Mshikamano wa dhati kutoka kwa Papa Francisko kwa wagonjwa wa Ebola!
Kardinali Peter Turkson, Rais wa Baraza la Kipapa la haki na amani, kuanzia tarehe
16 Desemba, 2014 anafanya hija ya upendo na mshikamano kwa wananchi wa Sierra Leone
na tarehe 18 Desemba 2014 anatarajiwa kuwa nchini Liberia, mataifa ambayo yameathirika
vibaya sana kutokana na kukumbwa kwa janga la Ebola!
Takwimu za Shirika la
Afya Duniani, WHO, zinaonesha kwamba, kuna zaidi ya watu 18, 000 ambao wameambukizwa
Virusi vya Ebola. Zaidi ya wagonjwa 6, 500 wamekwishafariki dunia kutokana na ugonjwa
huu huko Afrika Magharibi. Hija hii ya mshikamano kutoka kwa Baba Mtakatifu Francisko,
inapania kuwatia shime na matumaini wadau wote ambao wanaendelea kupambana na ugonjwa
huu wa hatari pasi na kukata tamaa.
Kardinali Peter Turkson katika hija hii
anaambatana na Monsinyo Robert J. Vitillo, Mshauri mkuu wa masuala ya afya kutoka
Shirikisho la Mashirika ya Misaada ya Kanisa Katoliki Kimataifa, Caritas Internationalis.
Kanisa Katoliki Afrika Magharibi ni kati ya wadau wakuu ambao wameendelea kutoa msaada
wa hali na mali kwa waathirika wa ugonjwa wa Ebola ambao umesababisha pia athari kubwa
katika masuala ya kiuchumi, kijamii na kisiasa. Kuna kundi kubwa la watoto wanaoishi
katika mazingira hatarishi kutokana na kuondokewa na wazazi pamoja na walezi wao.
Kardinali
Turkson anasema, kuna haja ya kuisaidia mihimili ya shughuli za kichungaji Afrika
Magharibi ili kuweza kutekeleza kikamilifu dhamana na utume wao kwa wagonjwa wa Ebola,
kwa kuzingatia kanuni na mwongozo wa huduma kwa wagonjwa wa Ebola.
Baba Mtakatifu
kwa nyakati mbali mbali ameonesha kuguswa na mateso pamoja na mahangaiko ya wagonjwa
wa Ebola Afrika Magharibi, ndiyo maana wakati huu anapenda kumtuma Kardinali Peter
Turkson, ili kuwatembelea watu walioathirika na ugonjwa wa Ebola, ili kuonesha mshikamano
wake wa karibu. Anawashukuru na kuwapongeza wahudumu wa sekta ya afya wanaoendelea
kutolea maisha yao kwa ajili ya kuwahudumia wagonjwa wa Ebola huko Afrika Magharibi.