. Waamini wajenge utamaduni wa kumshukuru Mungu kwani amewajalia zawadi kubwa ya imani, wanayopaswa kuwashirikisha wengine kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao.

Baba Mtakatifu mwishoni mwa hija yake ya kichungaji Parokiani hapo amekutana na kusalimiana na wananchi wanaoishi katika mazingira magumu, ili kuwatia moyo wasikate tamaa!







All the contents on this site are copyrighted ©.